Serikali imehaidi kuendelea kushirikiana na wadau wa Sekta ya Elimu katika kuhakikisha watoto wa kitanzania wanapata  Elimu iliyo bora ili kufikia malengo ya mkakati wa kuwa na uchumi wa viwanda.

 Hayo yamesemwa leo na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mheshimiwa Wiliam Ole Nasha jijini Dar es Salaam katika kikao cha pamoja kilichowakutanisha Wadau wa Elimu walio chini ya Shirika la  Maendeleo ya Kimataifa ya Uingereza-DFID
Naibu Waziri Ole Nasha amesema ushirikiano wa serikali ambao umekuwepo kwa muda mrefu na wadau hao wa Elimu DFID umechangia katika kuhakikisha mtoto wa Kitanzania anapata Elimu iliyobora.

“Elimu bora kwa kila mtoto wa kitanzania ndiyo msimamo wa Serikali, katika kutekeleza hilo sera ya Elimu bila malipo imekuwa  na baadhi ya chagamoto  na katika kukabiliana nazo ndiyo maana wamekuwepo wadau wa Elimu ambapo sasa wanafanya kazi kwa kushirikiana na Serikali ili kutimiza malengo yanayokusudiwa, kwani hatuwezi kuboresha Elimu kama kila mtu atafanya kazi peke yake, Umoja ni Nguvu.”amesema Mheshimiwa Ole Nasha.

Ole Nasha amesema mpaka sasa wadau hao wa  Elimu kupitia Mpango wa Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R) wameshatoa  kiasi cha zaidi ya bilioni 200 ambazo zimekusudiwa kufanya uboreshaji wa Miundombinu ya shule za msingi na Sekondari, pamoja na kukarabati na kujenga vyuo vya Ualimu.

Naye Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Kimataifa ya Uingereza-DFID Jane Miller ameishukuru serikali ya Tanzania kwa ushirikiano ambao wamekuwa wakiupata katika kuhakikisha fedha zinazotolewa zinatumika kama zilivyokusdiwa. Kikao hicho kimewashirikisha wadau wa Elimu kutoka EQUIP –T, EP4R,HDIF,GPE, British Council, GPE, na RISE

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano Serialini
WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA

6/6/2018
Share To:

msumbanews

Post A Comment: