Wabunge wa CCM wamempongeza Rais John Magufuli anavyoshughulikia sekta ya madini ikiwamo kuzuia usafirishaji wa mchanga wa madini ya dhahabu ‘makinikia’ nje ya nchi.

Wabunge hao Goodluck Mlinga (Ulanga) na Sixtus Mapunda (Mbinga Mjini) wamesema hayo leo Juni 1, 2018 bungeni wakati wakichangia bajeti ya madini ya mwaka 2018/19.

“Nampongeza Rais (Magufuli) kwa kuzuia makinikia kupeleka nje ya nchi, Tanzania ni nchi ya nne kwa uzalishaji wa dhahabu kwa nchi za Afrika na duniani. Katika nchi matajiri wa uzalishaji wa mali tupo lakini mafanikio ya wananchi na Serikali tuko chini,” amesema Mlinga.

Amesema anampongeza Rais kwa kujenga ukuta katika mgodi wa Mirerani kwani ni madini adhimu.

“Tanzania ni nchi ya nne kwa uzalishaji wa gesi katika bara la Afrika. Lakini katika nchi masikini tupo,” amesema.

Akiendelea kuchangia, Mlinga amesema, Rais anapaswa kufanya mabadiliko katika wizara ya madini kwani watendaji wake wamesababisha haya.

Naye Mapunda amesema alichokifanya Rais ni jambo kubwa kwani tuna madini mengi lakini yalikuwa hayatunufaishi.

“Tuko katika mpito kutengeneza mfumo bora wa kutunufaisha na yote yanahitaji ushirikiano na kupeana moyo. Biashara ya dhababu ni ya familia kubwa na jinsi ya kuiingia inahitaji kutumia ubongo mkubwa sana,” amesema Mapunda na kuongeza:

“Ili kuingia kupambana nao inahitaji kuwa na mfumo mzuri na Serikali inapoanza kutengeneza sheria, hawa hawawezi kukubali, lazima watatuhujumu.”
Share To:

msumbanews

Post A Comment: