Dar es Salaam.  Shughuli katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu zilisimama kwa muda baada ya kutokea kwa hitilafu ya umeme katika transfoma ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) iliyopo katika eneo la mahakama hiyo.

Trasfoma hiyo imelipuka na kusababisha nyaya mbili kushika moto na kuzua hofu miongoni mwa watu waliokuwa mahakamani hapo, kuanza kukimbia hovyo, Tukio hilo limetokea leo asubuhi Machi 1, 2018 wakati kesi mbalimbali zikiendelea kusikilizwa.

Akizungumza na MCL Digital, Mtendaji wa Mahakama Mkoa wa Dar es Salaam, Gasto Kanyairita amesema baada ya kutokea kwa mlipuko huo ulizuka moto  na kushika nyaya mbili, ikiwemo ya intaneti ambazo hutumiwa kwa ajili ya mawasiliano ya simu.

"Moto uliingia moja kwa moja katika jengo letu na kushika seva yetu ambayo tunatumia kwa ajili ya mawasiliano ya simu,” amesema.

"Baada ya kushika nyaya hizo,  moto huo uliambaa amba na kuingia katika chumba cha Tehama na kisha kushika soketi ya umeme iliyopo ndani ya jengo la mahakama.”

Baada ya kutokea kwa hitilafu hiyo ya umeme,  askari polisi walikuwepo mahakamani hapo,  alitumia vidhibiti moto na kufanikiwa kuuzima.

Dakika tano, baada ya kutokea kwa hitilafu hiyo,  gari la zimamoto lilifika mahakamani hapo na kukuta tayari moto huo umezimwa.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: