Waziri
wa Madini Doto Biteko akizungumza wakati Agosti 1, 2021 wakati akifunga
Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga
yaliyoanza Julai 23 katika uwanja wa Zainab Telack Kijiji cha Butulwa
Manispaa ya Shinyanga
Mwenyekiti
wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula, akizungumza wakati Agosti 1, 2021
wakati Waziri wa Madini Doto Biteko akifunga Maonesho ya Pili ya
Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga Agosti 1, 2021
Waziri
wa Madini Doto Biteko akiwa katika banda la kampuni ya Barrick kwenye
Maonesho ya Pili ya Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga
yaliyoanza Julai 23 katika uwanja wa Zainab Telack Kijiji cha Butulwa
Manispaa ya Shinyanga.
Waziri
wa Madini Doto Biteko, ametoa siku 60 za kufuta leseni za uchimbaji wa
madini zilizohodhiwa na wawekezaji kwa muda mrefu bila kuzitumia.
Biteko
amesema hayo Agosti 1, 2021 wakati akifunga Maonesho ya Pili ya
Biashara na Teknolojia ya Madini Mkoa wa Shinyanga yaliyokuwa
yakifanyika katika uwanja wa Zainab Teleck kijiji cha Butulwa kata ya
Old Shinyanga Manispaa ya Shinyanga.
Amesema, kumekuwepo na
tatizo kwa baadhi ya wawekezaji wa madini kuhodhi leseni kwa muda mrefu
na kutozitumia na pale yanapovumbuliwa madini na wachimbaji wadogo ndipo
hujitokeza na kudai eneo hilo ni lao.
“Tutafuta leseni na
mahakamani utakwenda, utatulipa kutoka mahakamani, kama una leseni
endeleza leseni yako, hatutaki tuwasumbue wachimbaji wakubwa lakini
vilevile wakubwa wasiwasumbue wachimbaji wadogo,’’ ameeleza Biteko.
Kufuatia
hali hiyo, Biteko amesema wametoa siku 60 za kutaifisha leseni za
uchimbaji wa madini zilizohodhiwa na wawekezaji kwa muda mrefu bila
kuzitumia huku akibainisha kuwa Serikali imedhamiria kuinua Sekta ya
Madini, pamoja na kumaliza migogoro yote ambayo hujitokeza baina ya
wachimbaji wadogo na wakubwa.
“Naomba mfikishe salamu kwa
wawekezaji wa madini ambao wana leseni za uchimbaji na hawazitumii,
tumetoa siku 60 tu zianze kutumika, zaidi ya hapo tutazitaifisha na
kutoza gharama ambazo Serikali imeingia kutokana kutolipiwa kodi kwa
muda mrefu na kusababisha Serikali kukosa mapato na fedha hizi lazima
zilipwe hatutakuwa na msalia mtume, hatutaki migogoro ya uchimbaji wa
madini,’’ amesema Biteko.
“Tumeondoa kila aina ya kikwazo
kilichokuwa kinawafanya watu watoroshe madini, tumeondoa kodi peke yake
zaidi ya asilimia 23, tunaona watu kutoka Nje ya nchi Congo, Zambia na
Msumbiji wanaleta madini kuja kuuza hapa, unashangaa kumuona Mtanzania
na yeye anatorosha madini kupeleka mahali kwingine,” amesisitiza Biteko.
Aidha,
amewataka wachimbaji wenye leseni walipe kodi na waepuke vitendo vya
utoroshaji madini huku akibainisha kuwa atakayetorosha madini atakuwa
anachoma madini kwa tochi, hivyo akikamatwa hatabaki salama na kuwataka
wapeleke madini yote kwenye masoko.
“Tumefungua masoko, leo
Tanzania tuna masoko ya madini 39, tuna Vituo vya kuuza madini 50, na
hata Shinyanga masoko yapo mengi, Mwaka 2019 tulifungua soko la kwanza
la madini na hili limetuletea faida kubwa, tuone fahali kulipa kodi,
tuone fahali kupeleka madini kwenye masoko yetu, kama Wizara ya Madini
tutaendelea kuwahudumia watanzania wanaohitaji kuchimba,’’ ameongeza
Biteko
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Prof. Idris
Kikula ameunga mkono kauli ya Waziri Biteko kwa kutoa siku 60 kwa
wawekezaji ambao wanamiliki leseni za uchimbaji madini na kutoziendeleza
kuwa watachukuliwa hatua kali za kisheria, pamoja na kufidia fedha
ambazo zilipaswa kulipwa kwa kipindi chote walichohodhi leseni hizo.
Mkuu
wa Mkoa wa Shinyanga, Dkt. Philemon Sengati amesema maonesho hayo
yamesaidia kuutatangaza Mkoa huo na kuonyesha fursa za biashara hasa
katika sekta ya madini.
Pia, kama mkoa utaendelea kuboresha
maonesho hayo na kuwaunganisha wafanyabiashara na wajasiriamali
akiongeza kuwa maonesho hayo ni muhimu kwa sababu Mkoa wa Shinyanga una
madini mengi na una madini ya pekee ya Almasi ambayo yanaendelea
kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.
“Kupitia maonesho haya
washiriki wamepata fursa ya kutambulisha biashara zao, kuuza bidhaa na
kujifunza teknolojia ya kisasa na kujua wapi wapate mitaji,’’ amesema
Sengati.
Naye, Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Madini mkoa wa
Shinyanga (SHIREMA) Hamza Tandiko amezishukuru Taasisi za kifedha kwa
kuanza kuwapatia mikopo wachimbaji wa madini huku akiomba Serikali
kupeleka umeme wenye nguvu ya kuendesha mitambo kwenye maeneo ya
machimbo kwani umeme uliopo sasa ni kwa ajili ya mwanga tu.
Kwa
upande wake, Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi, Said Pamui
ambao ni miongoni mwa wadhamini wakuu wa Maonesho hayo, amesema taasisi
za kifedha ikiwemo Benki ya CRDB zimeanza kuwezesha mikopo kwa vikundi
vya wachimbaji wa madini na wajasiriamali hivyo kuwakaribisha kupata
huduma katika Benki yao ambayo pia inatoa Bima za aina mbalimbali
zitakazowasaidia wachimbaji.
Maonesho hayo yaliyokwenda kwa kauli
mbiu ya Uwekezaji wa Madini na Viwanda Shinyanga kwa Uchumi Endelevu
yaliyoanza Julai 23 na kufungwa Agosti 1 na Waziri wa Madini Doto
Biteko.
Post A Comment: