KATIBU Tawala Mkoa wa Arusha Richard Kwitega ameipongeza Wizara ya Fedhana Mipango na Serikali kwa ujumla kwa kuweka mfumo imara wa ukusanyaji mapato ya Serikali wa GePG ambao unawawezesha wananchi kulipia huduma mbalimbali za Serikali kupitia mfumo huo.


Akizungumza wakati akifungua semina ya siku mbili kwa Wahariri kutoka Vyombo mbali mbali nchini kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Bw. Doto James iliyoanza leo jijini Arusha, amesema kuwa mfumo wa GePG umeimarisha ukusanyaji mapato ya ndani na kuwezesha mwananchi kuwa na uhakika wa malipo mbali mbali yanayofanyika kupitia ( Control Number) ambayo ni salama zaidi katika mchakato wa ukusanyaji mapato.

Amesema, mfumo huo pia unawezesha wananchi kuokoa muda kuanzia anapopata Ankara zake, namna ya ulipaji wake, na upatikanaji wa Stakabadhi yake ikiwa ni pamoja na fedha kufika serikalini kwa wakati na kuepuka upotevu wa mapato ya Serikali.

’’Mfumo huu wa GePG umeimarisha ukusanyaji mapato kwa kuondoa gharama za miamala ya fedha kwa Umma, utaratibu usio rafiki wa ulipaji huduma za Umma pamoja na makusanyo yote kuonekana kwa uwazi na uhakika wa taarifa mbali mbali." Amesema Kwitega.

Aidha, alisema kuwa, mfumo huu umeweza kuongeza mapato mfano Wakala wa misitu Tanzania walikuwa wakikusanya kiasi cha shilingi bilioni 95 kwa mwaka kabla ya mfumo huu wa GePG lakini baada ya kutumia mfumo huo waliweza kukusanya kiasi cha shilingi bilioni.115.

Vile vile, alisema kuwa Shirika la Umeme TANESCO liliweza kuokoa kiasi cha shilingi bilioni 38 kwa mwwaka ambazo zilikuwa zikitumika kulipia gharama za wakala kabla ya mfumo huo ambapo baada ya kufunga mfumo huu wameweza kuokoa fedha hizo ambazo zilikuwa gharama za miamala kwa umma.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mifumo ya Fedha kutoka Wizara ya Fedha na Mipango Bw. John Sausi amewataka wahariri kuhakikisha kuwa wanatoa elimu sahihi kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kutumia mfumo wa Serikali wa Kielektroniki wa Ukusanyaji wa Mapato(GePG) katika kufanya malipo ya huduma mbalimbali za Serikali . Sausi amesema, kabla ya mfumo huo wa GePG kulikuwa na upotevu mkubwa wa mapato ya Serikali kutokana na kutokuwepo kwa uwazi wa ukusanyaji wa mapato pamoja na ukosefu wa taarifa sahihi na kwa wakati.

“Niwaombe wahariri muwaeleze wananchi kuepuka kulipa pesa taslimu kwa kuwa, kwanza hazitafika kwa wakati pili zitapotea na mwananchi ataingia hasara ya kulipa kwa mara nyingine tena, hivyo watumie 'Contorl Number' ili kuepuka upotevu usio wa lazima.”amesema John.

Aidha alisema kuwa Mfumo huo umeunganishwa na Taasisi mbalimbali za Serikali za mitaa, Halmashauri, Taasisi na serikali kuu zipatazo 670.

Bw. Sausi alisema mfumo huo ulianzishwa rasmi mwaka 2017 kwa Taasisi chache ambapo umewezesha kuongezeka kwa mapato kiasi kikubwa.

Kwa upande wake Mchumi Mwandamizi anayesimamia mapato ya Serikali kutoka Idara ya Uchambuzi wa Sera Bi. Neema Maregeli alibainisha kuwa mfumo wa GePG umeongeza mapato ya Serikali kutoka wastani wa shilingi bilioni 800 kabla ya Mfumo huu hadi wastani wa trioni 2.4 kwa mwaka.

Alisema kuwa mapato haya yamewezesha Serikali kutekeleza shughuli zake mbalimbali ikiwemo kuimarisha utoaji wa huduma za jamii na utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Vile vile , alisisitiza umuhimu wa vyombo vya habari kupitia wahariri walioshiriki mafunzo hayo kuwaelimisha wananchi kwa ufasaha umuhimu wa kulipa kodi, kudai risiti wanapofanya manunuzi na kwa upande wa wafanya biashara kutoa risiti wanapouza huduma na bidhaa mbalimbali.

KATIBU Tawala Mkoa wa Arusha Richard Kwitega akizungumza wakati akifungua Semina ya Siku mbili kwa Wahariri kutoka Vyombo mbali mbali nchini kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya fedha Doto James),kuhusu Mfumo wa Ukusanyaji Mapato Serikalini (GePG), iliyoanza leo katika ukumbi wa jengo la hazina ndogo iliopo chini ya Wizara ya Fedha na Mipango leo Februari 3,2021 ambapo mada mbalimbali zitatolewa na wataalamu wa mfumo huo na kuwajengea uelewa wahariri namna ya kuripoti habari zinazohusu mfumo huo.Picha kushoto ni Mkurugenzi wa mifumo ya kifedha kutoka Wizara ya Fedha na Mipango John Sausi


Mkurugenzi wa mifumo ya kifedha kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, John Sausi akizungumza kwenye Semina ya Siku mbili kwa Wahariri kutoka Vyombo mbali mbali nchini akieleza umuhimu wa kutumia Mfumo wa Ukusanyaji Mapato Serikalini (GePG), Semina hiyo imefanyika leo Februari 3,2021 katika ukumbi wa jengo la hazina ndogo iliopo chini ya Wizara ya Fedha na Mipango jijini Arusha. 
Baadhi ya Wahariri na Waandishi wa Habari kutoka vyombo mbalimbali wakifuatilia yaliyokuwa yakizungumzwa na Mgeni rasmi wakati wa ufunguzi wa semina hiyo ya siku mbili,jijini Arusha.

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Benny Mwaipaja akiwatambulisha viongozi mbalimbali na maofisa wa Wizara ya Fedha pamoja na wahariri wa vyombo vya habari kabla ya kuanza kikao kazi cha siku mbili kinachofanyika katika ukumbi wa jengo la hazina ndogo iliopo chini ya Wizara ya Fedha na Mipango leo Februari 3,2021.Mchumi Mwandamizi (Mapato) Wizara ya Fedha na Mipango,Neema Maregeli akizungumza mbele ya Wahariri na Waandishi wa Habari kwenye Semina ya Siku mbili akifafanua umuhimu wa kutumia Mfumo wa Ukusanyaji Mapato Serikalini (GePG). Semina hiyo imefanyika leo Februari 3,2021 katika ukumbi wa jengo la hazina ndogo iliopo chini ya Wizara ya Fedha na Mipango jijini Arusha.
Baadhi ya Wafanyakazi wa Wizara ya Fedha na Mipango wakijatambulisha kwa Wahariri na Waandishi wa Habari kutoka vyombo mbalimbali
 Baadhi ya wahariri kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini wakimsikiliza Katibu Tawala Mkoa wa Arusha Bw.Richard Kwitega wakati akizungumza katika ufunguzi wa semina hiyo inayoendelea kwenye ukumbi wa Hazina ndogo Jijini Arusha. 

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Benny Mwaipaja akimueleza jambo kwa mgeni rasmi KATIBU Tawala Mkoa wa Arusha Richard Kwitega kabla ya kufungua Semina ya Siku mbili kwa Wahariri kutoka Vyombo mbali mbali nchini kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya fedha Doto James.
Mhariri Mkuu kutoka kituo cha matangazo cha Redio5 Arusha Bi.Ashura Mohamed akijitambulisha kabla ya kuanza kwa semina ya siku mbili ya wahariri wa vyombo vya habari nchini inayoendelea jijini Arusha.
Share To:

Post A Comment: