Na Mwandishi Wetu,HESLB,
BODI ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imetangaza orodha ya wanafunzi 5168 wa awamu ya pili wa mwaka wa kwanza waliopangiwa mikopo yenye thamani ya TZS 19.9 bilioni.

Taarifa iliyotolewa katika vyombo vya habari na Mkurugenz Mtendaji wa HESLB, Abdul-Razaq Badru inasema hadi leo (Jumanne, Novemba 17, 2020), jumla ya wanafunzi 52,473 wa mwaka wa kwanza wamepangiwa mkopo yenye thamani ya TZS 170.02 bilioni.

Basru alisema Novemba 11, mwaka huu HESLB ilitangaza orodha ya Awamu ya Kwanza waliopangwa mikopo iliyokuwa na wanafunzi wa mwaka wa kwanza wapatao 47,305 ambao walipangiwa mikopo yenye thamani ya TZS 150.03 bilioni.

“Wanachotakiwa kufanya kwa sasa ni kutembelea katika akaunti zao za SIPA walizotumia kuomba mkopo na watapata taarifa za kina kuhusu mkopo,” amesema Abdul-Razaq Badru leo (Jumanne, Novemba 17, 2020) Jijini Dar es Salaam.

Waliokosea sasa ruksa kurekebisha
Kuhusu wanafunzi waombaji ambao maombi yao yalikua na upungufu, Badru amesema HESLB imetoa muda wa siku tano (05) kuanzia kesho (Jumatano, Novemba 18, 2020) kurekebisha taarifa zao na kuzituma kwa njia ya mtandao.

“Tuna wanafunzi wachache ambao maombi yao yana upungufu ambao kuanzia kesho wataweza kuingia katika akaunti zao za SIPA walizotumia kuomba mkopo na kurekebisha kwa kuweka nyaraka sahihi na tutazifanyia uchambuzi na wenye sifa watapangiwa mikopo mapema iwezekanavyo,” amesema Badru.

katika mwaka 2020/2021, Serikali imetenga kiasi cha TZS 464 Bilioni kwa ajili ya kugharamia mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu 145,000 wakiwemo wanafunzi 54,000 wa mwaka wa kwanza na wanafunzi 91,000 wanaoendelea na masomo.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: