Na, Tito Mselem Dodoma,


Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya leo Aprili 12, 2021 amefungua Mkutano wa siku moja wa wadau wa madini unao jadili na kutoa mapendekezo kuhusu Kanuni za ushiriki wa Serikali kwenye Miradi ya Madini nchini.


Akizungumza kwenye Mkutano huo, Prof. Manya amesema, Wizara ya Madini ilitunga Kanuni zinazo simamia Shughuli za Madini za Mwaka 2017 ambapo baadhi ya kanuni hizo zimeonekana zina changamoto katika utekelezaji wake.


“Tumeamua kuzirekebisha baadhi ya Kanuni zilizotungwa Mwaka 2017 ambapo tumeona ni vyema tukawaita wadau wote wa Sekta ya Madini ili kila mmoja kwa nafasi yake atoe mchango wake  anaoona  unafaa ili tuziboreshe Kanuni zilizopo hususani Kanuni za Ushiriki wa Serikali katika Sekta ya Madini,” amesema Prof Manya.


Prof. Manya amesema, Wizara ya Madini imeona umuhimu wa kuwaita wadau wa Sekta ya Madini ili kuwashirikisha  katika kutoa mapendekezo kwenye marekebisho hayo na kuwafanya kuwa sehemu ya kutengeneza Kanuni hizo zinazoiongoza sekta hiyo.


Aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati, Dkt. John Pombe Magufuli alikuwa anatumia muda wake mwingi kuhakikisha Sekta ya Madini inakuwa na kuongeza mchango wake kwenye Pato la Taifa ambapo amewataka wadau wote wasimuangushe Hayati, Dkt. Magufuli kwa maono yake mazuri aliyo yaacha.


Aidha, Prof. Manya amesema Wizara ya Madini imeweka lengo la kukusanya zaidi ya Shilingi bilioni 600 kwa Mwaka wa fedha 2021/2022 na kuongeza kuwa lengo ni kuhakikisha mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa unakuwa na kufikia asilimia 10 ifikapo 2025.


Pia, Prof. Manya amesema Mwaka 2020, Sekta ya Madini iliongoza katika kuliingizia Taifa fedha za kigeni nchini ambazo zilitokana na shughuli za madini ambapo mapato yatokanayo na shughuli za madini yameongezeka na kufikia asilimia 5.7 katika mchango wake kwenye Pato la Taifa ukilinganisha na asilimia 3.4 Mwaka 2015.

  

Akiwasilisha mada na miongozo iliyopo kwenye Kanuni za Sekta ya Madini, Mkurugenzi wa Huduma ya Sheria wa Wizara ya Madini Edwin Igenge,  amewataka wadau wote kushiriki kwa uwazi ili kufanikisha suala la kuziboresha Kanuni zinazoiongoza sekta hiyo.


Kwa upande wake Meneja Mkuu wa Kampuni ya Shanta-Singida Mhandisi Philbert Rweyemamu, ameipongeza Wizara ya Madini kwa kuamua kuwashirikisha katika kuzichambua na hatimaye kuzifanyia marekebisho baadhi ya Kanuni zinaoonekana kuwa zina changamoto katika utekelezaji wake.

Share To:

msumbanews

Post A Comment: