Mkurugenzi wa Kituo cha Faraja Singida, Sr Catherine Grady (wa kwanza kulia) akiwa na baadhi ya wafanyakazi wa kituo hicho kwenye banda lao la maonyesho katika maadhimisho ya siku ya wanawake duniani, eneo la shule ya sekondari Mwenge mkoani Singida jana.
 Mgeni rasmi wa maadhimisho ya siku ya wanawake duniani kwa mkoa wa Singida, Aysharose Mattembe akisikiliza jambo kutoka kwa mmoja wa wafanyakazi wa Faraja Centre kwenye kilele cha siku ya wanawake mkoani Singida jana.
Baadhi ya watoa huduma wa Kituo cha Faraja mkoani hapa.
Na Godwin Myovela, Singida
SUALA la kupambana na biashara haramu ya ulanguzi wa binadamu sambamba na kusaidia watoto waishio katika mazingira magumu vinapaswa kupewa msukumo wa kipekee kuanzia ngazi ya kaya mpaka taifa ili kulinda wahanga- hususani makundi ya watoto na wasichana ambao wengi wao hujikuta wakitumbukia katika majanga mbalimbali ikiwemo kupata maambukizi ya VVU/UKIMWI kwa kigezo cha umaskini.
Akizungumza kwenye kilele cha siku ya wanawake, mkoani hapa jana, mratibu wa Mradi kutoka Kituo cha Faraja, Stella Mwagowa alisema  Kituo hicho kwa kushirikiana na serikali, pamoja na Shirika lisilo la kiserikali la ‘CHTEA’ lililopo nchini Kenya  wamefanikiwa kuokoa wahanga wapatao 8 na wengine 5 nje ya Tanzania ambao tayari walikuwa wamelanguliwa.
“Watoto wengi wamekuwa wakichukuliwa majumbani na kupelekwa kusikojulikana kwa kigezo cha kwenda kutafutiwa ajira, lakini ukijaribu kufuatilia utakuta wengi huishia kupelekwa kwenye majumba ya starehe, na wengine kufanyishwa biashara za ukahaba kwenye maeneo mbalimbali kama kivutio cha biashara za watu kinyume na matarajio na bila ridhaa yao,” alisema.
Mwagowa aliwataka wazazi na jamii, na hasa kwenye ngazi  ya mtaa kuwa na uelewa katika utambuzi na ufuatiliaji wa kina kujua wanapomtoa mtoto ndani ya familia au mtaa ni lazima mzazi awe na uhakika kujua mtoto anapokwenda.
Katika kukabiliana na tatizo la biashara haramu, pamoja na mambo mengine, alisema kituo cha Faraja kimejikita katika kutoa elimu na kuhamasisha kwenye uongozi ngazi za mitaa ili ikiwezekana kabla mtoto hajaondoka basi sharti uongozi wa mtaa husika upewe taarifa.
Lakini pia kupitia kituo hicho kumeanzishwa Jukwaa  la wadau wakiwemo Kituo cha Faraja, Jeshi la Polisi, Ustawi wa Jamii, Takukuru, Serikali za Mitaa, Wajasiriamali, Uhamiaji , Hospitali na wadau wengine, ambalo pamoja na mambo mengine, azma yake ni kufanya kazi kwa pamoja na umoja katika kuhakikisha kesi zote zinazoibuliwa na kusajiliwa kuhusiana na biashara haramu ya ulanguzi wa binadamu na madhara ya ukatili wake haziishii njiani.
“Pia kwa baadhi ya shule za msingi na sekondari ndani ya manispaa ya Singida tayari tumeanzisha “clubs” za wanafunzi, mambo haya ya mtoto kupewa pipi, biskuti kisha anaishia kubakwa hayakubaliki! tunaendelea kutoa elimu kwa wanafunzi, viongozi wa dini, makanisa na misikiti zikiwa ni shabaha za kusambaza jumbe mbalimbali za kukabiliana na hali hiyo,” alisema Mwagowa.
Akizungumzia namna Faraja kinavyosaidia watoto walio katika mazingira magumu, Afisa Ustawi wa Jamii kutoka kituo hicho, Fatuma Jumanne, alisema mpaka sasa idadi ya watoto waliofikiwa na kupatiwa huduma stahiki ndani ya manispaa ya Singida imefikia 115, wakiwemo wanafunzi wa shule za msingi, sekondari na vyuo
Bi. Jumanne alisema kituo kimekuwa kikiwapa huduma zote muhimu kwa mahitaji ya shule ikiwemo kuwalipia ada za shule na michango mbalimbali, sanjari na huduma za mahitaji ya vifaa vya kujifunzia
“Niombe sana kuwepo na ushirikiano kwa ngazi zote ndani ya jamii katika kufuatilia mienendo na tabia za watoto, wazazi na jamii ni wajibu wetu kuwa karibu na hawa watoto tujikite katika malezi ipasavyo…akitoka shuleni fuatilia amejifunza nini au ana changamoto gani, kuwa karibu na mtoto, usimwache,” alisema Jumanne.
Tangu kuanzishwa kwake Faraja Centre zaidi kimejikita katika kutoa ushauri nasaha na huduma za upimaji wa VVU/UKIMWI, kusaidia watoto walio katika mazingira magumu kwenye nyanja mbalimbali, kupambana na biashara haramu ya ulanguzi wa binadamu kwa kutoa elimu na shughuli za uokozi, sambamba na huduma ya ‘Tiba Shufaa’ kwa wagonjwa wasiojiweza.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: