Mihogo ni miongoni mwa mazao ya mizizi ambayo ni muhimu sana kwa chakula, hasa maeneo yenye mvua kidogo na sehemu zenye ukame. Mihogo hutumika kama zao la kinga ya njaa ambapo mizizi yake hutumika kama chakula na majani yake pia hutumika kama mboga.

Kutokana na baadhi ya maeneo ya nchi yetu kuwa na ukame, wataalamu wa kilimo wanasisitiza na kushauri mazao ya kinga ya njaa yalimwe. Na Mihogo ni miongoni mwa mazao hayo.
Kwa hiyo basi, uangalizi wa shamba toka kuandaa shamba mpaka mavuno unatakiwa kuzingatiwa.

HALI YA HEWA ,UDONGO UFAAO NA UTAYARISHAJI WA SHAMBA.
Ni zao linalostahimili ukame,hustawi vizuri katika maeneo yenye joto la wastani kama ya ukanda wa pwani na yale ya mwinuko usiozidi mita 1500.

 Ili shamba la Mihogo listawi vizuri ni vyema lilimwe kwenye ardhi ya yenye rutuba ya wastani, udongo tifutifu au kichanga na mvua ya wastani. Unyevunyevu ukizidi na mbolea kuwa nyingi husababisha mhogo kukua sana sehemu ya juu na kutoa majani mengi.

Endapo mihogo inaoteshwa sehemu yenye udongo wa mfinyanzi au mzito, ambao unatuamisha maji, mihogo hushindwa kuweka Viazi itakiwavyo.

Pia sehemu zenye mawe siyo nzuri kwani huzuia mizizi kusambaa vizuri ardhini.Pia udongo au mchanga wenye asili ya chumvichumvi kwa wingi hufanya baadhi ya mbegu ambazo ni mihogo mitamu  kuwa na uchungu,mfano muhogo wa kiroba unaweza kuwa na uchungu kama utachelewa sana kuvunwa kutoka katika eneo la aina hii.

AINA
Kuna aina mbalimbali za mihogo. Baadhi ya Sifa zinazoangaliwa wakati wa kutayarisha Mbegu za Mihogo ni;-

  • Muda wa kukomaa
  • Mhogo mtamu au mchungu
  • Uwingi waavuno


Aina ya mihogo mitamu ni;-

  • Kibaha, 
  • Aipin Valeca, 
  • Msitu Zanzibar, 
  • Kigoma 
  • Kigoma red.
  • kiroba,
  • Binti Athumani,
  • Mzungu.


Aina ya mihogo michungu ni;- 
  • Liongo, 
  • Ali mtumba, 
  • Mapangano, 
  • Luanda, 
  • mzimbatala  
  • Lumbaga.


KUPANDA
Mihogo kama mazao mengine, Mkulima hana budi kuzingatia matumizi ya mboga bora ili aweze kupata mavuno mengi na bora.

Kwa kawaida Mihogo hupandikizwa kwa kutumia vikonyo au pingili zinazotokana na mihogo yenye Sifa zinazotakiwa.

Pingili ziwe zenye urefu wa wastani wa sentimita 25-30 na wastani wa macho 5-6, na unene wa sentimita 2-4. Mara nyingi sehemu ya shina ndiyo inayofaa kukata pingili.

Katika kilimo cha sesa, nafasi zinazopendekezwa ni meta 1 kwa meta 1. Katika kilimo cha Matuta nafasi zinazopendekezwa ni meta 1.5 kwa meta 0.75.

Mkulima asipande pingili changa au zilizokomaa na kuzeeka, na wakati wa kupanda ahakikishe macho 2-3 yako ndani ya ardhi. Aisha hakikisha kuwa pingili urefu wa sentimeta 10-15 unakuwa ndani ya ardhi.

Mkulima apande pingili kwa kulaza, nyuzi 45 (45°) yaani kimshazari kidogo na macho yatakayotoa machipukizi yawe yameelekea juu. Udongo ugandamizwe kudogo kwa mguu ili pingili ishike vizuri.

PALIZI
Ipaliliwe mapema inapokuwa hufunika ardhi hivyo majani huzuiwa kuota na kukua vizuri.

SAMADI NA MBOLEA ZA VIWANDANI
Mihogo hulimwa bila kutumia mbolea na inastawi vizuri hata katika udongo usio na rutuba ya kutosha,Matumizi ya mbolea za nitrogeni hayashauriwi katika kilimo cha muhogo labda kama unataka majani na si muhogo.

MAGONJWA
Zao la mhogo halina magonjwa mengi lakini ugonjwa wa "Cassava Mosaic" na Batobato ndiyo yanayoathiri sana uzalishaji wa zao hili.Ugonjwa huu husababishwa na virusi na huenezwa na nziwadogo weupe.Mmea ulioathirika ukitumika kwa vipando mche mpya nao utakuwa na ugonjwa huu.Majani ya mmea ulioshambuliwa yatakuwa na rangi ya njano na yasiyo na umbo la kawaida.

Kuzuia ugonjwa huu-panda aina ya muhogo inayostahimili ugonjwa huu,Panda vipandikizi ambavyo havijatoka katika mmea ulioathirika na ugonjwa huu,pia unaweza kuchovya mbegu ulizokata katika maji ya moto kwa muda mfupi na kwa tahadhari kubwa. Pia tumia dawa za wadudu kuua nzi weupe.

WADUDU
Mdudu hatari wa mihogo ni " Cassava green mite" ( Buibui wa mhogo) ambaye hupunguza mavuno kwa asilimia 40-80.

Wadudu wengine ambao wameonyesha madhara makubwa ni cassava mealy bugs ( vidung'ata) ambao wameleta madhara makubwa katika maeneo yalimayo mihogo.

Mihogo iliyoshambuliwa na wadudu Hawa itaonyesha dalili zifuatazo;-

  • Shina la mmea huonekana limezungukwa na utando mweupe (white mealy wax)
  • Kunyauka kwa majani ya mmea.
  • Mmea hudumaa
  • Shina la mmea huonekana limepinda
  • Majani ya mmea hupukutika
  • Mmea hufa.


Wadudu hupenda kushambulia majani machanga hasa Yale ya ndani ambako mmea huendelea kukua.

TIBA ZA KUTUMIA WADUDU
Kutokana na utafiti, wadudu Hawa wanaweza kuangamizwa kwa njia ya Asili (Biological control). Wataalamu waliagiza manyigu kutoka nje ya nchi pale tu ugonjwa huu iliposhamiri lakini njia hii ilionekana ni gharama kwa Mkulima wa kawaida.

Kinachoshauriwa ni kupanda Mbegu ambazo hazijashambuliwa na magonjwa.

Zuia wadudu hawa kwa dawa za wadudu kama vile DIMETHOATE, n.k

MUDA WA KUKOMAA.
Muda wa kukomaa unatofautiana kutokana na aina ya mhogo.
Ila mihogo mingi huanzia miezi sita hadi tisa na kuendelea

UVUNAJI
Ikiwa mihogo yako imekomaa ing'oe yote au chagua unayoitaka kuvuna.Epuka kuweka kidonda katika muhogo unaovuna ili kuepusha kuoza kwa urahisi.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: