Afisa Ustawi wa Jamii Mkoa wa Singida, Shukrani Mbago, akizungumza na Waganga Wafawidhi na Maafisa wa Jeshi la Polisi kwa niaba ya Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida ambaye alikuwa mgeni rasmi wa kikao kazi kilichofanyika jana ambacho kiliandaliwa na Shirika lisilo la kiserikali la Empower Society Transform Lives (ESTL) lenye makao yake makuu mkoani Singida  kwa ufadhili wa Ubalozi wa Uholanzi. Kulia ni Mtendaji Mkuu wa Shirika hilo, Joshua Ntandu Lisu.


Mratibu wa Dawati la Jinsia na Watoto mkoani hapa Mkaguzi wa Polisi, Idda John, akichangia jambo kwenye kikao hicho.

Mkaguzi wa Polisi, Juma Baltazar, akichangia jambo kwenye kikao hicho.


Kikao kikiendelea.

Dkt.Getrude Mughamba, akichangia mada kwenye kikao hicho.

Kikao kikiendelea.

Afisa kutoka Shirika la ESTL, Emmanuel Nkumbi, akizungumza kwenye kikao hicho.

Kikao kikiendelea.

Dkt. Swalehe Jula, akichangia kwenye kikao hicho.


Kikao kikiendelea.

Mratibu wa mradi wa shirika hilo , Annamaria Mashaka akitoa mada katika kikao hicho. 

Kikao kikiendelea. Katikati ni Mganga Mkuu wa Polisi Mkoa wa Singida, Dkt. Hassani Muhidini.

Kikao kikiendelea.
Kamisha Msaidizi  wa Polisi  (ACP) Hassani Omary  Maya, akielezea namna ya ujazaji wa fomu ya Polisi namba tatu PF3.
Afisa wa Polisi, Ulinyambusya Ambukege,akichangia jambo kwenye kikao hicho.
Dkt.Anwar Mkulu, akichangia kwenye kikao hicho.



Na Dotto Mwaibale, Singida


SHIRIKA lisilo la kiserikali la Empower Society Transform Lives (ESTL) lenye makao yake makuu mkoani Singida limewakutanisha Jeshi la Polisi na Waganga Wafawidhi kwa lengo la kupeana elimu ya namna bora ya uboreshaji  ujazaji wa fomu ya Polisi namba tatu PF3.

Kwa mujibu wa ESTL kumekuwa na mkanganyiko wa huduma stahiki inayotokana na fomu hiyo hususani katika kukabiliana na vitendo vyote vya ukatili kwa watoto wa kike katika masuala ya ukeketaji na ukatili wa kijinsia ambayo bado hufanyika kwa siri.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Mtendaji Mkuu wa Shirika hilo Joshua Ntandu Lisu alisema lengo la kuwakutanisha wadau hao wawili ni kuona namna gani watabadilisha mawazo ya kumaliza changamoto ya ujazaji wa Polisi fomu namba tatu PF3 ili kuweza kutoa haki katika kesi za wahanga wa vitendo vya ukatili ambazo zimekuwa zikiwapa ushindi watuhumiwa kutokana na fomu hizo kutojazwa vizuri na waganga hao wafawidhi.

"Leo tulikuwa na kikao kazi baina ya Jeshi la Polisi na Waganga Wafawidhi wa Vituo 62 vya Afya vya kutoka Manispaa na Halmashauri ya Singida na lengo kubwa lilihusu utambuzi wa watoto waliofanyiwa ukatili wa kijinsia vikiwemo vitendo vya ubakaji pamoja na utoaji wa taarifa ambapo tulikuwa tukijadili namna gani ya kutatua changamoto inayojitokeza kutokana na ujazaji wa fomu ya Polisi namba Tatu PF3." alisema Lisu.

Lisu alisema katika kazi ambazo walikuwa wanazifanya kesi nyingi zilikuwa zinaharibika kutokana na ujazaji wa fomu hizo kwa hiyo kikao hicho kililenga kutatua changamoto hiyo kwani madaktari walikuwa wazito wa kuzijaza kwa sababu PF3 nyingi zilikuwa zikitoka Polisi wanawapa wahanga ambao walikuwa wanaenda kuzijaza hospitali na baada ya hapo wanazirudisha tena polisi ambapo madaktari waliona haikuwa salama kutokana na unyeti wa kazi yao.

Alisema madaktari hao walipendekeza kuwa ni vizuri mhanga atoke na polisi kwenda hospitali kujaza fomu hiyo na kisha polisi aipeleke mahakamani kwa ajili ya kuendelea na mashauri na kuwa hiyo ndiyo ilikuwa changamoto kubwa ya wao kushindwa kujaza fomu hiyo.

Aidha Lisu alisema kupitia kikao kazi hicho waligundua kuwa baadhi ya madaktari walikuwa hawana uelewa wa kutosha juu ya masuala ya ujazaji wa fomu hizo na kuwa kupitia kikao hicho maaskari polisi wamepata fursa ya kuwaelekeza madaktari namna ya ujazaji wa fomu hizo na kuwa hivi sasa wanaamini kesi zote za ukatili zitakuwa zinaenda sawasawa.

Alisema Shirika hilo linalojishughulisha na shughuli mbalimbali zikiwemo masuala ya Afya, Elimu, Mazingira kwa kutumia mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA ) umetekeleza mradi huo waliouanza mwaka 2017 kwa ufadhili wa Civil Society Foundation, Ubalozi wa Finland  na sasa Ubalozi wa Uholanzi  ambao umewawezesha kufanya kikao kazi hicho na kuwa wamejipanga kufanya kikao cha namna hiyo na halmashauri zote za Mkoa wa Singida ili nao wanufaike na jambo hilo.

Akizungumza kwa niaba ya Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida ambaye alikuwa mgeni rasmi katika kikao hicho Afisa Ustawi wa Jamii mkoani hapa, Shukrani  Mbago alisema wahanga wa matukio hayo mara wanapofikishwa katika vituo vya afya wahudumu wa afya wawape huduma stahiki kwa haraka ndani ya masaa 72 na kuacha tabia ya kuchelewa kujaza PF3.

Mratibu wa Dawati la Jinsia na Watoto mkoani hapa Mkaguzi wa Polisi, Idda John alisema moja ya changamoto ambayo inasababisha kesi nyingi kushindwa au kuharibika kwa ushahidi ni ule unaotokana na fomu yao ya Polisi PF3 kwani mara nyingi wenzao watoa huduma za afya kwa maana madaktari wamekuwa wakijaza fomu hizo sehemu tofauti kwa mfano kwenye makosa yanayohusiana na ngono mfano kulawiti na kubaka ile PF3 inaelekeza ijazwe sehemu hiyo lakini wao wanajaza eneo la mashambulio ya mwili au ajali jambo linaloharibu ushahidi na kuwafanya wahanga kukosa haki zao.

Kwa upande wake Dkt. Getrude Mughamba kutoka Wilaya ya Singida alikiri kuwepo  changamoto hiyo kwa baadhi yao kutojua namna ya ujazaji wa fomu hizo na kuwa kuanza hivi sasa baada ya kupata mafunzo hayo wanaamini hazitajitokeza tena na kila muhusika atapata haki zake. 

Share To:

Post A Comment: