Na Alex Sonna, Dodoma.

Mbunge wa Kwela kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Mhe.Deus Sangu ameishauri Serikali kuunda tume kwa ajili ya kuchunguza unyanyasaji unaofanywa na Askari wa Jeshi la Magereza Mollo Sumbawanga kuhusu tamko la Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi la kutoa shamba lenye ukubwa wa Ekari 495 kwa wananchi wa vijiji vya Msanda Muungano, Songambele na Sikaungu

Katika maswali yake ya nyongeza bungeni wakati wa maswali na majibu, Mhe. Sangu amebainisha kuwa Jeshi la Magereza linasema halijapata barua rasmi kutoka Wizarani.

“Tamko hili limesababisha askari Magereza sasa kuingia mgogoro na wananchi na kuwapiga na juzi mama mmoja amepigwa na kugalagazwa kwenye matope, je,Wizara ipo tayari kuunda tume kuchunguza manyanyaso haya na itakapobainika hatua za kisheria zichukuliwe ili iwe fundisho kwa wengine,” amesema.

Aidha ameiomba Serikali kutimiza ahadi ya kukabidhi shamba lililokuwa limechukuliwa na Jeshi la Magereza Mollo Sumbawanga kwa wananchi na Waziri wa Mambo ya ndani kwa wakati huo aliahidi kukabidhi shamba hilo kwa wananchi.

Akijibu swali hilo Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamza Khamis Khamis, amesema Wizara itachunguza na ikibainika kuna watu wanahusika hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Aidha amebainisha kuwa Jeshi hilo na wananchi wa vijiji hivyo walikuwa na mgogoro ambao ulimalizwa Mwaka 2019 kwa Serikali kutoa eneo la ekari 1,800 kwa lengo la kumaliza mgogoro huo.

Amesema kuwa hitaji la ekari 495 ni dai jipya ambalo Wizara kwa kushirikiana na Jeshi la Magereza na Ofisi ya Mkoa wa Rukwa litaendelea kulifanyia kazi.

Share To:

TANGA RAHA BLOG

Post A Comment: