Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dkt Rehema Nchimbi (katikati) akiwa na Watafiti Waandamizi na Mtaalamu kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo TARI Naliendele, na Bodi ya Korosho ofisini kwake jana, mda mfupi baada ya kufanya mazungumzo ya namna bora ya kuinua ubora wa zao la korosho ndani ya mkoa huo.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dkt Rehema Nchimbi akiwa na Mratibu wa zao la Korosho kitaifa, Dkt Geradina Mzena wakiangalia moja ya aina za mbegu bora za korosho.

Mkulima wa Korosho kutoka Singida, Hassan Tati, akishiriki mafunzo yanayotolewa na TARI Naliendele kwa Maafisa ugani na Wakulima ya Kilimo Bora cha Korosho eneo la namna bora ya kuandaa shimo kabla ya kupanda mkorosho kwenye shamba la mfano eneo la Somoku, Kata ya Mungu Maji Singida jana.

Afisa Kilimo Manispaa ya Singida, Halima Kalungwana akishiriki kwa vitendo mafunzo hayo.

Mkulima Seleman Mohamed wa Kata ya Unyianga akiwa kwenye mafunzo hayo.
Afisa Kilimo Kata ya Msisi Singida, Alphoncina Muna (aliyevaa kofia) akishiriki mafunzo hayo.

Mtaalamu wa Agronomia kutoka TARI Naliendele Kasiga Ngiha, akiendesha mafunzo. 

Mtafiti Mwandamizi na Mtaalamu wa Magonjwa ya Mikorosho kutoka TARI Naliendele, Dkt Wilson Nene akiwaonyesha wakulima na Maafisa Ugani namna magonjwa na Wadudu waharibifu walivyoshambulia moja ya mkorosho uliopo eneo hilo na namna bora ya kudhibiti hali hiyo.

Watafiti kutoka TARI Naliendele wakiangalia moja ya mkorosho ulioathiriwa vibaya na ugonjwa wa Ubwiriunga kwenye shamba la Somoku-Mungu Maji singida jana, kupitia mafunzo hayo wakulima na Maafisa Ugani wanaendelea kupewa mafunzo ya namna ya kudhibiti hali hiyo.
Akinamama wakiwa kwenye mafunzo hayo.
Mafunzo yakiendelea.
Mafunzo yakiendelea.
Mafunzo yakiendelea.
Mafunzo yakiendelea.
 



Godwin Myovela na Dotto Mwaibale, Singida


MKUU wa Mkoa wa Singida, Dkt Rehema Nchimbi amesema wakulima mkoani hapa wamedhamiria kuwa kinara kwenye uzalishaji wa zao la Korosho nchini, kutokana na jiografia yake kuwa rafiki kwa ‘Dhahabu hiyo ya Kijani’ ambayo inatajwa kuwa na utajiri mkubwa, huku mfumo wa soko ukiendelea kuwa wazi, salama na uhakika.

Aidha, watafiti kutoka TARI Naliendele wamebaini, kwa msimu ujao wa mavuno korosho ya mikoa ya Kanda ya Kati ikiwemo Singida, Morogoro na Dodoma italeta ushindani mkubwa wa soko kwa viwango na ubora, kutokana na wakulima wake kuendelea kuzingatia kanuni bora za kilimo cha zao hilo.

Nchimbi akizungumza na Mratibu wa zao la Korosho kitaifa kutoka TARI Naliendele, Dkt Geradina Mzena ofisini kwake jana, alisema kwa sasa mkoa huo umedhamiria kwa dhati kuinua tija na uzalishaji sambamba na kutoa msukumo wa kipekee wa zao hilo kwa ubora na viwango vinavyokidhi soko.

“Baada ya kubaini korosho pia ni zao letu wana-singida, ni mkombozi, na litaubadili kabisa mkoa wetu kiuchumi na kuondokana na kadhia yoyote ya kuturudisha nyuma; hicho ndicho kilichotusukuma kuingia jumla jumla katika kilimo hiki cha kitajiri na cha kimkakati,” alisema Mkuu huyo wa mkoa.

Alisema mpaka sasa, mkoa huo unamshukuru sana Rais John Magufuli, ambaye serikali yake ya Awamu ya Tano ndiyo iliyobeba wazo hilo la kuwa na stratejia makini za kuifanya korosho kuwa na tija na ufanisi unaoonekana, wazo ambalo limeendelea kuwaletea wakulima wa zao hilo matokeo chanya, hususani  kwenye vita dhidi ya umasikini.

Hata hivyo, akizungumzia juu ya mradi wa ‘Kilimo cha Pamoja’ au maarufu ‘Kilimo cha Bega kwa Bega,’ kilichoshika kasi kwenye baadhi ya maeneo ya mkoa huo, Nchimbi alisema kilimo hicho kimelenga kushirikiana ili hatimaye wakulima waweze kupata huduma za kiugani na agronomia stahiki za korosho kwa pamoja, usawa na kwa wakati.

“Nawapongeza sana TARI Naliendele na serikali kwa ujumla kwa mafunzo ya kilimo bora cha korosho mnayoendelea kuyatoa ndani ya mkoa wa Singida. Lengo la serikali yoyote ni kuwatumikia wananchi wake…tukiwa kwenye safari ya kuelekea katika Uchumi wa Viwanda, mikoa yote nchini tunatakiwa tutembee pamoja kwa kasi inayodhihirika na ya kuaminika, tusibaguane” alisema Nchimbi.

Mkoa huo ambao una nadharia ya “Twende Wote” “Twende Pamoja”  katika kukuza uchumi na kuifanya Singida kuwa ya Viwanda, kwa sasa umegeuka kuwa kivutio kikubwa cha ustawi wa zao la korosho, na zaidi unatajwa kuwa miongoni mwa mikoa ya Kanda ya Kati, ambao unaanza kwenda kuzalisha korosho kwa kasi na yenye tija stahiki.

Nchimbi alisema wakati wa utekelezaji wa nadharia ya ‘Singida Twende Pamoja kwenye zao la korosho huwa hakuna bingwa, hakuna mzoefu wala mkuu, ndio maana kuna ufanisi. “Inapofika wakati wa kupanda tunapaswa tupande wote, tupalilie pamoja, tupulize viuatilifu pamoja, tuokote wote, na pia tuuze wote.”

Kwa upande wake Mratibu wa zao la Korosho Kitaifa, kutoka Naliendele, Dkt Geradina Mzena alimshukuru na kumpongeza ‘mama’ Nchimbi kwa kuwa balozi mzuri kwa wana-singida wote, na hasa pale anapobaini fursa amekuwa mstari mbele kuiboresha na kuipa msukumo wa kipekee kwa maslahi ya mkoa huo.

Mzena akizungumzia aina za mbegu bora 54 za korosho, alisema mbegu hizo baada ya kufanyiwa utafiti zimethibitika pasipo shaka kuwapo kwa ongezeko la thamani, ubora na kiwango cha juu cha uzalishaji, sambamba na kuwa na uwezo mkubwa wa kuhimili magonjwa na wadudu waharibifu, ikilinganishwa na za kienyeji.

Share To:

Post A Comment: