📌 Watembelea mradi kuona ufanisi wake

📌 Shilingi bilioni 118 zatumika kutekeleza mradi

📌 Watoa rai awamu ya pili kuanza kwa kasi


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imelipongeza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa usimamizi na utekelezaji mzuri wa Mradi wa Uzalishaji Umeme kwa nguvu ya Jua wa Kishapu wenye uwezo wa Megawati 50 unaotekelezwa katika Mkoa wa Shinyanga.

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Subira Mgallu, mara baada ya Kamati kutembelea mradi huo tarehe 13 Machi, 2026 kwa lengo la kujionea maendeleo ya utekelezaji wake pamoja na ufanisi wa matumizi ya fedha zilizotolewa na Serikali.

Akizungumza mara baada ya ziara hiyo, Mhe. Mgallu alisema mradi huo ni hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya nishati nchini kutokana na matumizi ya teknolojia ya nishati jadidifu.

“Tumetembelea mradi huu wa uzalishaji wa umeme kwa kutumia teknolojia ya jua na tunaona ni mapinduzi makubwa katika sekta ya nishati nchini. Hii ni hatua muhimu kwani kwa mara ya kwanza Tanzania inapata Megawati 50 za umeme kutoka kwenye nishati ya jua,” alisema Mhe. Mgallu.

Alisema Kamati imeridhishwa na namna fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo zimetumika ipasavyo na kufanikisha utekelezaji wa mradi huo kwa ufanisi.

“Kama Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, tumeridhishwa na matumizi ya fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya mradi huu. Tunaona wazi kuwa fedha hizo zimetumika vizuri katika utekelezaji wa mradi huu wenye thamani ya takribani shilingi bilioni 118,” alieleza.

Aidha, alisema mradi huo tayari umeanza kuchangia Megawati 50 katika Mfumo wa Gridi ya Taifa, hatua inayochangia kuongeza uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini pamoja na kuimarisha vyanzo mseto vya nishati.

“Utekelezaji wa mradi huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kunakuwa na vyanzo mbalimbali vya kuzalisha umeme. Hii inaongeza uhakika wa upatikanaji wa nishati ya umeme nchini,” alisema.

Kwa upande wake, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, alisema mradi wa Kishapu unatekelezwa kwa awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ya Megawati 50 tayari imekamilika na imeanza kuingiza umeme katika Gridi ya Taifa.

“Mradi huu una awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ya Megawati 50 tayari imekamilika na imeanza kuingiza umeme kwenye Gridi ya Taifa. Awamu ya pili itahusisha uzalishaji wa Megawati 100 zaidi na kufanya jumla ya Megawati 150 kutoka katika mradi huu,” alisema Mhe. Ndejembi.

Kamati hiyo imetoa Rai kwa Wizara ya Nishati na TANESCO  inaendelea kuendelea na  mikakati ya kuanza utekelezaji wa awamu ya pili ya mradi huo ili kuongeza zaidi uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini.

 


Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, ameitaka Menejimenti ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuhakikisha kuwa miradi ya mafuta na gesi asilia inayoendelea nchini inatekelezwa na kukamilika kwa wakati ili iweze kuendelea kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Dkt. Mataragio ametoa maelekezo hayo leo wakati alipokutana na menejimenti ya TPDC  kwa lengo la kujadili fursa zilizopo katika sekta ya Mafuta  na Gesi Asilia, changamoto pamoja na kuweka mikakati madhubuti ya kuimarisha sekta.

Aidha, Dkt. Mataragio ameiagiza TPDC, kuongeza vitalu vipya vya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji zaidi katika shughuli za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia.

“Ni muhimu TPDC ikaendelea kupanua maeneo ya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji zaidi katika shughuli za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia kama mnavyofahamu rasilimali hii ni muhimu katika kutoa uhakika wa nishati nchini mfano kwenye  uzalishaji wa umeme na kukuza uchumi wa viwanda." Amesisitiza Dkt.Mataragio

Kwa upande wake, Kamishna wa Petroli, Goodluck Shirima, amesema Serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia ili kuongeza matumizi yake katika sekta mbalimbali ikiwemo majumbani, viwandani na katika uzalishaji wa umeme.

Ameongeza kuwa Serikali inaendelea kutenga na kuandaa maeneo kwa ajili ya ushiriki wa sekta binafsi kwenye miradi ya usambazaji wa gesi, akibainisha kuwa miradi hiyo ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati (flagship projects) inayolenga kuongeza matumizi ya gesi asilia.

Naye,  Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Mussa Makame amesema Shirika hilo litaendelea kutekeleza maagizo  yanayotolewa na viongozi wa Wizara kwa lengo la kuzidi kuiimarisha sekta ya Mafuta na Gesi Asilia.

“TPDC itaendelea kufanya kazi kwa karibu na Wizara ya Nishati ili kuhakikisha miradi ya gesi asilia na mafuta inatekelezwa kwa ufanisi na kwa manufaa ya Watanzania wote."  Amesema Makame

Ziara ya Dkt. Mataragio TPDC ni muendelezo wa ziara zake katika Taasisi zinazosimamia Sekta ya Mafuta na Gesi Asilia ikiwa ni sehemu ya jitihada za Wizara ya Nishati kuimarisha usimamizi wa taasisi zake ili ziendelee kutekeleza majukumu kwa ufanisi lengo likiwa ni kuhakikisha wananchi wananufaika  na rasilimali zilizopo nchini.

 


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imedhamiria kujenga barabara zote zinazounganisha mkoa wa Katavi kwa lami ili kuufanya mkoa wa kimkakati na kibiashara.

Amesema hayo leo mkoani Katavi alipoweka jiwe la msingi ujenzi wa barabara ya Kagwira-Ikola- Karema yenye urefu wa km 112.

Dkt. Nchema amesema barabara hiyo inaunganisha mji wa Mpanda na ziwa Tanganyika kwenye bandari ya Karema itachochea huduma za bandari na shughuli za kiuchumi itakapokamilika.

" Tumedhamiria kuunganisha barabara zenu za Rukwa- Mpanda na Mpanda -Kigoma kwa lami ili kuifanya Katavi mkoa wa kimkakati na kiuchumi", amesisitiza Dkt. Nchemba.

Nae Naibu Waziri wa Ujenzi Eng. Godfrey Kasekenya amesema Serikali imeipandisha hadhi barabara ya Kagwira- Karema kutoka kuwa barabara ya mkoa kuwa barabara Kuu hivyo ujenzi wake utakuwa wa viwango vya juu ili kuwezesha magari makubwa kupeleka na kuchukua mizigo katika bandari ya Karema ambayo ujenzi wake umekamilika.

" Katika kuhakikisha ujenzi wa barabara hii unakamilika kwa wakati na ubora tumeugawa sehemu mbili ambazo ni Kagwira-Kasekese km 54.1 na Kasekese- Karema km 56", amesema Eng. Kasekenya.

Barabara hiyo yenye madaraja makubwa 7 na madogo 88 inatarajiwa kugharimu shilingi bilioni 219 itakapokamilika.

Naibu Waziri Kasekenya amesema Serikali inaendelea kuzijenga kwa kiwango cha lami barabara za Kibaoni-Sitalike km 72 na Vikonge- Mishamo hadi Uvinza km 156 ili kuunganisha mkoa wa Rukwa, Katavi na Kigoma kwa lami na hivyo kuufungua ushoroba wote wa mwambao wa ziwa Tanganyika na hivyo kuchochea uchumi wa mikoa hiyo.



Wakala wa Nishati Vijijini (REA), umeendelea kutekeleza miradi ya kupeleka huduma ya umeme katika maeneo ya vitongoji ili kuwawezesha wananchi waliopo maeneo hayo kupata huduma bora ya nishati ya umeme kwa ajili  ya Maendeleo yao na Taifa kwa ujumla. 

Hayo yamebainishwa na Msimamizi wa Miradi ya REA, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Mha. Danstan Kalugira wakati akizungumza  na Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) kuhusu miradi inayotekelezwa na REA katika wilaya ya Ludewa mkoani Njombe.

Mha. Kalugira amesema kuwa, kiasi cha fedha takribani shilingi bilioni 3.1 tayari zimetolewa na Serikali kupitia REA ili kutekeleza mradi huo wa kupeleka umeme kwenye vitongoji takribani 6 vya wilaya ya Ludewa ili wananchi wanufaike na huduma ya umeme.

"Katika mradi huu hapa wilayani Ludewa, mkandarasi kampuni ya SUMA JKT ndiye anayetekeleza mradi huu mkubwa ambao unatarajiwa kuunganishia wateja wapatao 160 wa awali mara baada ya mradi kuwa umekamilika, " Amesema Mha. Kalugira

Ameongeza kuwa, japokuwa kipindi hichi ni cha masika mvua nyingi zinanyesha  ila mkandarasi huyo anaendelea kutekeleza mradi kwa kasi, weledi na ni matarajio kuwa atakwenda kumaliza mradi huo kwa wakati katika muda uliopangwa ili wananchi watakaounganishwa na nishati ya umeme waweze kunufaika.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri (TEF), Bw. Deodatus Balile ameishukuru Serikali kwa kutoa fedha ya utekelezaji wa miradi hiyo inayoendelea katika mkoa wa Njombe na maeneo mengine nchini.

"Tumejionea kwa macho yetu namna fedha hizi zinazotolewa na Serikali na  jinsi zinavyotekeleza miradi ya kupeleka huduma ya umeme katika wilaya hii ya Ludewa ili wananchi wapate nishati bora ya uhakika, " Amesisitiza Bw. Balile.

Ziara ya TEF imelenga kutembelea miradi ya kimkakati inayotekelezwa na REA katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo miradi ya Awamu ya Pili B (HEP 2B) ya kupeleka umeme kwenye vitongoji vipatavyo 9,009.

  



Na OWM – TAMISEMI, Ufaransa


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, amekutana na Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Mhe.Ali Mwadini, kujadili mikakati ya kuvutia na kutafuta wawekezaji katika eneo la Bonde  la Msimbazi lililopo jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao wamekubaliana kuwa na mpango madhubuti wa kutafuta wawekezaji wa kimataifa watakaoshiriki kuwekeza katika maendeleo ya bonde hilo, ambalo Serikali imeanza kulijenga ili kupunguza athari za mafuriko na wakati huo huo kufungua fursa mpya za uwekezaji na biashara.

Utekelezaji wa mpango huo unatarajiwa kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi, kuboresha huduma za kijamii pamoja na kuongeza fursa za ajira kwa wananchi wa jiji la Dar es Salaam na maeneo jirani, huku pia ukivutia wafanyabiashara na wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.

Prof. Shemdoe amefanya ziara katika ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa jana Machi 13, 2026, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha uwekezaji unaofanyika katika Bonde la Msimbazi unaleta manufaa makubwa kwa uchumi wa taifa na kuwawezesha wajasiriamali na wafanyabiashara wa jijini Dar es Salaam.

Uwekezaji unaotarajiwa katika bonde hilo ni sehemu ya mikakati ya Serikali ya kuendeleza miundombinu ya kisasa mijini, kudhibiti mafuriko na kuifanya Dar es Salaam kuwa kitovu muhimu cha biashara na uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki.


Wananchi na wakazi wa Hydom wilayani Mbulu mkoa wa Manyara wamemshukuru Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kufuatia Wizara ya Maji kupitia RUWASA kutekeleza mradi mkubwa wa Majisafi ya bomba wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 41 na tayari vijiji vinne vimeshaanza kunufaika na mradi huo.

Wametoa pongezi hizo wakati wa ziara ya kamati ya kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira alipotembelea na kukagua mradi huo ikiongozwa na Mwemyekiti wake Mhe. Jackson Kiswaga (Mb) katika eneo la Hydom lilipo tangi kubwa la ujazo wa lita 2,000,000 la mradi huo.

Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA Mha. Wolta Kirita aliieleza Kamati hiyo kuwa tayari wananchi zaidi 800 wameshasajiliwa na kupatiwa kadi za malipo kabla ya matumizi kwani mradi huo unaenda sambamba na ufungaji wa dira za maji za malipo ya kabla, ambapo mwananchi anaweza kuchota maji kwenye kituo muda wowote anapokuwa anahitaji huduma hiyo.

Mkurugenzi Mkuu Kirita alisema mradi huo unatarajiwa kukamilika Novemba 2027.

Kwa mujibu wa Meneja wa RUWASA mkoa wa Manyara Mha. James Kionaumela alisema mradi huo umeshaanza kutoa huduma katika vijiji vinne na ukikamilika utahudumia zaidi ya wakazi 100,000 wa eneo hilo.

Naye Mkuu wa wilaya ya Mbulu Mhe. Michael Semindu akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Sendiga alisema kwa sasa wananchi wa wilaya hiyo wanapata maji kwa saa 12 kwa siku huku akiipongeza RUWASA kwa kazi nzuri katika kutekeleza mradi huo.








Na. Joyce Ndunguru, Dodoma.

Kaimu Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Mlage Yussuf Kabange amefungua rasmi kikao kazi cha maandalizi ya bajeti ya TAWA kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao kazi kilichofanyika Machi 13,2026, Jijini Dodoma, Kamishna Kabange amesema Bajeti ya mwaka 2026/27 ni ya kipekee kwa kuzingatia kuwa ni bajeti ya kwanza katika kuchangia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2025 pamoja na Dira ya maendeleo ya Taifa 2050.

“Pia bajeti hii imezingatia kutafsiri Hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan wakati wa kuzindua Bunge la 13, Mkakati wa kuongeza mapato wa TAWA na ni bajeti ya kwanza tangu Bodi ya Nne ya Wakurugenzi ya TAWA iteuliwe”, amesema Kamishna Kabange.

Kamishna Kabange ameongeza kuwa katika bajeti hii TAWA itajielekeza katika vipaumbele mbalimbali ikiwemo kuimarisha ulinzi na usimamizi wa Rasilimali wanyamapori na malikale.

Pia, Kuimarisha shughuli za utalii pamoja na kuongeza idadi ya watalii kwa kuboresha miundombinu ya utalii pamoja na kuongeza vyanzo vipya vya mapato.

Kadhalika, Utatuzi wa migogoro ya mipaka na udhibiti wa wanyamapori wakali na waharibifu pamoja na Kuimarisha mazingira ya utendaji kazi kwa watumishi na uwezo wa Mamlaka katika kutoa huduma.

Vilevile , Kamishna Kabange amewapongeza Makamanda na Askari ambao wamekuwa mstari wa mbele kusimamia utekelezaji wa malengo ya Mamlaka. Aidha, amewaelekeza Makamanda wa vituo kuhakikisha Usimamizi madhubuti wa vitendea kazi yakiwemo magari.

Aidha, Kamishna Kabange amewaelekeza Makamanda kuendelea na utangazaji wa vivutio vya utalii pamoja na kubuni mazao mapya ya utalii.

“Nitoe rai kwenu kuendelea kuwa wabunifu na kutangaza maeneo mnayoyasimamia,” amesema Kamishna Kabange 

Sambamba na hilo, Kamishna Kabange amewaelekeza Makamanda kuendelea kusimamia askari kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kwa kuzingatia haki, sheria na miongozo iliyowekwa.

Kikao kazi cha maandalizi ya bajeti kimehudhuriwa na viongozi wa TAWA kwa ngazi ya Makao Makuu, Kanda na Vituo.

Mhandisi wa Maji na Usafi wa Mazingira wa EWURA Kanda ya Kati, Saidi Mwangalo,akiwasilisha mada kuhusu uvunaji na uhifadhi wa maji ya mvua kwa wadau mbalimbali mkoani Singida,wakati wa semina iliyotolewa leo Machi 13,2026 kwa wanachama wa Chama cha Watu Wenye Ulemavu, viongozi kutoka wilaya ya Singida pamoja na wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Watumiaji wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA CCC).

Na.Mwandishi Wetu-SINGIDA

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imetoa elimu ya uvunaji na uhifadhi wa maji ya mvua kwa wadau mbalimbali mkoani Singida, wakiwemo wanachama wa Chama cha Watu Wenye Ulemavu, viongozi kutoka wilaya ya Singida pamoja na wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Watumiaji wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA CCC), leo tarehe 13 Machi 2026.

Akiwasilisha mada kuhusu uvunaji wa maji ya mvua, Mhandisi wa Maji na Usafi wa Mazingira wa EWURA Kanda ya Kati, Saidi Mwangalo, alieleza mbinu mbalimbali za kuvuna na kuhifadhi maji ya mvua ili yaweze kutumika kwa muda mrefu na bila kuharibika.

Alisema uvunaji wa maji ya mvua ni njia muhimu ya kuongeza upatikanaji wa maji, hususan wakati wa ukame au pale kunapotokea changamoto katika huduma ya maji. Alisisitiza kuwa mvua ni rasilimali inayopatikana bure, hivyo ni muhimu kutunza na kutumia kila tone la maji ipasavyo ili kukabiliana na changamoto za upatikanaji wa maji.

Washiriki pia walipatiwa elimu na Ofisa Huduma kwa Wateja, Bw. Juma Singano, kuhusu utaratibu wa kushughulikia malalamiko na kutatua migogoro kati ya watoa huduma na wateja wa sekta zinazodhibitiwa na EWURA

Mada nyingine zilizowasilishwa ni pamoja na utaratibu wa utoaji vibali vya ujenzi wa vituo vya mafuta mijini na vijijini, iliyowasilishwa na Mhandisi wa Petroli Kanda ya Kati, Bi. Roselyne Mndeme, pamoja na matumizi sahihi na salama ya gesi ya kupikia majumbani, iliyowasilishwa na Ofisa Uhusiano Mwandamizi wa EWURA, Bi. Tobietha Makafu.

Akitoa neno la shukrani baada ya semina hiyo, Mkurugenzi wa Chama cha PPD, Bw. Ramadhan Mrisho aliishukuru EWURA kwa kuwafikia wanachama wao kwa elimu hiyo muhimu.

Pia aliishauri EWURA kuendelea kutoa elimu kwa jamii, hususan katika maeneo yenye changamoto ya upatikanaji wa maji, ili wananchi waweze kutumia misimu ya mvua kuvuna na kuhifadhi maji kwa matumizi ya baadaye.

Mhandisi wa Maji na Usafi wa Mazingira wa EWURA Kanda ya Kati, Saidi Mwangalo,akiwasilisha mada kuhusu uvunaji na uhifadhi wa maji ya mvua kwa wadau mbalimbali mkoani Singida,wakati wa semina iliyotolewa leo Machi 13,2026 kwa wanachama wa Chama cha Watu Wenye Ulemavu, viongozi kutoka wilaya ya Singida pamoja na wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Watumiaji wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA CCC).

 Ofisa Huduma kwa Wateja, Bw. Juma Singano, akitoa mada kuhusu utaratibu wa kushughulikia malalamiko na kutatua migogoro kati ya watoa huduma na wateja wa sekta zinazodhibitiwa na EWURA wakati wa semina iliyotolewa leo Machi 13,2026 kwa wanachama wa Chama cha Watu Wenye Ulemavu, viongozi kutoka wilaya ya Singida pamoja na wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Watumiaji wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA CCC).

 

Mhandisi wa Petroli Kanda ya Kati, Bi. Roselyne Mndeme,akitoa mada wakati wa semina iliyotolewa na EWURA leo Machi 13,2026 kwa wanachama wa Chama cha Watu Wenye Ulemavu, viongozi kutoka wilaya ya Singida pamoja na wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Watumiaji wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA CCC) iliyofanyika Mkoani Singida.

Ofisa Uhusiano Mwandamizi EWURA, Bi. Tobietha Makafu,akitoa mada  wakati wa semina iliyotolewa na EWURA leo Machi 13,2026 kwa wanachama wa Chama cha Watu Wenye Ulemavu, viongozi kutoka wilaya ya Singida pamoja na wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Watumiaji wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA CCC) iliyofanyika Mkoani Singida.

Mkurugenzi wa Chama cha Walemavu (PPD), Bw. Ramadhan Mrisho,akitoa neno la shukrani baada ya kupatiwa elimu na EWURA  kuhusu uvunaji na uhifadhi wa maji ya mvua kwa wadau mbalimbali mkoani Singida, iliyotolewa leo Machi 13,2026 kwa wanachama wa Chama cha Watu Wenye Ulemavu, viongozi kutoka wilaya ya Singida pamoja na wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Watumiaji wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA CCC).

Sehemu ya washiriki wakifuatilia mada mbalimbali wakati wa semina iliyotolewa na EWURA  kuhusu uvunaji na uhifadhi wa maji ya mvua kwa wadau mbalimbali mkoani Singida.

Sehemu ya washiriki wakifuatilia mada mbalimbali wakati wa semina iliyotolewa na EWURA  kuhusu uvunaji na uhifadhi wa maji ya mvua kwa wadau mbalimbali mkoani Singida.

Sehemu ya washiriki wakifuatilia mada mbalimbali wakati wa semina iliyotolewa na EWURA  kuhusu uvunaji na uhifadhi wa maji ya mvua kwa wadau mbalimbali mkoani Singida.

Sehemu ya washiriki wakifuatilia mada mbalimbali wakati wa semina iliyotolewa na EWURA  kuhusu uvunaji na uhifadhi wa maji ya mvua kwa wadau mbalimbali mkoani Singida.

Benki ya Absa Tanzania, kwa ushirikiano na Microsoft na Women in Tech, imezindua rasmi Mpango wa ElevateHer AI nchini Tanzania, ambao unalenga kuwawezesha wasichana 5,000 wa Kitanzania kupata ujuzi na cheti cha Akili Mnemba (AI).

Mpango huu ni sehemu ya juhudi pana za kiafrika zinazolenga kutoa mafunzo kwa wanawake 50,000 barani Afrika ili waweze kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali unaokua kwa kasi.

Kupitia mpango wa ElevateHer, washiriki watapata fursa ya kujifunza mtandaoni kwa njia ya kujitegemea bila malipo, ambapo watapata maarifa ya msingi ya AI, matumizi ya AI katika biashara, na maendeleo ya taaluma katika mazingira ya kazi yanayoendeshwa na teknolojia ya AI. Mpango huu utakuwa wazi kwa mwaka mzima.

Ofisa Mkuu wa Uendeshaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Oscar Mwamfwagasi, amesema mpango huu unaakisi dhamira ya benki kuhakikisha wasichana wanapata ujuzi wa kidijitali unaohitajika kwa siku za usoni. “Artificial intelligence inabadilisha jinsi uchumi unavyofanya kazi na jinsi watu wanavyofanya kazi. 

Kupitia Mpango wa ElevateHer AI, Benki ya Absa Tanzania inalenga kuhakikisha wasichana wa Kitanzania wanapata ujuzi na kujiamini kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali na kuchangia ubunifu na ukuaji.”

Juhudi hii inaendeleza michango ya Absa Tanzania ya kukuza ushiriki wa wanawake katika teknolojia, ikiwa ni pamoja na GirlCode Hackathon ya mwaka jana, ambapo wasichana wabunifu walikusanyika ili kutengeneza suluhisho za kiteknolojia.

Mpango wa ElevateHer unatoa njia tatu za kujifunza: AI kwa Wote, AI kwa Biashara, na AI kwa Ukuaji wa Kitaaluma, na kutoa fursa kwa washiriki kujenga maarifa ya vitendo na kutumia zana za AI katika safari zao za kitaaluma au za ujasiriamali.

Bi. Tiara Pathon, Mkurugenzi wa Ujuzi wa AI katika Microsoft Elevate, Microsoft Afrika Kusini, amesema upatikanaji wa ujuzi wa kidijitali kwa kila mmoja ni muhimu kwa ushiriki wa Afrika katika uchumi wa AI duniani. “Ukuaji wa uchumi jumuishi katika zama za AI unahitaji kujenga ujuzi kwa wingi katika masoko yanayokua. Kwa Afrika, hii inamaanisha kuwekeza kwa makusudi katika ujuzi wa kidijitali na AI kwa wanawake. Kupitia ushirikiano wetu na Absa na Women in Tech, mpango wa ElevateHer unawawezesha wanawake barani kote kupata ujuzi wa vitendo unaohitajika kazini na kuimarisha nafasi ya Afrika katika ajira za baadaye.”

Mpango huu pia unasaidiwa na Women in Tech Global, shirika linalojitolea kuwawezesha wanawake na wasichana milioni tano katika Sayansi, Teknolojia, Uhandisi, na Hisabati (STEM) kufikia mwaka 2030.

Wanawake wanaopenda kushiriki wanaweza kujisajili mtandaoni kupitia: https://elevateher-in-africa.org/⁠ 

Kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), napenda kuungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na jumuiya ya kimataifa katika kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Figo. Siku hii ni muhimu katika kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa kulinda na kutunza afya ya figo.

Takwimu za kimataifa zinaonesha kuwa zaidi ya watu milioni 850 duniani wanaishi na aina fulani ya ugonjwa wa figo, huku takribani asilimia 10 ya watu wazima duniani wakiwa na dalili za ugonjwa huo. Aidha, mamilioni ya watu hulazimika kutegemea matibabu ya gharama kubwa kama dialysis au upandikizaji wa figo (kidney transplant) ili kuendelea kuishi.

Barani Afrika, tafiti zinaonesha kuwa kati ya asilimia 13 hadi 15 ya watu wazima wanaweza kuwa na dalili za ugonjwa wa figo. Nchini Tanzania, tafiti mbalimbali zinaonesha kuwa takribani asilimia 10 hadi 12 ya watu wazima wanaweza kuwa katika hatari au tayari wana dalili za ugonjwa wa figo, huku wengi wakigundulika katika hatua za mwisho za ugonjwa.

Gharama za matibabu ya magonjwa ya figo ni kubwa sana. Mgonjwa anayehitaji dialysis hulazimika kufanya matibabu hayo mara mbili hadi tatu kwa wiki, ambapo gharama ya kikao kimoja inaweza kufikia wastani wa dola za Marekani 80 hadi 200. Hii ina maana kuwa kwa mwaka mmoja, gharama za matibabu zinaweza kufikia dola 10,000 hadi 25,000 au zaidi kwa mgonjwa mmoja.

Aidha, matibabu ya upandikizaji wa figo (kidney transplant) yanaweza kugharimu kati ya dola 15,000 hadi 30,000, bila kujumuisha gharama za dawa za kudhibiti kinga ya mwili ambazo mgonjwa hulazimika kutumia maisha yote.

Kutokana na hali hii, ni wazi kuwa kinga ni bora zaidi kuliko tiba, na jamii inapaswa kuhamasishwa kuchukua hatua za kulinda afya ya figo mapema.

Katika muktadha huu, tiba asilia ina nafasi muhimu katika kusaidia kuimarisha kinga ya mwili na afya kwa ujumla. Hata hivyo, bado kuna changamoto ya uhaba wa ushahidi wa kisayansi unaothibitisha kwa kina baadhi ya dawa na mbinu za tiba asilia. Kwa sababu hiyo, TRAMEPRO inaendelea kusisitiza umuhimu wa tafiti za kisayansi, uthibitishaji wa dawa za asili, na ushirikiano kati ya wataalamu wa afya na taasisi za utafiti.

Kwa sasa, nikiwa katika ziara ya kitaaluma mjini New Delhi, India, ninapata uzoefu na kujifunza kuhusu matibabu mtambuka (Integrative Medicine) katika taasisi mbalimbali ikiwemo Max Super Speciality Hospital pamoja na taasisi za tiba asilia chini ya mfumo wa AYUSH. Uzoefu huu unalenga kuimarisha uelewa na ushirikiano katika kuunganisha tiba asilia na tiba za kisasa kwa manufaa ya afya ya jamii.

TRAMEPRO itaendelea kushirikiana na taasisi za utafiti, hospitali, na wataalamu wa magonjwa ya figo ili kuendeleza tafiti, kutoa elimu kwa jamii, na kuhakikisha matumizi salama na yenye tija ya tiba asilia.

Katika maadhimisho haya, ninatoa wito kwa:

Watabibu wa tiba asilia kuzingatia viwango vya usalama, maadili ya kitaaluma na uthibitisho wa kisayansi katika huduma wanazotoa.

Wananchi kuchukua hatua za kinga dhidi ya magonjwa ya figo ikiwa ni pamoja na kudhibiti shinikizo la damu na kisukari, kunywa maji ya kutosha, kutumia dawa kwa usahihi, na kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara.

Serikali na taasisi za utafiti kuendelea kuwekeza katika tafiti za dawa za asili na kuimarisha mfumo wa huduma za afya jumuishi.

Kwa pamoja tunaweza kujenga mfumo wa afya unaounganisha hekima ya tiba asilia na sayansi ya tiba ya kisasa kwa manufaa ya binadamu na mazingira yetu.

Mungu aibariki Tanzania na awajalie wananchi wake afya njema.

Boniventura Mwalongo Katibu Mkuu – TRAMEPRONew Delhi, India 12 Machi 2026

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Mambo ya Ndani ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Shaibu Mmari, amesema ushirikiano kati ya TRA na mawakala wa forodha ni nguzo muhimu katika kuimarisha usimamizi wa maadili na uwajibikaji kwa watumishi wa Mamlaka.

Bw. Mmari amesema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa kikao cha mazungumzo kati ya TRA na viongozi wa Chama cha Waondoshaji na Wapelekaji Shehena Bandarini na Mipakani Tanzania (TAFFA), kilicholenga kuimarisha mahusiano ya kikazi na kubadilishana taarifa kuhusu uvunjifu wa maadili unaoweza kujitokeza katika shughuli za forodha.

Amesema kuwa ushirikiano wa karibu kati ya TRA na wadau wa sekta ya forodha ni muhimu katika kusaidia kubaini na kudhibiti vitendo vinavyokiuka maadili, pamoja na kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika utoaji wa huduma.

“TRA ina jukumu la kukusanya mapato ya Serikali, kusimamia shughuli za forodha, na kuhakikisha sheria na taratibu za ushuru zinafuatwa ipasavyo. Ushirikiano na wadau kama TAFFA unatusaidia kuimarisha uadilifu na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu haya,” amesema Bw. Mmari.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa wadau kuendelea kushirikiana na TRA katika kutoa taarifa pale wanapoona dalili za uvunjifu wa maadili au vitendo vinavyoweza kuathiri uadilifu wa huduma za forodha.

Kwa upande wake, Mhasibu Mkuu wa TAFFA, Bw. Anthony Mukyamuzi, ameipongeza TRA kwa juhudi inazoendelea kufanya katika kuboresha mifumo ya forodha na utoaji wa huduma kwa wadau.

Amesema maboresho hayo yameongeza ufanisi katika shughuli za uondoshaji na uingizaji wa mizigo bandarini na mipakani, na kuimarisha mazingira ya biashara kwa wadau wa sekta ya usafirishaji na uondoshaji shehena.

Mwisho, pande hizo mbili zimeahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano katika kubadilishana taarifa, kuhamasisha maadili mema kwa watumishi, na kujenga mfumo wa uwajibikaji utakaosaidia kulinda uadilifu wa shughuli za forodha nchini.