Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma limekaa na kujadili utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya robo ya kwanza ya mwaka kuanzia Januari mpaka Machi kwa mwaka wa fedha 2018/2019.

Kikao cha Baraza la madiwani kimeshirikisha wakuu wa Idara mbalimbali za Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Watendaji wa Kata pamoja na waandishi wa habari ili kuweza kuwapasha wananchi kinachojadiliwa katika Kikao hicho.

Kikao kimeongozwa na Mwenyekiti wake, Mstahiki meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Prof. Devis Mwamfupe pamoja na Katibu wake ambaye ni Mkurugenzi wa Halmshauri ya Jiji la Dodoma, Godwin Kunambi.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika robo ya kwanza kwa mwaka huu, Kunambi alisema kuwa Halmashauri ya Jiji la Dodoma kupitia Idara ya Mipango Miji, Ardhi na Maliasili imepunguza kwa kiasi kikubwa migogoro sugu ya ardhi na kwamba idara kushirikiana na wadau wengine wameendelea kutekeleza majukumu ya Upangaji, Upimaji na uthamini wa viwanja. 

‘Kwa kipindi cha mwaka mmoja, Halmashauri ya Jiji la Dodoma limeweza kupima viwanja zaidi ya Laki 1, tofauti na CDA ambayo kwa miaka yote ilipima viwanja elfu 69 tu, na Kati ya viwanja hivyo tulivyopima tumetenga viwanja zaidi ya 2005 kwa ajili ya kumaliza kabisa migogoro ya ardhi katika Jiji la Dodoma’ Alisema Kunambi.

Kunambi aliendelea kusema kuwa kama Halmashauri ya Jiji la Dodoma ingeviuza viwanja hivyo kwa gharama nafuu kabisa vyenye ukubwa wa mita za mraba 480, Halmashauri ya Jiji ingeweza kupata mapato ya zaidi ya Bilioni 1.9, hela ambazo Halmashauri ingeweza kujengea shule, zahanati na huduma nyengine za jamii.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: