Kaimu Kamishna wa Uhifadhi Mamlaka ya Usimamizi Wanyamapori  Tanzania (TAWA) Mabula Misungwi  akizugumza na waandishi wa habari jijini Arusha.

MAMLAKA ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania(TAWA), imewaonya watu wanaojenga nyumba,kulima na kufanya shughuli nyingine za kibinaadamu katika maeneo ya mapito ya wanyamapori(shoroba), kwa kuwa wanavunja sheria na wataondolewa.


Akizungumza na waandishi wa habari Kaimu Kamishna wa uhifadhi wa TAWA, Mabula Misungwi amesema uvamizi wa maeneo ya mapito ya wanyama kwa kufanya shughuli za kibinaadamu, ikiwepo kilimo na ujenzi ni makosa kisheria na umekuwa ukiendelea.

Amesema kwa Sasa TAWA unafanya tathimini ya maeneo yote na watachukuwa hatua, kwani kuna sheria na kanuni ambazo zinalinda maeneo haya ambayo baadhi yapo katika maeneo ya vijiji.

Ameongeza miongoni mwa maeneo ambayo tathmini inafanyika ni shoroba ya kwa kuchinja na eneo kati ya hifadhi ya Taifa ya Tarangire na Manyara na akaonya shughuli za uharibifu ambazo zinaendelea ikiwepo ujenzi wa makazi.

Misungwi amesema pia tathimini inafanyika katika maeneo ya Lake Natroni na mengine ambayo kuna uvamizi wa shughuli za kibinaadamu.

Amezishauri Serikali za vijiji ambavyo kuna mapito ya wanyama kujitahidi kuchukuwa hatua kuzuia shughuli za kibinaadamu ikiwepo ujenzi na kilimo.

Kwa mujibu wa tafiti za maswala ya Wanyamapori, hadi sasa zaidi ya asilimia 50 ya maeneo ya corridor yamevamiwa na kufungwa.

Kwa upande wake Mhifadhi wa Hifadhi ya taifa ya Manyara, Noelia Myonga Akizungumza na Mwandishi wa habari hizi hivi karibuni amesema kuvamiwa Kwa maeneo ya mapito ya wanyama Kuna athari katika Uhifadhi.

Myonga amesema miongo mwa athari ni magonjwa kwani wanyama watakuwa wakizaliana familia Moja lakini pia watakosa mahitaji mengine nje ya maeneo ya hifadhi kama Madini ya chumvi na mengine ambayo ni muhimu kwao.

Katika eneo la ikolojia ya hifadhi ya Tarangire na Manyara vikao kadhaa vimewahi kufanyika kudhibiti uvamizi maeneo ya mapito ya wanyama lakini hadi sasa hakuna suluhu.

Vikao hivyo vimekuwa vikihusisha viongozi wa TAWA, watendaji wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Mkurugenzi wa Wanyamapori,Taasisi ya utafiti wa Wanyamapori (TAWIRI) na viongozi wa halmashauri ya Babati na Mkoa wa Manyara.
Share To:

Post A Comment: