Na Rhoda Simba, Dodoma

WANANCHI wametakiwa kulipia kodi  ya pango la Ardhi kabla ya Januari mosi mwaka huu ili kuepuka riba ya asilimia moja ambayo watatozwa kila mwezi kama faini endapo  watachelewa kulipa kodi hiyo.

Hayo yamesemwa leo Disemba 30 jijini hapa na Kamishina wa Ardhi wa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi,Nathaniel Nhonge wakati  akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na kodi ya  pango hilo la Ardhi.

Aidha Nhonge amesema Wizara hiyo imeweka utaratibu mzuri  ili kuhakikisha wanatoa huduma bora za ulipaji kodi ambapo wameanzisha kituo cha mawasiliano kwa wateja na  wanaweza kuwahudumia wananchi popote walipo ili kuwawezesha kulipa kodi.

“Badala ya kutumia muda mwingi kupanga foleni tumeona ni bora kuanzisha huduma hiyo kwa wateja ili waweze kupata huduma za malalamiko yao popote walipo”amesema Nhonge

Nhonge amesema  mikakati ya Wizara hiyo  ni kuhakikisha ina pima ardhi kwa kasi ili kila mtanzania aweze kumiliki ardhi ambapo tayari Wizara hiyo ilishapokea fedha kiasi  cha Shilingi bilioni 50 kutoka Serikalini.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Kodi Wizara ya Ardhi,Nyumba na maendeleo ya Makazi Denis Masami amesema kuwa katika kipindi cha kuelekea mwisho wa mwezi muitikio wa ulipaji kodi ya pango la ardhi umeongezeka ambapo hadi sasa wameshakusanya kiasi cha Shilingi bilioni 60 na malengo ni kukusanya bilioni 221.

“ kwa wiki moja tunakusanya bilioni 3 hadi 4 na hapa tunaona jinsi gani wananchi walivyokuwa na muitiko katika ukusanyaji wa kodi hii ya pango matarajio yetu ni kila mwananchi anayemiliki ardhi alipe kodi ya pango”amesema Masami

MWISHO.

 

Share To:

RHODA SIMBA

Post A Comment: