Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki akifungua Mkutano wa 44 wa Wataalam wa Uzalishaji Mifugo Tanzania ambapo amewataka wataalam hao kutumia utaalamu wao kuwaelimisha wafugaji na wavuvi ili waweze kufuga kisasa. Mkutano huo umefanyika katika ukumbi wa Olasiti Garden Hotel Jijini Arusha.


Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Huduma za Ugani, Dkt. Angello Mwilawa akiwasalimia wajumbe wa Mkutano wa 44 wa Wataalam wa Uzalishaji Mifugo Tanzania ambapo pia alisema mkutano huo unawasaidia wataalam kutoka maeneo tofauti kubadilishana uzoefu. Mkutano huo umefanyika katika ukumbi wa Olasiti Garden Hotel Jijini Arusha.


Mwenyekiti wa Chama cha Wataalam wa Uzalishaji wa Mifugo Tanzania (TSAP), Dkt. Daniel Komwihangilo akitoa maelezo mafupi kuhusu chama hicho kwenye Mkutano wa 44 wa chama hicho ambapo amesema moja ya malengo yake ni kuhimiza maendeleo katika sayansi ya uzalishaji na uendelezaji wa mifugo hapa nchini. Mkutano huo umefanyika katika ukumbi wa Olasiti Garden Hotel Jijini Arusha.


Msajili wa Bodi ya Maziwa nchini ambaye pia ni Katibu Msaidizi wa TSAP, Dkt. George Msalya akiwatambulisha wajumbe walioshiriki Mkutano wa 44 wa Wataalam wa Uzalishaji Mifugo Tanzania kwa mgeni rasmi Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki. Mkutano huo umefanyika katika ukumbi wa Olasiti Garden Hotel Jijini Arusha.


Wajumbe wa Mkutano wa 44 wa Wataalam wa Uzalishaji Mifugo Tanzania wakifuatilia mada zilizokuwa zikiwasilishwa katika mkutano huo uliofanyika kwenye ukumbi wa Olasiti Garden Hotel Jijini Arusha.


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (kulia) akipokea zawadi ya maziwa kutoka kwa wawakilishi wa Kampuni za Kilimanjaro Fresh na Asas Dairies Ltd mara baada ya kumaliza kufungua Mkutano wa 44 wa Wataalam wa Uzalishaji Mifugo Tanzania uliofanyika katika ukumbi wa Olasiti Garden Hotel Jijini Arusha.


Picha ya Pamoja ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki (wanne kutoka kushoto waliokaa) na Wajumbe wa Mkutano wa 44 wa Wataalam wa Uzalishaji Mifugo Tanzania mara baada ya kumalizika kwa ufunguzi wa mkutano uliofanyika kwenye ukumbi wa Olasiti Garden Hotel Jijini Arusha.

..................................................................

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki amewataka wataalamu wa mifugo na uvuvi kutoa elimu ya kitaalam kwa wafugaji na wavuvi ili waweze kufuga kwa tija.

Waziri Ndaki aliyasema hayo leo (27.10.2021) wakati akifungua Mkutano wa 44 wa Wataalam wa Uzalishaji Mifugo Tanzania (TSAP) wenye kauli mbiu ya Uzalishaji Endelevu wa Mifugo na Samaki wakati wa janga la UVIKO 19 uliofanyika kwenye ukumbi wa Olasiti Garden Hotel jijini Arusha.

Kutokana na janga la UVIKO 19, wataalam wametakiwa kuongeza kasi katika utoaji elimu kwa wafugaji na wavuvi ili kuwapa mbinu bora zitakazowasaidia kuongeza uzalishaji na kuweza kukidhi soko la nyama na samaki ambalo kwa sasa linazidi kukua kutokana na kufunguka kwa masoko ya nje ya nchi kutokana na jitihada kubwa zinazofanywa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan za kufungua fursa za masoko ya mifugo na samaki nchi za nje haswa kwenye masoko ya Uarabuni, Ulaya na China.

Pia amewasihi wataalam walioshiriki mkutano huo kuishauri serikali haswa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuhusu namna bora ya kuongeza uzalishaji na kupunguza migogoro ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi. Waziri Ndaki amesema kuwa Wizara itaendeleza jitihada za kuhakikisha kuna kuwa na mazingira bora ya kufuga, kusindika na kufanya biashara ya mazao ya mifugo na uvuvi.

Lakini pia Waziri Ndaki amewasisitiza wafugaji kuendelea kununua maeneo kihalali kwa ajili ya shughuli za ufugaji na kuhakikisha wanayapima na kuyamiliki ili waondokane na migogoro. Vilevile amewasisitiza kuendelea kupanda malisho katika maeneo watakayoyamiliki ili kuondokana na tatizo la malisho kwa mifugo.

Naye Mwenyekiti wa Chama hicho cha TSAP, Dkt. Daniel Komwihangilo alisema lengo la chama hicho ni kuhimiza maendeleo katika sayansi ya uzalishaji na uendelezaji wa mifugo hapa nchini, kutoa fursa kwa wadau wote wa tasnia ya mifugo kukutana ili kubadilishana mawazo na uzoefu, na kushirikiana na wataalam na wanachama wa waliopo katika vyama vya taaluma chini katika sekta ya mifugo na uvuvi ili kuendeleza sekta hizo. Chama hicho kwa sasa kina wanachama zaidi ya 300 ambao wapo hai kutoka katika sekta mbalimbali.

Aidha, amemuomba Waziri kuangalia uwezekano wa kuunda chombo maalum cha kutambua na kuisimamia kada hiyo kisheria. Vilevile amemshukuru Waziri kwa ushirikiano anaoutoa katika kusimamia sekta ya mifugo na uvuvi na kwamba wao kama chama wataendelea kutoa ushirikiano kwa serikali katika kuhakikisha uzalishaji unaongezeka.
Share To:

emmanuel mbatilo

Post A Comment: