Mkuu wa Wilaya ya Monduli Mhe.Frank Mwaisumbe akizungumza katika kuadhimisha Siku ya Viwango Afrika leo Machi 31, 2022 mkoani Arusha.

Baadhi ya wadau wa viwango wakiwa katika hafla kuadhimisha Siku ya Viwango Afrika kitaifa leo Machi 31,2022 Jijini Arusha.

***********************

NA MWANDISHI WETU

WAJASIRIAMALI wadogo na wa kati wametakiwa kutumia huduma zinazotolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) ili kukuza ubora wa bidhaa na huduma zao na kujihakikishia kuingia katika masoko ya ndani, ya kikanda na ya kimataifa na hatimaye kuchangia katika ustawi wa kijamii na kiuchumi wa taifa.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Monduli Mhe.Frank Mwaisumbe katika kuadhimisha Siku ya Viwango Afrika leo Machi 31, 2022 mkoani Arusha.

Amesema kazi inayofanywa na TBS kwa kushirikiana na Shirika la Viwango barani Afrika (ARSO) na taasisi nyingine za kimataifa katika utayarishaji wa viwango vya kimataifa husaidia kuhakikisha usalama wa afya na mali, ulinzi wa mazingira na elimu kwa umma.

Aidha Mhe. Mwaisumbe amesema kuwa Matumizi ya viwango vya Kimataifa husaidia kuondoa vikwazo katika biashara baina ya nchi tajiri na maskini, hivyo kusaidia kuboresha uchumi wa taifa na maisha ya wananchi kwa ujumla.

"Tusipozidi kusonga mbele, kazi ya TBS kwa kushirikiana na taasisi za kimataifa za viwango itaendelea kusaidia katika maendeleo ya teknolojia mpya ambazo zitachochea maendeleo ya uchumi wetu, hivyo kuchangia katika ustawi wa Watanzania". Amesema DC Mwaisumbe.

Pamoja na hayo Mhe.Mwaisumbe ametoa wito kwa TBS kuongeza juhudi katika kuwianisha viwango katika ngazi za kikanda na pia kushiriiki kikamilifu katika michakato ya kutayarisha viwango vya kimataifa ili kuziwezesha bidhaa na huduma za Tanzania kupenya kirahisi katika masoko ya kikanda na kimataifa.
Share To:

emmanuel mbatilo

Post A Comment: