Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Singida, Adili Elinipenda (katikati) akitoa taarifa ya utekelezaji kwa kipindi cha miezi mitatu Oktoba hadi Disemba 2020 mkoani hapa juzi.



 Na Dotto Mwaibale, Singida


TAASISI ya kuzuia na kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Singida imeokoa zaidi ya shilingi 270.7 kutoka maeneo mbalimbali ikiwemo mikopo umiza.

Akitoa taarifa ya utekelezaji kwa kipindi cha miezi mitatu Oktoba hadi Disemba 2020 Mkuu wa Taasisi hiyo Mkoani hapa Adili Elinipenda alisema Takukuru imeokoa shilingi milioni 270,079,600 ndani ya kipindi hicho kutoka maeneo mbalimbali.

Elinipenda alisema shilingi milioni 154,416,000 pekee zimeokolewa kutoka mikopo umiza, shilingi milioni 28,000,000 ziliokolewa kutokana na fidia ya maeneo ya wananchi yaliyotwaliwa kufanya shughuli za uchimbaji madini Wilayani Mkalama,wakati kiasi kingine kikiokolewa kutoka maeneo mengine ikiwemo mahakama ya Manyoni.

"Fedha hizi tulizikabidhi kwa wahusika baada ya kuokolewa ambapo fedha tulizoziokoa kutoka mikopo umiza, Mkuu wa Mkoa Dk Nchimbi aliwakabidhi wananchi hao wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani Manispaa ya Singida." alisema Elinipenda.

Alisema katika kuhakikisha Vitendo vya Rushwa vinaisha Takukuru kwa kushirikiana na wadau wengine imeendelea kutoa Elimu kwa jamii kwa kushirikisha makundi mbalimbali ikiwemo Vijana wa shule za msingi, Sekondari na Vyuo.

Aidha Elinipenda alisema Taasisi hiyo imeanzisha utaratibu wa Takukuru inayotembea (MOBILE PCCB) ambapo itatenga siku moja ndani ya mwezi ili kuwatembelea wananchi kwenye maeneo yao lengo la kufanya hivyo ni kusikiliza na kutatua kero zao.

Hata hivyo Taasisi hiyo inazidi kutoa rai kwa wananchi wa Mkoa wa Singida kujiepusha na Vitendo vya Rushwa huku ikiwataka kushiriki kikamilifu katika kutoa taarifa za Vitendo hivyo pamoja na kutoa ushirikiano kwenye uchunguzi na kutoa ushahidi mahakamani

Share To:

Post A Comment: