Na Asila Twaha, OR TAMISEMI

 

Mwenyekiei wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya masuala ya UKIMWI, Kifua Kikuu, Dawa za Kulevya na Magonjwa yasiyoambukiza Mhe. Fatma Toufiq(Mb) amewapongeza uongozi wa chama cha Wataalam wa Ustawi wa Jamii kwa kuandaa mafunzo ya siku mbili kwa kamati hiyo  kuwajengea uwezo kuhusu masuala muhimu ya ustawi wa jamii.

 

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo Mhe. Toufiq amesema mafunzo yamekua na tija na yameongeza uelewa wao kwa mada  zote zilizowasilishwa kutoka Ofisi ya Rais Tamisemi, Chama cha Wataalam wa Ustawi wa Jamii(TASWO) pamoja na Wadau wa Maendeleo.

 

Akifafanua mada iliyowasilishwa ya usalama wa ulinzi wa mtoto amesema jukumu la kusimamia mtoto ni wazazi/walezi na jamii akiomba jamii kuendelea kusimamia kwa kutambua majukumu ya kila mtoto kwa kufanya hivyo itapunguza uwepo wa wimbi kubwa kwa tegemezi na watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi.

 

“Sisi kama Wabunge na watunga Sheria tunahusika moja kwa moja na jamii tutaendelea kuishauri Serikali kuwa sehemu ya Ustawi wa Jamii iwe Idara kama zamani na sio Kitengo  kama ilivyo hivi sasa ili iweze kutekeleza majukumu yake kama taaluma nyingine” amesema Mhe. Fatma Toufiq

 

Naye Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tamisem Dkt. Grace Magembe amewashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa kushiriki mafunzo hayo na kuwaomba kuendelea kutambua kazi za Maafisa Ustawi wa Jamii kwa kuwaelimisha wananchi  kuhusu majukumu ya Maafisa Ustawi wa Jamii ambao wapo kwa mujibu wa Sheria.

 

“kada ya Maafisa Ustawi wa Jamii ni taaluma kama zilivyo taaluma nyengine za Afya, kuna wakati mwengine jamii inahitaji ushauri tu sio kila mtu anaeumwa apewa dawa wakati mwengine mtu anahitajika ashauriwe ndio hapo Afisa Ustawi wa Jamii anapohusika zaidi” Dkt. Grace

 

Naye Mwenyekiti wa CAUCUS ya Wabunge wa huduma za Ustawi wa Jamii Mhe. Neema Mwandabila(Mb) ameishukuru Serikali na kuomba kuendelea  kupokea ushauri wao sababu wao ndio wanaowakilisha changamoto za wananchi katika maeneo yao.

 

Mafunzo hayo yaliyofanyika siku mbili ya kuwajengea uwezo Waheshimiwa Wabunge wa wanaohusika na masuala ya Ustawi wa Jamii na yameandaliwa na Chama cha Maafisa Ustawi wa Jamii, OR-TAMISEMI kwa kushirikiana na UNICEF, PACT, PLAN INTERNATIONAL pamoja na Wadau wengine wa masuala ya Ustawi wa Jamii.

Share To:

Post A Comment: