Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nauye amezikumbusha taasisi za TANROAD na TARURA kuweka majina ya barabara ili kurahisisha Operesheni ya Anwani za Makazi

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua mwenendo wa utekelezaji wa Operesheni hiyo Mkoani Kilimanjaro, Waziri Nape amesisitiza kuwa iko hatari ya ukiritimba unaoweza kufanywa na baadhi ya watu kwa kujiita majina ya mitaa yote na barabara kwa kigezo cha kuchangia fedha za utekelezaji wa zoezi la uwekeji wa Anwani za Makazi.

"Haya ni maelekezo yaliyotolewa na Waziri Mkuu kwamba TANROAD  na TARURA kwasababu barabara zote ni za kwao wahakikishe wanaweka majina ya hizi barabara ili isaidie kasi ya kukamilisha zoezi hili na mie naomba niwakumbushe watekeleze maelekezo kwa kuweka majina ya hizi barabara ili kuzipunguzia mzigo halmashauri na kuongeza kasi ya utekelezaji wa operesheni ." Amesema Waziri huyo

Ameongeza kuwa, viongozi na wananchi wanatakiwa kuwa makini katika kuweka majina ya mitaa kwa kuwa kuna wadau wanajitolea, wanachangia fedha zao lakini ni vizuri majina yawe yenye uzalendo na yanayoendana na uhalisia wa nchi yetu yakiwemo majina ya viongozi  pamoja na watu mashuhuri.

Katika hatua nyingine, Waziri Nape ameonesha kuridhishwa na kasi ya utekelezaji wa operesheni hiyo katika Mkoa wa Kilimanjaro ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia 99.1.

Share To:

Post A Comment: