Waziri wa Madini, Dkt. Doto Biteko amewaagiza Mkuu wa Wilaya ya Bunda,  Afisa Madini Mkazi na Katibu Tawala wa Mkoa kuhakikisha wanafungua Soko la Madini wilayani  Bunda Mkoa wa Mara ili kuwarahisishia wachimbaji na  wafanyabiashara wa madini kupata huduma hiyo karibu.


Agizo hilo amelitoa leo Desemba 28, 2021 wakati akizungumza na wachimbaji katika eneo la Kinyambwiga lililopo Kata ya Guta wilayani Bunda mkoani Mara.

Dkt. Biteko amesema kuwa, haiwezekeni mchimbaji ana dhahabu yake mfukoni anaenda hadi Musoma kutafuta soko.

Amesema, ni lazima soko la madini lianzishwe Bunda ili watu wafanye biashara ya madini kwa urahisi.

"Natoa agizo kwa Mkuu wa Wilaya, Afisa Madini na Katibu Tawala wa Mkoa ambaye kwa mujibu wa kanuni ya uanzishwaji wa masoko ya madini ndiye mwenye kutafuta eneo sahihi ya kuweka soko la madini," ameongeza Dkt. Biteko.

Ameongeza kuwa, bado kuna umbali mkubwa hivyo kutoka eneo la machimbo mpaka Bunda na kuwataka kianzishwe kituo kidogo cha kununua madini katika eneo la Kinyambwiga. Amesema, eneo litaandaliwa kwa wafanyabiashara wa madini ( Brokers) ili biashara yote ifanyike katika eneo hilo la wachimbaji.

Share To:

Post A Comment: