Na John Walter-Manyara
Mahakama ya Wilaya ya Babati, mkoani Manyara imemuhukumu Salimu Hassan Kijuu (38) kwenda jela miaka 20 kwa kupatikana na tuhuma za kumiliki nyara za serikali kinyume na utaratibu.

Akisoma mashtaka hayo agosti 26,2020, Mheshimiwa Hakimu wa mahakama hiyo Victor Kimario, alisema baada ya mahakama kuridhika na ushahidi uliotolewa, Mahakama  imemtia hatiani na kumpa adhabu hiyo ili iwe fundisho kwa wote wenye nia ya kutenda kosa kama hilo.

Mwendesha Mashtaka wa serikali upande wa Wanyamapori Rusticus Mhundi,  alieleza mahakamani hapo kuwa, mshtakiwa alitenda kosa hilo mwaka 2019  kijiji cha Gijedabong wilaya ya Babati kinyume na sheria ya wanyamapori Kifungu cha 86 (1) na (2) (b) ya sheria namba 5 ya mwaka 2009.

Alisema kuwa Mshtakiwa huyo ambaye ni mkazi wa Kijiji hicho  alitiwa hatiani baada ya kupekuliwa na Askari na kukutwa akiwa na nyama ya mnyama Pundamilia kilo 17 kwenye mfuko  ambayo thamani yake ni shilingi milioni Mbili laki saba na sitini.

Mahundi amesema mtuhumiwa amehukumiwa kwa kosa la uhujumu uchumi kama inavyoelekeza aya ya 14 kifungu cha 57 (1) na kifungu namba 60, kifungu kidogo cha pili cha sheria ya kuhujumu uchumi iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 na kufanyiwa marekebisho na kifungu cha 16 (a) na 13 (b) za sheria namba 3 ya mabadiliko ya sheria ya mwaka 2016.
Share To:

Post A Comment: