Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limethibitisha kupokea barua ya Yanga yenye ombi la kujiondoa kwenye mashindano ya Kagame Cup yanayotarajia kuanza Juni 29 mpaka Julai 13 2018.

Kwa mujibu wa Ofisa wa Habari wa TFF, Clifford Ndimbo, amesema wamepokea barua hiyo inayoeleza kuwa Yanga ina nia ya kuwapa mapumziko wachezaji wake.

Barua hiyo iliyowasili katika makao makuu ya TFF, imesema Yanga inahitaji kuwapa muda wa kupumzika wachezaji wake kwa ajili ya mashindano ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Yanga itakuwa ina kibarua kizito kitakachopigwa nchini Kenya dhidi ya mabingwa wa ligi nchini humo kwa msimu wa 2017/18, Gor Mahia FC Julai 18.

Kutokana na muingiliano wa ratiba hiyo ya Kagame na CAF, Yanga wameona ni vema zaidi kuwapa wachezaji wake mapumziko ili kujiandaa kuelekea mechi hiyo ya kimataifa.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: