Jaji Mstaafu wa mahakama ya Rufaa Eusebia Munuo akiongea kwenye Kongamano la wanawake wa Jumuiya ya Afrika mashariki Leo ikiwa ni kuanza kwa maadhimisho ya siku ya wanawake duniani kesho kutwa tarehe 8 picha zote na Ahmed Mahmoud Arusha

Mbunge wa bunge la Afrika mashariki EALA Francoise Uwumukiza akiongea kwenye Kongamano hilo la kujadili changamoto za wafanyabiashara wanawake mipakani lililofanyika kwenye ukumbi wa Jumuiya ya Afrika mashariki Jijini Arusha leo.

Meza kuu wakifuatilia mjadala uliokuwa unaendelea kwenye Kongamano la wanawake wafanyabiashara wa mipakani ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya wanawake duniani.


 Ahmed Mahmoud Arusha
Wanawake duniani na hapa nchini wametakiwa kuikataa kwa nguvu zote rushwa ya ngono na vitendo vya ukatili wa kijinsia ambayo imekuwa ikiendelea kukithiri ndani jamii zetu.

Akizungumza kwenye Kongamano la kinamama kuazimisha siku ya wanawake duniani kwa nchi za jumuiya ya Afrika mashariki Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufaa Eusebia Munuo ambaye pia ni Mwenyekiti msaafu wa chama Cha majaji wanawake nchini alisema ni muhimu kwao kuanza kujitambua na kujua haki zao sanjari na kupinga ndoa za utotoni.

Alisema kuwa kumekuwa na wimbi kubwa la ongezeko la mimba za utotoni jambo linalopelekea matunzo kushuka kwa watoto wetu hivyo kuongeza wimbi la watoto wa mitaani suala ambalo linahitaji kusimama kama kinamama kuhakikisha tunapaaza sauti zetu.

"Hatutakiwa kukatisha ndoto za watoto wa kike tuwaache watimize ndoto zao za kumaliza masomo yao na hivyo kusaidia kuweza kujenga familia na kuondoa changamoto ya mimba za utotoni"

Jaji Mstaafu Munuo alisema kuwa alipata wakati mgumu Sana alipoenda kanisani na kuwakuta wasichana wengi wakiwa na watoto alipouliza mama zao wapo wapi alijibiwa ndio hao hivyo suala hili sio la kuacha ni jukumu letu kuanza kulingalia na kulipatia ufumbuzi wa kudumu kuondoa mimba za utotoni.

Kwa upande wake Mbunge wa bunge la EALA kutoka Rwanda Mh.Francoise Uwumukiza alisema kuwa siku hiyo ni muhimu kwa wanawake kutafakari na kujitambua ili kuondoa changamoto zao kwa jamii inayowazunguka.

Alisema kuwa kwa msingi huo kila mwanamke akisimama na kujitambua changamoto zetu zitakuwa historia na hivyo kufikia malengo ya Kimataifa na kupata haki zetu za msingi ikiwemo umiliki wa ardhi na kuondoa mimba za utotoni.

"Suala hilo la umiliki wa Ardhi kwenye jamii zetu limekuwa changamoto kwa kinamama kupata haki zao za msingi na linaondoa utu wetu kwenye jamii hususani pia mimba za utotoni nazo zinakatiza ndoto zetu kufikia malengo"

Share To:

Arusha Newsroom

Post A Comment: