Mwanasiasa wa upinzani aliyezuiwa kuingia Kenya wiki iliyopita na kusafirishwa kwa lazima hadi Dubai ameelekea nchini Canada, vyombo vya habari nchini Kenya vimeripoti.

Bw Miguna Miguna, ambaye ni wakili, amesafiri kwa ndege iliyokuwa ikielekea Toronto, Canada, baada ya kukaa katika uwanja wa kimataifa wa Dubai kwa siku nne.

Gazeti la Nation, limesema afisa mmoja wa serikali amewafahamisha kwamba Bw Miguna aliondoka Dubai akitumia ndege ya Air Canada 57 (ACA57) baada ya kuwasilisha pasipoti yake ya Canada.

Wakili huyo alikuwa amesema hakuwa na pasipoti hiyo alipowasili uwanja wa ndege wa Jomo Kenyatta, Nairobi Jumatatu wiki iliyopita.
Wakili wake Cliff Ombeta hata hivyo ameambia BBC kwamba mteja wake hakuwa na pasipoti hiyo.

Aidha, amesema kwa sasa hawezi kuthibitisha iwapo Bw Miguna yumo safarini kuelekea Canada.

Safari ya ndege kutoka Dubai kwenda Toronto huchukua takriban saa 13.


Bw Miguna ndiye aliyeidhinisha kiapo cha Bw Raila Odinga alipokuwa anajiapisha kuwa 'Rais wa Wananchi' mwezi Januari.

Bw Miguna Miguna alijaribu kurejea Kenya Jumatatu lakini akazuiwa kuingia baada yake kudaiwa kutowasilisha pasipoti ya Canada ambayo ilitumiwa kumsafirisha kwa nguvu hadi Canada.

Wakili huyo alisisitiza kwamba ni raia wa Kenya na hafai kuzuiwa kurejea.

Taarifa zinasema Bw Miguna, ambaye pasipoti yake ya Kenya ilitwaliwa na polisi kabla ya kuondolewa kwake Kenya mwezi jana, alikuwa ametakiwa kuwasilisha ombi la kupata visa ya kukaa Kenya kwa miezi sita kwa kutumia pasipoti hiyo yake ya Canada.

Alikataa jaribio hilo na badala yake kutoa kitambulisho chake cha taifa kuonesha kwamba yeye ni Mkenya na kutaka aruhusiwe kuingia.

Bw Miguna, aliyekuwa amewasili uwanja wa ndege wa kimataifa wa Jomo Kenyatta mwendo wa saa nane adhuhuri, alikesha kwenye uwanja huo.

Maafisa walijaribu kumsafirisha kutoka uwanja huo mara ya kwanza kwa kutumia ndege ya shirika la Emirates ambayo ilikuwa inaelekea Canada kupitia Dubai usiku huo wa Jumatatu lakini hawakufanikiwa.
Hata hivyo, walifanikiwa usiku wa kuamkia Jumatano.

Bw Miguna asubuhi aliandika kwenye Facebook kwamba aliamka na kujipata yuko Dubai na kwamba anahitaji matibabu.

Mwanasiasa huyo alisema alisindikizwa na afisa wa idara ya ujasusi na kwamba amemuona daktari uwanja wa ndege.

Bw Miguna alisisitiza kwamba hatasafiri kwenda popote ila kurejea Nairobi.

Serikali imechukua hatua hiyo licha ya kuwepo kwa maagizo ya mahakama ya kuzuia kutimuliwa kwake na ya kuitaka serikali kufanikisha kurejea kwake nchini humo.

Jaji wa Mahakama Kuu George Odunga aliwapata na hatia waziri wa usalama nchini humo, mkuu wa polisi na mkuu wa idara ya uhamiaji ya kukaidi maagizo ya mahakama iwapo wangekataa kumwachilia huru.

Aliwatoza faini ya Sh200,000 (Dola 2,000) kila mmoja.

Kukamatwa kwa Miguna mara ya kwanza
Bw Miguna alikamatwa na polisi kwa mchango wake katika kuapishwa kwa Bw Odinga kuwa "rais wa wananchi", hafla iliyofanyika uwanja wa Uhuru Park, Nairobi mnamo 30 Januari.

Bw Miguna, ambaye pia ni wakili, ndiye aliyetia saini hati ya kiapo ya Bw Odinga.

Serikali ilikuwa imeeleza hatua hiyo ya kiongozi huyo wa upinzani kuwa uhaini wa hali ya juu.

Bw Odinga anadai kwamba alimshinda Rais Uhuru Kenyatta katika uchaguzi mkuu wa 8 Agosti ambao matokeo yake yalifutiliwa mbali na Mahakama ya Juu kwa sababu ya kutokea kwa kasoro nyingi.

Mahakama iliamuru uchaguzi mpya ufanyike lakini Bw Odinga akasusia uchaguzi huo mnamo 26 Oktoba.

Chini ya Kifungu 17 cha Katiba ya Kenya, mtu aliyezaliwa nchini Kenya anaweza tu kuupoteza uraia wake iwapo itabainika kwamba aliupata uraia huo kwa njia ya ulaghai, au ibainike kwamba mtu huyo au wazazi wake walikuwa raia wa nchi nyingine, au ibainike kwamba mtu huyo alikuwa na umri wa zaidi ya miaka minane alipogunduliwa akiishi Kenya.

Serikali ya Kenya imekuwa ikisisitiza kwamba chini ya katiba ya zamani, Wakenya hawangekuwa na uraia wa nchi mbili.

Serikali inasema hatua ya Bw Miguna ya kupata pasipoti ya Canada mwaka 1988 ina maana kwamba aliupoteza uraia wa Kenya wakati huo.

Raila Odinga: ''Hatutambui uchaguzi wa Uhuru Kenyatta''
Ingawa Bw Miguna aliwasilisha maombi na akapewa pasipoti ya Kenya mwaka 2009, serikali inasema pasipoti hiyo ya Kenya si halali kwa sababu hakufichua kwamba wakati huo alikuwa raia wa Canada pia.

Serikali imesema mwanasiasa huyo hakuwasilisha tena ombi la kuruhusiwa kuwa raia wa Kenya katiba ilipofanyiwa marekebisho mwaka 2010 na Wakenya wakakubaliwa kuwa na uraia wa nchi mbili.

Bw Miguna amekuwa akisisitiza kwamba hakuwahi kuukana uraia wake wa Kenya na kamwe hawezi kufanya hivyo.

"Katiba iko wazi kabisa: hakuna mtu yeytoe anayeweza au anayeweza kudai kuufuta uraia wa Mkenya aliyezaliwa nchini Kenya," alisema awali.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: