Na. Catherine Sungura,Dodoma

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI Mhe. Mohamed Mchengerwa ameipongeza Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kwa kazi kubwa wanayofanya tangu kuanzishwa kwakwe.

Waziri Mchengerwa ameyasema hayo jana wakati wa kikao chake na Menejimenti na watumishi wa TARURA kilichofanyika ofisi za TARURA zilizopo mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

Mhe. Mchengerwa amesema kuwa tangu kuanzishwa kwa Wakala huyo mwaka 2017 kumekuwa na ongezeko la barabara Za lami kutoka kilomita 1,449.55 hadi kilomita 3,053.26 sawa na ongezeko la  110% pia barabara za changarawe zimeongezeka kutoka kilomita 24,405.40 hadi kilomita 38,141.21 sawa na ongezeko lako la 56%.

“Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeongeza fedha za matengenezo,ukarabati na ujenzi wa barabara na madaraja kutoka Bilioni 275.03 mwaka 2020/21 hadi kufikia Bilioni 836.237 kWa mwaka wa fedha 2021/22,2022/23 sawa na ongezeko la 204% na mwaka huu 2023/2024”.Amesema Mhe. Mchengerwa.

Aidha, ameipongeza TARURA kwa kutumia teknolojia mbalimbali ikiwemo ujenzi wa barabara ya mawe (cobble stone roads) na madaraja ya mawe (stone arch bridges) na majaribio ya teknolojia nyingine katika kuboresha barabara wanazosimamia.

Hata hivyo ameitaka TARURA  kulipa kipaumbele jukumu la  kukuza na kuwaendeleza wakandarasi wazawa ili kutoa mchango mkubwa kwa Taifa na kuwataka kuwatambua makampuni ya wakandarasi ishirini kila mkoa.

Naye,Mtendaji Mkuu wa TARURA Mhandisi Victor Seff amesema wataendelea kufanya kazi ili kutimiza malengo ya TARURA na kuhusu kukuza wakandarasi wazawa amesema watashirikiana na bodi ya wakandarasi nchini pamoja na taasisi za kifedha.

Matumizi ya teknolojia mbadala Mhandisi Seff amesema teknolojia hiyo ndio muelekeo wa TARURA wa kupunguza gharama na kutunza mazingira.

Share To:

Post A Comment: