Waziri
wa Kilimo Mhe. Japhet Hasunga akiwasilisha makadirio ya mapato na
matumizi ya fedha ya Wizara ya Kilimo kwa mwaka 2018/2019 Bungeni Jijini
Dodoma jana tarehe 17 Mei 2019. (Picha Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo)
Waziri
wa Kilimo Mhe. Japhet Hasunga jana tarehe 17 Mei 2019 ameliomba Bunge
kulidhia na kupitisha kiasi cha Shilingi Bilioni 253 kwa ajili ya
kugharamia matumizi ya kawaida na miradi mbalimbali ya maendeleo ya
Sekta ya Kilimo kwa mwaka wa Fedha wa 2018/2019.
Akisoma
Bajeti kuhusu makadirio ya mapato na matumizi ya Fedha za Wizara ya
Kilimo kwa Mwaka 2019/2020, Waziri wa Kilimo, Mhe. Japhet Hasunga
amesema, Serikali imepanga kubadilisha kilimo kutoka kuwa cha kujikimu
na kuwa kilimo cha kibiashara kama ilivyoainishwa katika Dira ya Taifa
ya Maendeleo 2025.
Aidha,
Mpango wa Pili wa Taifa wa Maendeleo umesisitizia mapinduzi ya viwanda
na umeitambua Sekta ya Kilimo kuwa mhimili imara kwa ajili ya
upatikanaji wa malighafi za viwanda. Miongozo
hiyo ya Kitaifa, pamoja na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015 na
Sera ya Kilimo ya mwaka 2013, inatekelezwa na Wizara kupitia Programu ya
Kuendeleza Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II) ambayo inalenga
kuleta mageuzi katika Sekta ya Kilimo na kwa kutambua umuhimu wa
kuongeza mitaji, teknolojia na ubunifu, Sekta Binafsi inashirikishwa
kikamilifu katika utekelezaji wa ASDP II.
Mhe.
Hasunga ameongeza kuwa Fedha nyingi katika kiasi hicho cha Bilioni 253
zitaelekezwa kwenye utekelezaji wa Programu ya Maendeleo ya Kilimo Awamu
ya Pili (ASDP II) iliyozinduliwa rasmi tarehe 4 Juni, 2018 na
Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, ambayo inalenga kubadilisha maisha ya mkulima kwa kufanya
mageuzi makubwa kwenye kilimo kwa kuzingatia mazao ya kipaumbele
kulingana na ikolojia za kilimo.
Akizungumzia
kuhusu upatikanaji wa chakula katika mwaka 2018/2019 Waziri Hasunga
amesema upatikanaji wa chakula kwa mwaka 2018/2019 ulifikia tani milioni
16.89 zikiwemo tani milioni 9.53 za mazao ya nafaka na tani milioni
7.35 za mazao yasiyo nafaka. Kiwango hicho cha uzalishaji kimeiwezesha
nchi kujitosheleza kwa mahitaji yake ya chakula ya tani milioni 13.56 na
hivyo kuwa na ziada ya tani milioni 3.32 za chakula kwa kiwango cha
utoshelevu cha asilimia 124.
“Niwahakikishie watanzania kwamba, tunacho chakula cha kutosha nchini. Hata
hivyo, tuendelee kuweka akiba katika kaya zetu hadi tutakapovuna tena
kwani inaonekana kwamba huenda tusiwe na mavuno mazuri sana msimu huu
kutokana na uhaba wa mvua kwenye maeneo ya Kanda ya Ziwa, Kati na
Kaskazini mwa nchi yetu”. Amekaririwa Waziri Hasunga.
Kuhusu
kilimo cha umwagiliaji, Mhe. Hasunga amesema katika mwaka 2018/2019,
Wizara kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji imekamilisha mapitio ya
Mpango Kabambe wa Taifa wa Umwagiliaji wa mwaka 2002 ili kubaini maeneo
yanayofaa kwa kilimo cha umwagiliaji kwa kuzingatia Mipango Shirikishi
ya Maendeleo ya Rasilimali za Maji. Katika mpango huo, hekta 560,880
zimepangwa kuendelezwa kwa lengo la kuongeza eneo la umwagiliaji kutoka
hekta 475,052 mwaka 2018/2019 hadi hekta 1,000,000 ifikapo mwaka 2035.
Waziri
Hasunga ameuzungumzia Ushirika na kusema Wizara kupitia Tume ya
Maendeleo ya Ushirika imeendelea kuimarisha Sekta ya Ushirika kwa
kusimamia na kuhamasisha maendeleo yake. Vyama vya Ushirika vimeongezeka
kutoka vyama 10,990 Desemba 2017 hadi vyama 11,331 kufikia Desemba
2018. Vilevile, idadi ya wanachama wa vyama vya ushirika imeongezeka
kutoka 2,619,311 mwaka 2017 hadi 3,998,193 Februari, 2019 sawa na
ongezeko la asilimia 53.
Hadi
Desemba 2018, mikopo yenye thamani ya Shilingi trilioni 1.3 imetolewa
kwa wanachama ikilinganishwa na Shilingi bilioni 902 iliyotolewa kufikia
Desemba 2017.
Aidha, Akiba na Amana za wanachama katika SACCOS zimefikia Shilingi bilioni 575 na hisa Shilingi bilioni 79.
Bunge
litaendelea kujadili hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Kilimo ya Mwaka
2018/2019 kwa siku mbili ambapo Jumatatu tarehe 20 Mei, 2019 inakuwa
siku ya kuhitimisha majadiliano hayo na kupitisha makadirio ya mapato na
matumizi ya Fedha za Wizara ya Kilimo kwa Mwaka 2019/2020
MWISHO.
Post A Comment: