Meneja wa Shirika la Posta Mkoa wa Singida, Joseph Mutatina akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi kompyuta tano zilizotolewa na Mbunge wa Jimbo la Singida Mussa Sima kwa ajili ya Shule ya Msingi Nyerere mjini hapa jana.


Diwani wa Kata ya Mghanga Manispaa ya Singida, Vellerian Kimambo akizungumza wakati akikabidhi kompyuta hizo.

Wanafunzi wa shule hiyo wakiwa kwenye hafla ya kukabidhiwa kompyuta hizo.

Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo Charles Ngowi akizungumza wakati wa hafla hiyo.

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi  (CCM) Kata ya Mghanga, Issa Mwanja akizungumza wakati wa hafla hiyo.

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Singida, Hamisi Karage akizungumza wakati wa hafla hiyo.

Makabidhiano ya kompyuta hizo yakifanyika.


Viongozi mbalimbali wakiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi wa shule hiyo baadaya hafla hiyo.

Walimu wa shule hiyo, wazazi, pamoja na viongozi mbalimbali wakiwa katika picha yapamoja baada ya kumpokea msaada wa kompyuta hizo.

.

Na Godwin Myovela, Singida.

SHIRIKA la Posta nchini kupitia Ofisi yake ya Mkoa wa Singida limetangaza mashindano mbalimbali yatakayojikita katika kuonyesha ubunifu wa matumizi ya Tehama katika muktadha wa matumizi ya kidijitali kuelekea kilele cha Siku ya Posta Duniani itakayoadhimishwa Oktoba 9, 2021.

Pamoja na mambo mengine, Shirika hilo limeandaa mashindano ya uandishi wa barua kwa wanafunzi wa Shule za Msingi na Sekondari, wabunifu bora wa TEHAMA, uandishi wa Makala Kwa Wanahabari, uandishi wa Insha kwa Wasanii na Wanamichezo na ubunifu wa video inayotumia vibonzo bora.

Akizungumza mkoani hapa jana wakati akishiriki kwenye hafla ya kukabidhi Kompyuta zilizotolewa na Mbunge wa Jimbo la Singida Mjini Mussa Sima kwa ufadhili wa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) kwenye Shule ya Msingi Nyerere iliyopo Manispaa ya Singida, Meneja wa Posta Mkoa wa Singida Joseph Mutatina alihamasisha wadau mbalimbali kujitokeza na kushiriki. 

"Washindi watakabidhiwa fedha taslimu na zawadi nyingine mbalimbali ifikapo Oktoba 9 mwaka huu ikiwa ni katika kuadhimisha kilele cha Posta Duniani sherehe ambazo kitaifa zitafanyika Dodoma. Nawasihi mjitokeze kwa wingi maana mwisho wa mashindano haya ni ifikapo Septemba 20 mwaka huu," alisema Mutatina.

Kwa Mkoa wa Singida, Shirika la Posta ambalo lipo chini ya Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari mpaka sasa lina ofisi kamili 4 zilizopo Singida Mjini, Kiomboi Halmashauri ya Iramba, Manyoni na Itigi ambazo zimeendelea kufanya vizuri kwenye utoaji wa huduma za kupokea, kusafirisha na kusambaza barua, vifurushi na vipeto.

Mutatina alizitaja huduma nyingine kuwa ni pamoja na usafirishaji wa barua kwa njia ya haraka (EMS) ndani na nje ya nchi, usafirishaji mizigo mikubwa, kutoa huduma ya masanduku ya barua ikiwemo kwa kutumia TEHAMA ya Posta Kiganjani na huduma ya uwakala wa fedha.

Shirika hilo ambalo lilianzishwa kwa Sheria ya Bunge Namba 19 ya mwaka 1993 na kuanza kazi rasmi Januari Mosi, 1994 huduma zake nyingine ni usafirishaji wa fedha kwa njia ya 'Posta Cash', Uwakala wa Bima ikiwemo Shirika la Bima nchini na Shirika la Bima Zanzibar.

Meneja Mutatina pamoja na mambo mengine alisema huduma za uuzaji wa hisa za makampuni mbalimbali, ulipaji wa wastaafu, huduma ya Bodi ya Mikopo na Baraza la Mitihani Kwa maana ya maulizo, kupokea maombi ya mikopo na kuyasafirisha kwenda Bodi sanjari na Baraza la Mitihani maulizo na kusajili watahiniwa vyote vinafanywa ndani ya shirika hilo.

"Posta tunagusa kila mahali, pia tuna huduma za Duka Mtandao, Intaneti Cafe, tunakodisha majengo kwa huduma mbalimbali na zaidi tuna mfumo wa kufuatilia barua au kifurushi kilichotumwa kupitia Mtandao kujua kimefikia wapi au kimepokelewa na nani," alisisitiza Meneja.

Kwa huduma za usafirishaji wa barua, vifurushi, vipeto na mizigo yote kuanzia bahasha mpaka Tani 30 imeelezwa kwamba utaratibu wa safari zake Kwa kuanzia Singida kuelekea Mikoa ya Dar es Salaam, Mwanza na Kigoma hufanyika kila siku majira ya jioni.

"Magari yetu ya Dar es Salaam hupitia miji ya Manyoni, Dodoma na Morogoro, na yale ya Mwanza hupitia njia ya Shinyanga, na Kigoma hupitia miji ya Nzega, Tabora, Urambo hadi Kigoma," alisema Mutatina.


Share To:

dotto mwaibale

Post A Comment: