Mkurugenzi Mtendaji mpya wa Benki ya CRDB Abdulmajid Nsekela akitoa taarifa yake ya mwaka 2018 kwenye Mkutano Mkuu wa 24 wa Wanahisa wa benki hiyo leo Mei 18, 2019 uliofanyika Kituo cha Kimataifa ya Mikutano, Ukumbi wa Simba jijini Arusha. (Picha na Yusuph Mussa).
Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa 24 wa Wanahisa wa Benki ya CRDB. Kikao hicho kimefanyika leo Mei 18, 2019 kwenye Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (AICC), Ukumbi wa Simba jijini Arusha. (Picha na Yusuph Mussa). 
 
Na Yusuph Mussa, Arusha

MKURUGENZI Mtendaji mpya wa Benki ya CRDB Abdulmajid Nsekela amesema wamejipanga kukabiliana na ushindani kwa siku zijazo ikiwa ni pamoja na kuwa wabunifu zaidi hasa katika kuongeza huduma kwa njia za kielektroniki.


Akitoa taarifa ya utendaji wa benki hiyo kwa mwaka 2018, leo Mei 18, 2019 kwenye Mkutano Mkuu wa 24 wa Wanahisa wa Benki ya CRDB uliofanyika kwenye Kituo cha Kimataifa cha Mikutano (AICC) Ukumbi wa Simba jijini Arusha, Nsekela alisema sekta ya fedha kwa siku zijazo itakabiliwa zaidi na  kasi kubwa ya ubunifu na mabadiliko ya teknolojia.



"Sekta ya fedha kwa siku zijazo itakabiliwa zaidi na  kasi kubwa ya ubunifu na mabadiliko ya teknolojia. Sambamba na hali hiyo, matarajio ya wateja yataendelea kuongezeka kadri ushindani unapoongezeka. Mwaka 2019, benki na kampuni zake tanzu zitaendelea kuwekeza katika kukuza biashara, watu na bidhaa ili kuboresha huduma kwa wateja. 





"Tutatumia kikamilifu ukubwa na upeo wetu kuboresha faida wanayopata wateja wanapotumia bidhaa zetu huku tukihakikisha kunakuwa na utamaduni imara wa kudhibiti vihatarishi na kujielekeza kuwa na ufanisi wa hali ya juu kiutendaji. Lengo letu ni kufanya mageuzi ya kibiashara ili kuwa benki bora kwa wateja wadogo na wakubwa kwa kujenga kampuni yenye mtandao mpana wa huduma unaowezeshwa na ubunifu wa kidijitali" alisema Nsekela.





Nsekela alisema wataongeza wigo wa huduma zao ili kufikia wilaya zote nchini kabla ya mwaka 2022 kwa kusajili mawakala wengi zaidi kila kona nchini kuendana na kauli mbiu yao isemayo 'Ulipo Tupo', na hatimaye kuhamasisha wateja wao wote watumie njia za kidijitali kupata huduma.





Alisema benki inatarajia kukamilisha ujenzi wa jengo la Makao Makuu, hatua ambayo itaboresha taswira ya benki hiyo. Pia benki na kampuni zake tanzu zinategemea kupata mafanikio zaidi mwaka huu kutokana na kuimarika kwa hali ya uchumi na usimamizi madhubuti wa mamlaka za usimamizi.





Nsekela pia alizungumzia mazingira ya utendaji, ambapo mfumo wa benki ulikuwa imara, na faida na mtaji kwenye sekta ya benki vilianza kuongezeka kutokana na usimamizi wa Benki Kuu (BoT). Hata hivyo, sekta ya benki ilikabiliwa na changamoto kutokana na mabadiliko ya taratibu na miongozo ya uendeshaji  ambayo ilisababisha BoT kuzifungia benki na taasisi tano za fedha kutokana na kutokuwa na mtaji wa kutosha. Kiwango cha mtaji katika sekta ya mabenki kilikuwa asilimia 16.3 na uwiano kati ya mikopo na amana ulikuwa asilimia 84.2 mwaka 2018.





Nsekela alisema benki ziliboresha taratibu za usimamizi wa mikopo ili kupunguza mikopo chechefu, ambayo ilipungua kutoka asilimia 11.9 mwaka 2017 hadi asilimia 10.4 mwaka 2018. Kuanza kutumika kwa utaratibu mpya wa kiuhasibu (IFRS9) kulibadirisha ukadiriaji wa hasara ya mikopo na kuongeza kiasi  kinachotengwa kwa ajili ya hasara ya mikopo na hatimaye kupunguza faida.





"Mazingira ya uendeshaji yaliathiriwa na mabadiliko makubwa ya teknolojia na kuongezeka ushindani kutoka kampuni za simu, Fintechs, taasisi ndogo za kifedha na taasisi za kifedha ambazo sio benki. Hata hivyo, benki inaendelea kuwekeza katika kujenga ushirikiano na kutafiti mitandao mbalimbali duniani ili kupata teknolojia iliyo bora zaidi. Kuongezeka kwa ushindani kumeifanya kupitia upya taratibu za uendeshaji na kuziboresha na kuhakikisha wateja wetu wanapata huduma kupitia njia mbadala za kidijitali" alisema Nsekela.





Nsekela alisema Benki ya CRDB pamoja na kampuni zake tanzu zilipata matokeo mazuri katika taarifa zao za pamoja za kifedha zikiwa na faida baada ya kodi ya sh. bilioni 64.1 iliyopatikana mwaka 2018. Faida kwa kampuni zote za CRDB ni sh. bilioni 642.7 ikiwa ni ukuaji wa asilimia sita (6) ikilinganishwa na mwaka 2017.





"Benki ilitumia teknolojia ya uhakika kuboresha utendaji na kuhakikisha  wateja wanapata huduma kwa uhakika, na kulingana na mahitaji yao. Ndani ya mwaka husika, gharama za uendeshaji zilikuwa sh. bilioni 428.9 ikiwa ni ongezeko la asilimia 7.4 ikilinganishwa na mwaka 2017. Gharama hizi ni ndogo  ikilinganishwa na ukuaji wa wastani wa miaka mitano hali ambayo imesababishwa na mikakati iliyotekelezwa ya kudhibiti gharama na mikakati ya mageuzi ya kidijitali.





"Faida iliyopatikana kwa benki na kampuni zake tanzu ilikuwa sawa na malengo yaliyowekwa, matokeo ambayo yanadhihirisha ubora na mikopo, usimamizi na taratibu, kwani pengo la hasara ya mikopo lilipungua kwa asilimia 24.8 hadi sh. bilioni 115. Jumla ya rasilimali ilikuwa kwa asilimia 2.3 na kufikia sh. bilioni 6,035.4 na amana za wateja zilikuwa kwa asilimia 8.4 kutoka sh. bilioni 4,687.2 hadi mwisho wa mwaka husika" alisema Nsekela.







"Nachukua nafasi hii kuwashukuru kwa mara nyingine wajumbe wa Bodi za Benki ya CRDB, CRDB Microfinance Services Company Ltd, CRDB Bank Burundi SA na CRDB Insurance Broker Limited kwa kujituma na jitihada waliyoonesha katika kuishauri menejimenti. Benki na kampuni zake tanzu zimefaidika kwa kiwango kikubwa kutokana na maarifa, ujuzi na weledi na wajumbe wa bodi.





"Natambua mchango wa Menejimenti na wafanyakazi kwa kujituma na hamasa waliyoonesha mwaka mzima. Pia napenda kuwapongeza wanahisa, wateja, Serikali, mamlaka za usimamizi na wadau wengine kwa kutuunga mkono katika kipindi chote cha mwaka 2018" alisema Nsekela.





MWISHO.
Share To:

Post A Comment: