Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako leo amezindua mwongozo na mashindano ya ubunifu kitaifa mkoani Dodoma.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo ya uzinduzi Waziri Ndalichako amesema lengo la mashindano hayo ni kutambua na kuendeleza fikra za wabunifu kwa lengo la kuongeza ajira.
Prof. Ndalichako amesema katika kuimarisha uchumi wa viwanda lazima matumizi ya Sayansi, Teknolojia na ubunifu yaimarishwe kwa lengo la kuongeza tija viwandani na kwenye biashara.

“ Kutoka na umuhimu wa mashindano haya naielekeza Idara ya Sayansi , Teknolojia na ubunifu kuhakikisha mashindano haya yanafanyika kila mwaka, ili kukuza ujuzi, wabunifu kwa maendeleo ya viwanda,” alisisitiza Waziri Ndalichako.

Mashindano hayo yameshirikisha Makundi mbalimbali ya kijamii zikiwemo Shule za Sekondari, Vyuo vya Ufundi Stadi, Sekta isiyo rasmi, vyuo vya ufundi wa Kati, Vyuo vya Elimu ya Juu na Taasisi za utafiti na Maendeleo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Huduma za Maendeleo ya Jamii Mhe. Peter Serukamba amesema kuwa kuzinduliwa kwa mwongozo huo ni jambo kubwa na la kihistoria ikizingatiwa kuwa nchi inaelekea kwenye uchumi wa viwanda.

Serukamba amesema  bila Sayansi, Teknolojia na ubunifu nchi haiwezi kufanikisha malengo yake, hivyo ameiomba serikali ihakikishe inawekeza fedha nyingi.

“Kama hatutawekeza fedha za kutosha kwenye Sayasni, Teknolojia na Ubunifu hatuwezi kufanya kitu, hivyo tuwekeze fedha z kutosha ili tujiletee Maendeleo kwa haraka,” amesema Mhe. Serukamba.

Kauli mbiu ya mashindano hayo ni “kukuza ujuzi na ubunifu kwa uchumi wa viwanda.”

Imetolewa na:

KITENGO CHA MAWASILIANO SERIKALINI,

WIARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA.

14/11/2018
Share To:

msumbanews

Post A Comment: