Mamlaka ya Dawa na vifaa tiba nchini TMDA , imetambulika na Shirika la Afya Duniani (WHO) katika ubora wa udhibiti wa dawa na kuifanya Tanzania kupitia mamlaka hiyo kuwa ya kwanza barani Afrika kufikia mafanikio hayo.

Pia TMDA  imekuwa mshindi wa kwanza kwa ubunifu wa mfumo wa utoaji huduma kwa wananchi katika wiki ya Utumishi wa umma barani Afrika mwaka 2019.

Hayo yamebainishwa Jijini Dar es Salaam na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMDA Adam Fimbo, alipokutana na waandishi wa habari kuzungumzia mafanikio ya Taasisi hiyo katika kipindi cha miaka minne ya mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Tano, inayoongozwa na Dkt.John Pombe Magufuli.


Amesema katika kipindi hicho TMDA imefanikiwa kushikilia cheti cha kimataifa cha ithibati cha ISO 9001:2015 ambapo maabara ya Taasisi hiyo inatambuliwa na shirika la Afya Duniani kutokana na ubora na umadhubuti wa kazi zake.

“Katika kipindi cha Miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Tano, chini ya Jemedari wetu Rais Magufuli sisi kama taasisi tumefanya mambo mengi makubwa ambayo yameleta mageuzi katika masuala ya udhibiti na usalama wa Dawa na vifaa tiba, na tumeimarisha na kuongeza wigo wa ukusanyaji wa mapato” Alisema Kaimu Mkurugenzi huyo wa TMDA.

Aidha amesema TMDA imesajili zaidi ya bidhaa 20,247 za dawa na vifaa tiba baada ya kujiridhisha ubora ,usalama na ufanisi wake hivyo kuongeza wigo wa upatikanaji wa bidhaa kwaajili ya kulinda afya za watanzania.

Mamlaka pia imeimarisha udhibiti wa bidhaa kwa asilimia 96 katika kipindi cha mwaka 2015 hadi Novemba 2019 hivyo kuifanya nchi yetu kuwa salama, pia mamlaka imeweza kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kujenga maabara ya kisasa Jijiji Mwanza.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu huyo wa TMDA amesema Serikali ya Awamu ya Tano imeendelea kuwekeza katika taasisi hiyo ili kulinda afya za watanzania , kwa kuongeza bajeti kutoa Shilingi Bilioni 34.64  mwaka 2015/16 hadi Shilingi Bilioni 53.31 kwa mwaka 2018/19 ambayo ni sawa na asilimia 53.8.

Mafanikio hayo yamewezesha kuimarika kwa huduma pamoja na kiuwezesha taasisi kutoa gawio kwa serikali kila mwaka hadi kufikia shilingi Bilioni 29.1 katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Tano.

Katika kuelekea Tanzania ya Viwanda TMDA imetoa msaada wa kiufundi katika kuanzishwa kwa viwanda vipya 12 vya dawa na vifaa tiba hivyo kuchangia katika juhudi za kukuza uchumi kupitia viwanda, na katika kutimiza adhma hiyo imeanza kutumia mfumo wa kielektroniki katika utoaji wa vibali ambapo hutolewa kwa saa 24.

Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba TMDA  ni Taasisi ya Serikali chini ya Wizara ya Afya iliyoundwa kwa mujibu wa Sheria baada ya kufanyiwa marekebisho ya kiutendaji ya aliyokuwa Mamlaka ya na baadhi ya majukumu yake kuhamishiwa katika shirika la Viwango Tanzania TBS.

Share To:

Francis Godwin Mzee wa matukiodaima

Post A Comment: