Na Denis Chambi, Tanga.


MGOMBEA wa nafasi ya Urais kupitia chama cha Alliance Democratic Change (ADC) Wilson Elias Mulumbe ameahidi Serikali atakayoiongoza itahakikisha inarejesha viwanda vyote vilivyobinafsishwa pamoja na kufufua vilivyokufa ili viweze kuzalisha na hatimaye  kuwapatia wananchi ajira za kudumu hatua ambayo itainua uchumi wa mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.


Akizungumza katika mwendelezo wa kampeni zake mkoani Tanga Mulumbe amesema kuwa kutokana na ubinafsishwaji wa viwanda na vingine vikashindwa kuendelea kuzalisha kumechangia kwa kiasi kikubwa ukosefu wa ajira hususani kwa vijana ambao ndio Nguvu kazi ya Taifa.


Ameongeza kuwa pamoja na kuvirejesha viwanda hivyo ikiwemo vilivyokuwepo mkoani Tanga pia atahakikisha anajenga kiwanda cha kuchakata Samaki  ambao watakuza soko la ndani na nje ya nchi huku akiahidi kukaa upya na wawekezaji ambao walifunga viwanda vyao kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo kodi kuwataka wavifungue ili waweze kuzalisha ajira kwa watanzania.

" Wenzetu baada ya kubinafsisha viwanda hivi walitakiwa kuvisimamia lakini mwisho wa siku waliwaachia  mabepali ambao waliviua,  ahadi yetu kwa wananchi ni kwamba sasa tunaenda kuvifufua  na kuvirudisha mikononi mwa Serikali  na vijana wetu wataenda kufanya kazi"


"Viwanda vingi hapa Tanga vilifungwa kutokana na wingi wa kodi ambazo wawekezaji wameshindwa kulipa kwenye mamlaka  lakini sisi tutakapoingia madarakani tutawaita na kukaa nao wawekezaji wote ambao walifunga viwanda vyao  waendelee kufanya kazi ili kuzalisha ajira kwa watanzania" amesema na kuongeza


"Naomba mtuchague chama cha ADC ili viwanda vingi vilivyokufa ikiwemo kiwanda Cha Amboni  tutakifanya kuwa kiwanda Cha kuchakata minofu ya Samaki  na kutengeneza nyenzo za uvuvi wa Samaki ili kila mwezi tuweze kuvua tani 40 za Samaki ambazo zitachakatwa  na kupelekwa kwa walaji wa ndani na nje ya nchi yetu" amesema Mulumbe.


Mbali na hayo Mulumbe ameahidi endapo atachaguliwa October 29 kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Serikali yake itahakikisha inawalipa mishahara wenyeviti wa Serikali za mitaa ,vijiji na vitongoji ili kuwawezesha na kuwapa motisha ya kufanya kazi.

"Hata wenyekiti wetu wa Serikali za mitaa tutaweza kuwalipa mishahara mbali na kazi kubwa wanayoifanya lakini bado Serikali iliyopo madarakani haiwalipi chochote endapo mkitupa ridhaa ya kuiongoza hii nchi kuanzia mwishoni mwa mwaka huu wa 2025 tutaanza kuwalipa  mishahara hapo ndio wakati ambapo watafanya kazi kwa uadilifu  na kuweza kuwasaidia wananchi wetu" ameongeza mgombea huyo.


Awali akizungumza mwenyekiti wa Alliance Democratic Change 'ADC' Taifa Shabani Itutu ameeleza kero za wananchi ambazo zimekuwa zikielekezwa kwa Mahakama ma Jeshi la Polisi nchini ambapo  amesema kuwa utoaji wa haki umekuwa ukighubikwa na vitendo vya rushwa jambo ambalo limekuwa likiwanyima haki wanaostahili.


"Kuna malalamiko mengi ya wananchi juu ya Jeshi la Polisi unapopelekwa kituo chochote cha Polisi huwezi kutoka bila ya chochote hii sii haki kabisa wengine ni watu wa Mahakama  shida imekuwepo kwenye utoaji wa hukumu  watu wengi wenye maisha ya chini wanalalamika  hawapati haki mpaka watoe rushwa  tuwaambie tu kwamba nchi hii inafuata misingi ya sheria  na katiba ya nchi dhamana ni haki ya kila mtu na kupata haki ni haki ya kila mtu"


Aidha chama hicho cha Alliance Democratic Change (ADC) kimetumia kampeni hizo kumnadi mgombea ubunge kupitia chama cha Wananchi CUF wa Jimbo la Tanga Mussa Mbarouk  ikiwa ni ishara ya kumuunga mkono na kumuombea kura kwa wananchi ifikapo October 29 mwaka huu kwenye uchaguzi mkuu wa madiwani ,wabunge na Rais.


MWISHO.

Share To:

OSCAR ASSENGA

Post A Comment: