Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe.  Mhandisi, Hamad Yussuf Masauni (Mb), akijibu swali la Mbunge wa Jangómbe, Mhe. Ali Hassan Omar King, kuhusu wajibu wa kumlipa mteja aliyeibiwa fedha kwenye akaunti ya benki, bungeni jijini Dodoma.


Na. Peter Haule na Saidina Msangi, WFM, Dodoma

Serikali imesema kuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) hutoa adhabu kwa Benki yeyote itakayobainika kusababisha fedha za mteja kuibwa kutokana na utaratibu uliowekwa na Benki husika kuwa na kasoro.

Hayo yamebainishwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Mhandisi, Hamad Yussuf Masauni (Mb), alipokuwa akijibu swali la msingi la Mbunge wa Jang’ombe, Bw. Ali Hassan King, aliyehoji wizi unapotokea kwenye akaunti ya benki ya mteja uliofanywa na mtumishi wa benki nani mwenye wajibu wa kumlipa mteja.

“Endapo itabainika kuwa wizi umefanywa na mtumishi wa Benki, hatua stahiki huchukuliwa kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo ikiwa ni pamoja na mteja kulipwa kiasi alichoibiwa”, alisema Mhandisi Masauni.

Alieleza kuwa mhalifu huchukuliwa hatua za kinidhamu pamoja na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria ili Sheria ichukue mkondo wake.

Mhandisi Masauni alibainisha kuwa, wizi unapotokea kwenye akaunti ya benki ya mteja, uchunguzi wa kina hufanywa na vyombo husika katika masuala ya upelelezi ikiwa ni pamoja na Jeshi la Polisi na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kwa kadri hali na mazingira ya tukio yatakavyokuwa.

Share To:

Post A Comment: