Happy Lazaro,Arusha.
Arusha.Mwanasheria mkuu wa serikali Adelardus Kilangi amevitaka vyuo vikuu nchini kuwaandaa Vijana kulingana na mahitaji ya soko la ajira ili kuweza kuondokana na changamoto ya kukaa mitaani pindi watakapohitimu .
Aliyasema hayo Jana wakati akizungumza katika mahafali ya nne ya chuo kikuu cha mtakatifu Augustine Tanzania tawi la Arusha ambapo jumla ya wanafunzi 498 walihitimu kozi mbalimbali.
Kilangi alisema kuwa,umefika wakati Sasa wa vyuo vikuu kuhakikisha vinawaandaa Vijana kulingana na mahitaji ya soko ili waweze kupata ajira kwa haraka pindi watakapohitimu .
"Mimi naviomba vyuo kuanza kujiuliza kwa nini vijana wanaomaliza hawajiajiri ama kuajiriwa kwa kuzifuata fursa mbalimbali zilizopo nchini ikiwemo kwenye sekta ya kilimo jambo ambalo wanatakiwa kulitatua ili kuleta mabadiliko."alisema .
Alisema kuwa ,wahitimu wanapaswa kuangalia ni kwa jinsi gani watazitambua na kuzitumia fursa mbali mbali za kukuza maendeleo ya nchi kwa kutumia taaluma zao na kuwa washindani katika soko la ajira kwa kufungua fursa za kujiajiri wenyewe.
“tumieni muda wenu na elimu mliyoipata kuzitafuta fursa katika mitandao ya kijamii na kuacha kutumia mitandao hiyo kwa mambo yasiyofaa kwa kuwa soko kubwa lipo ndani ya mitandao hiyo”alisema Kilangi.
Awali Mkuu wa wilaya ya Arusha Fabian Daqarro alivitaka vyuo mbalimbali kuandaa mitaala ya masomo kulingana na mahitaji ya soko la ajira ndani na nje ya nchi na hiyo itapunguza changamoto ya Vijana wengi kukaa mitihani kwa muda mrefu wakisaka ajira.
Kwa upande wake Askofu Mkuu wa jimbo kuu katoliki Arusha ,Isaack Amani alisema kuwa,katika kipindi hiki ambacho Kuna changamoto kubwa ya ajira hususani kwa Vijana Kuna umuhimu mkubwa kwa wahitimu hao kutanguliza weledi na nidhamu mbele ili waweze kukabiliana na ushindani uliopo.
Aidha aliwataka wahitimu watumie talanta zao na vipawa kusukuma maendeleo ya Taifa mbele huku wakiendana na dhana ya uchumi wa viwanda .
Naye Mkurugenzi wa chuo hicho cha Arusha,Charles Rufyiliza alisema kuwa, kuna dhana imejengeka kuwa wanao soma vyuo vya binafsi hawapati mikopo kutoka Serikalini dhana hiyo sio kweli kwani wanafunzi walioomba mikopo mwaka huu pesa zao zimefika kabla wao hawajaripoti chuoni.
Nao baadhi ya wahitimu, Nashukuru Sanga na Freedom Kishokera walisema kuwa, watatumia elimu waliyoipata kujiajiri na kutumia fursa za ajira zilizopo ndani na nje ya nchi.
Mwisho.
Post A Comment: