Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi amewataka wahifadhi wasiokuwa tayari kutekeleza misingi ya pamoja waliyojiwekea katika kuhakikisha misitu inahifadhiwa nchini kutafuta mahala pengine pa kazi huku akieleza kuwa nyakati tamu na chungu zinakuja.


Akizungumza leo Aprili 8, 2023 wakati alipokutana na menejimenti ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania – TFS kujadili, kuchakata na kupeana miongozo inayolenga kupeleka mbele majukumu ya uhifadhi waliyonayo, Dkt. Abbasi amesema anatambua umuhimu wa sekta ya misitu nchini na hayuko tayari kuona mtu yoyote anakwamisha uhifadhi nchini.


“Sekta hii ya misitu pamoja na kujishughulisha na mambo mengine kwenye misitu ni sekta ya kiuchumi, ni muhimu sana kwa uchumi wa taifa letu, inaingiza mabilioni ya fedha katika Serikali lakini pia kwenye uchumi wa nchi kwa ujumla wake,”. Amesema Katibu Mkuu.


Hata hivyo, Katibu Mkuu ameitaka menejimenti ya TFS kufikisha ujumbe kwa askari, maafisa na wafanyakazi wengine walio na mikataba na wale wasiopo kwenye kundi lolote lakini ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu ya TFS watambue Wizara na Serikali inatambua na kuthamini kazi wanayoifanya.


Aidha ametumia nafasi hiyo kuwataka watendaji wote kuacha kukaa ofisini na badala yake waende kusikiliza na kutatua changamoto zilizopo pamoja na kujenga uhusiano baina ya Wakala huo na wadau. 


“Kazi kubwa ya uhifadhi mnafanya lakini kama hamuwasiliana na wadau wenu ili wawaelewe, kuwaamini na kuwakubali ni kazi bure, imarisheni mawasiliano ya ndani na nje.”


 Pia Katibu Mkuu Dkt. Abbasi alitoa somo la siri nane za mafanikio ambazo Wizara inazitumia katika utendaji wao wa kila siku.

Share To:

Post A Comment: