Hospitali  ya Taifa Muhimbili (MNH), imekiri kuharibika kwa moja ya mashine zake za CT-Scan hali inayolazimu wagonjwa kupimwa kwa kutumia mashine moja ambayo ni mpya.

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Umma na Huduma kwa Wateja wa Muhimbili, Aminiel Aligaesha alithibitisha kuharibika kwa mashine hiyo jana.

“Ni kweli mashine yetu moja ya CT Scan, ile ambayo ilikuwa inatumika kwa muda mrefu hapa hospitalini imeharibika si chini ya miezi mitatu sasa,” alisema.

Eligaesha alisema hivi sasa madaktari wanalazimika kuwafanyia uchunguzi wagonjwa katika mashine mpya iliyonunuliwa na Serikali miaka miwili iliyopita.

“Hii mpya haina tatizo lolote, MOI (Taasisi ya Mifupa Muhimbili), wanatarajia kufunga CT-Scan mpya, tutakuwa tunashirikiana nao kuwachunguza wagonjwa,” alisema.

Alipoulizwa iwapo pamoja na ushirikiano huo, Muhimbili itanunua mashine mpya nyingine ya CT-Scan, alisema hawana mpango huo kwa sasa.

“Mashine hizi ni gharama kubwa mno, ni kati ya Sh. bilioni mbili hadi tatu hivi, kwa kuwa MOI watafunga, tutaendelea kushirikiana nao pamoja na yetu kusaidia wagonjwa,” alisema.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: