Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe Prof. Hawa Tundui (kushoto) akikabidhi zawadi ya kumbukumbu kwa Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Exaud Kigahe (Mb.) kwenye Siku ya Mzumbe na Kambi ya Ujasiriamali

 


Rais mpya wa Baraza la 14 la Usimamizi wa Mkataba wa Lusaka (LATF), Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana, ametoa wito kwa nchi wanachama wa Mkataba huo kushirikiana katika uwekezaji wa teknolojia, uvumbuzi, na mifumo ya kisasa ya utawala ili kuimarisha maendeleo katika sekta mbalimbali za uhifadhi wa maliasili.

Akizungumza wakati wa kukabidhiwa rasmi nafasi ya urais wa Baraza hilo katika Mkutano wa 14 wa LATF unaofanyika leo Mei 8, 2025, jijini Arusha, Mhe. Chana ambaye ni Waziri wa Maliasili na Utalii, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kikanda katika kulinda na kuhifadhi bioanuai ya mimea na wanyama.


“Kwa niaba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nawakaribisha jijini Arusha – Mji wa kidiplomasia wa Afrika Mashariki, mahali ambapo amani, umoja na maendeleo hukutana. Mkutano huu si wa kikanuni tu, bali ni ishara ya mshikamano wetu wa Afrika katika kukabiliana na vitisho vya kimataifa kwa mazingira yetu, uchumi na uhuru wa mataifa yetu,” amesema Mhe. Chana.


Amebainisha kuwa Mkataba wa Lusaka umeendelea kuwa alama ya mshikamano na juhudi za pamoja za kupambana na uhalifu dhidi ya wanyamapori. Aidha, alisema mkataba huo si chombo tu cha kisheria, bali ni jukwaa linalowezesha ushirikiano wa kikanda, kubadilishana taarifa, uzoefu, na kutafuta suluhisho za pamoja za changamoto zinazowakabili wanachama.

Akizungumzia mafanikio ya Tanzania, Mhe. Chana ameeleza kuwa katika muongo uliopita, taifa limepiga hatua kubwa katika kupambana na uhalifu wa wanyamapori na kuimarisha juhudi za uhifadhi. Alitaja miongoni mwa hatua zilizochukuliwa kuwa ni pamoja na maboresho ya sheria, ikiwemo marekebisho ya Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori.

Pia, amesema kuanzishwa kwa Huduma ya Uhifadhi wa Wanyamapori na Misitu (WFCS); Ushirikiano wa kimataifa na kikanda ulioboreshwa;Uhamasishaji wa jamii kuhusu umuhimu wa uhifadhi;
Uvumbuzi wa kiteknolojia kwa ajili ya ufuatiliaji na udhibiti wa uhalifu wa wanyamapori;Hatua kali dhidi ya mitandao ya usafirishaji haramu wa wanyama.

“Juhudi hizi zimeungwa mkono na kutambuliwa na jamii ya kimataifa, na sasa ni wakati mwafaka kwa nchi wanachama wa LATF kuanza kutekeleza Mpango Mkakati wa LATF 2025–2030, ambao ni nyenzo muhimu katika kufikia malengo yetu ya pamoja,” ameongeza.

Kadhalika, Mhe. Chana amehitimisha hotuba yake kwa kutoa pongezi za dhati kwa Mhe. Rebecca Miano, Waziri wa Utalii na Wanyamapori wa Jamhuri ya Kenya, kwa uongozi wake bora katika kipindi cha miaka miwili iliyopita akiwa Rais wa Baraza hilo.

 


Waziri Masauni, Kamisheni ya Umoja wa Ulaya wakutana kujadili Mazingira
Mwandishi Wetu
Denmark
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni amefanya mkutano wa kimkakati wa uwili (Bilateral Meeting) kati ya Tanzania na Viongozi wa Kamisheni ya Umoja wa Ulaya (Europian Union).

Katika Mkutano huo uliofanyika Mei 8, 2025 jijini Copenhagen, Denmark Waziri Masauni ameelezea mkakati wa Tanzania katika utekelezaji wa programu za Mabadiliko ya Tabianchini. 

Mkutano huo umehudhiriwa na viongozi wakuu wa Kamisheni ya Umoja wa Ulaya akiwepo Bw. Wopke HOEKSTRA Kamishna wa Mazingira wa Ulaya, Bw. Krzysztof Bolesta, ambaye ni Katibu wa Nchi Wizara ya Hali ya Hewa na Mazingira- Poland akimwakilisha Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Ulaya pamoja na Bw. Christian Stenberg, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Hali ya Hewa/ Mazingira, Nishati na Fedha.

Katika Mkutano huo Mhe. Masauni aliambatana na Mshauri wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu masuala ya Mazingira na mabadiliko ya Tabianchi Dkt. Richard Muyungi, Mwakilishi kutoka Ubalozi wa Tanzania nchini Sweden pamoja na wataalam kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais.

Pamoja na masuala ya kubadilishana mawazo kuhusu vipaumbele kabla ya vikao vya Bonn na COP30, na Mwelekeo wa Nchi za kiafrika ambapo Tanzania ni mwenyekiti wa Kundi la Majadiliano la Afrika (AGN). 

Waziri Masauni alieleza kuhusu vipaumbele vitatu vya Tanzania ambavyo ni kuendelea kukabiliana na mabadiliko ya Tabianchi kwa kutumia njia mbalimbali vikiwamo vitu vya asili; kuendelea kuweka mazingira rafiki kwa watanzania kutumia nishati safi ya kupikia hadi kufikia kiwango cha asilimia 80 ifikapo mwaka 2034na kuendelea kuzijengea uwezo Taasisi zinazoratibu masuala ya biashara ya kaboni nchini.

Mhe. Masauni amesisitiza kuwa ni muhimu kwa Umoja huo wa Ulaya kuangalia namna bora ya kuiwezesha katika masuala ya kujengea uwezo, misaada ya kifedha yenye masharti nafuu, ruzuku na Teknolojia ya upimaji wa kiwango cha kaboni.

Akizungumza kwa niaba ya Rais wa Sasa wa EU, Bw. Krzysztof Bolesta, ameipongeza Tanzania kwa namna ilivyochukua hatua za kuanzisha Kituo cha Kaboni ambacho ni cha  mfano kwa nchi za Afrika. 

Aidha, alieleza kuwa siku zote Umoja wa Ulaya umekuwa ukifanya kazi na kuongoza kwa mfano mzuri na kwa kudumisha uwazi na haki na hivyo itaendelea kuhakikisha inatenda haki ya kutimiza ahadi zake zote za ufadhili wa programu za kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchini. 




 





Na MWANDISHI WETU,
 
TANGA. Waajiri wa sekta binafsi wametakiwa kuzingatia wajibu wao wa kuwasilisha michango ya wafanyakazi kwa wakati ili kuwawezesha wanachama wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kupata mafao yao kwa mujibu wa sheria.
 
Wito huo umetolewa tarehe 8 Mei 2025 jijini Tanga na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya NSSF, Bi. Mwamini Malemi, wakati akizindua rasmi Mkutano wa 54 wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mfuko huo.

Bi. Malemi amesema michango ya waajiri ni uti wa mgongo wa uendeshaji wa Mfuko, hivyo kucheleweshwa kwake kunaathiri moja kwa moja ustawi wa wanachama na ufanisi wa utoaji huduma za mafao.

“Naomba nitumie nafasi hii kuwaasa waajiri wote kuhakikisha wanawasilisha michango ya wafanyakazi wao kwa wakati. Hili si jambo la hiari bali ni wajibu wa kisheria unaolenga kulinda haki za wafanyakazi”, amesisitiza Bi. Malemi.

Ameongeza kuwa, NSSF inaendelea kutoa huduma bora na endelevu kwa wanachama wake kwa kuzingatia misingi ya uadilifu, uwajibikaji na matumizi ya teknolojia ili kuongeza uwazi na ufanisi katika shughuli za kila siku.

Akizungumza kuhusu mafanikio ya Mfuko, Bi. Malemi amesema NSSF imeendelea kuwa taasisi ya mfano katika sekta ya hifadhi ya jamii kwa kuimarisha mifumo ya TEHAMA, kuongeza kasi ya uandikishaji wanachama, kudhibiti mianya ya upotevu wa mapato na kufanya uwekezaji wenye tija.
“Lengo letu ni kuhakikisha kila mwanachama anaendelea kupata huduma bora, ya kisasa na inayokidhi matarajio. Tunataka NSSF iwe taasisi ya mfano katika uwajibikaji”, amesema Bi. Malemi.

Aidha, Bi. Malemi amewapongeza wajumbe wapya wa Bodi ya Wadhamini na kuwataka kuhakikisha Mfuko unasimamiwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo iliyowekwa, huku akiwataka wajumbe wa Baraza hilo kuwa chachu ya mabadiliko chanya katika maeneo yao ya kazi.
Kwa upande wake, Bw. Masha Mshomba, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, amesema Mfuko unatarajia kupata mafanikio makubwa zaidi kwa kuwa umewekewa vipaumbele vinavyolenga kupanua wigo wa wanachama, kuongeza mapato, kuboresha ulipaji wa mafao na kuimarisha huduma kwa wanachama kupitia mifumo ya TEHAMA.
Awali, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Rasilimali Watu na Utawala, Bw. Ekwabi Mujungu aliwataka wajumbe wa Baraza hilo kuzingatia kwa makini maazimio watakayoyapitisha ili kufanikisha utekelezaji wa majukumu ya Mfuko.
Bi. Flora Ndutta, akitoa neno la shukrani amesema NSSF itaendelea kutoa huduma bora kwa kutumia TEHAMA, kuwafikia wananchi waliojiajiri na kwamba wataendelea kufanya kazi kwa bidii, kwa weledi na kwa kuzingatia maadili.


MWISHO

 


Kampuni ya Mamba Minerals Ltd yenye Leseni ya uchimbaji Madini adimu (Rare Earth Elements) imesema itaanza ujenzi rasmi wa Mgodi huo Disemba,2025 na uzalishaji wa kwanza kufanyika mwisho wa mwaka 2026.

Hayo yameelezwa leo Jijini Dodoma wakati wa kikao kati ya Waziri wa Madini Mh. Anthony Mavunde na Viongozi wa Kampuni za Mamba Minerals na Shenghe Ltd.

Akizungumza wakati wa kikao hicho Mwenyekiti wa Kampuni ya Mamba Minerals Ndg.Russell Scrimshaw amesema Kampuni hiyo imeitikia wito wa serikali wa kuhakikisha uzalishaji wa madini unaanza mapema iwezekanavyo kamba ambavyo Waziri wa Madini amesisitiza na hivyo kwa kushirikiana na wabia wenza Kampuni ya Shenghe watahakikisha ujenzi wa mgodi unaanza mapema mwezi Disemba 2025 na uzalishaji wa kwanza kufanyika mwishoni mwa mwaka 2026. 

Naye Mwenyekiti wa Kampuni ya Shenghe Ndg. Quangan Wang amesema Ujenzi wa mgodi huo pia utaenda sambamba na ujenzi wa Kiwanda cha kuchenjua na kusafisha madini hayo pamoja na ujenzi wa Mtambo wa kuzalisha umeme wa kuanzia megawati 10-12 kwa matumizi ya mgodi na jamii inayozunguka mradi.

Madini adimu haya hutumika kwenye kutengeneza vifaa vya kieletroniki,vifaa vya uzalishaji umeme kutumia upepo,Mota za magari ya umeme na Vifaa vya hospitali.

Waziri wa Madini Mh. Anthony Mavunde amepongeza hatua ya Kampuni hiyo kuzingatia maelekezo ya serikali ya kuanza uendelezaji wa mgodi wa madini adimu kwa uharaka na kuendelea kusisitiza kwamba wamiliki wote wa Leseni za kati na Leseni kubwa kuhakikisha wanaanza shughuli za uchimbaji wa madini ndani ya miezi 18 ambayo imetamkwa kwenye Sheria ya Madini Sura ya 123.





 


📌 Asema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa elimu

📌 Asema Afrika lazima iendelee kuimarisha mazingira wezeshi kwa kampuni bunifu za kidigitali

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amewahimiza wadau wa elimu barani Afrika kuendeleza mkakati na ushirikiano utakaowezesha mageuzi ya kidigitali  katika sekta ya elimu.

Dkt. Biteko ametoa rai hiyo Mei 8, 2025 jijini Dar es salaam wakati alipomwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan katika ufunguzi wa Kongamano la 18 la eLearning Afrika.

“ Tanzania inaendeleza dhamira yake ya mageuzi ya kidigitali katika elimu na tungependa kushirikiana na Serikali, wadau wa maendeleo, sekta binafsi na wanazuoni  ili kufanya e- learning kuwezeshwa kwa ghrama nafuu kwa wote ,” amesema Dkt. Biteko.

Ameongeza kuwa Tanzania imedhamiria kuongoza katika mageuzi ya kidigitali barani Afrika ambapo Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050 inatambua kuwa mageuzi ya kidijitali ni kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi, maendeleo ya kijamii na ushindani wa kimataifa. Ili kufanikisha hili, Tanzania imeandaa mifumo kadhaa ikwemo Sera ya Taifa ya TEHAMA na Mkakati wa Uchumi wa Kidijitali Tanzania 2024-2034.

Dkt. Biteko amesema kuwa Mkakati wa Taifa wa Elimu ya Kidijitali na Programu ya Tanzania ya Kidijitali zinalenga kuimarisha miundombinu na huduma za kidijitali, kuhakikisha teknolojia muhimu, vifaa, muunganiko na rasilimali za e-learning vinafika maeneo mbalimbali nchini, aidha nchi zingine pia zitumie rasilimali zao katika kusaidia mageuzi ya kidijitali katika nchi zao.

Amewahimiza wadau wa kongamano hilo kuwa ili mageuzi ya kidijitali ya Afrika yaweze kufanikiwa, lazima kuwezeshwa kwa nguvu kazi yenye ujuzi kuanzia umri mdogo. Tanzania imefanya marekebisho ya Sera ya Taifa ya Elimu na Mafunzo mwaka 2023 na kuwa ni mfano muhimu, ikisisitiza uendelezaji wa ujuzi kuanza elimu ya msingi. 

“Sera hii pia inakuza matumizi ya teknolojia za kidijitali ili kukabiliana na upungufu wa walimu, kupanua upatikanaji wa elimu, na kuboresha ubora wa kujifunza. Mbinu hii inawaandaa wanafunzi kwa ajili ya baadaye na kuwawezesha waelimishaji kwa kuwapa zana bora za kufundishia katika nyakati za  kidijitali,” amesema Dkt. Biteko.

Pamoja na hayo amesema kuwa Afrika lazima iendelee kuboresha mazingira kwa kampuni za kibunifu ya ndani kwa kuunda sera saidizi zinazokuza ubunifu na ujasiriamali ili kusaidia kukuza masoko ya ndani  kwa teknolojia zinazoweza kuhamishwa na  kuwezesha mataifa ya Afrika kuongeza ufanisi wa rasilimali, kupunguza ucheleweshaji na kuharakisha mageuzi ya kidijitali.

Pia amebainisha kuwa ni muhimu kwa Bara la Afrika kuwabakisha wataalamu wenye ujuzi ndani ya Afrika na kushirikisha diaspora ili kuchangia ukuaji wa bara hilo. Kwa kuifanya Afrika kuwa kitovu cha maendeleo ya kiteknolojia.

Kwa upande wake, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda amesema Tanzania imeendelea kuwekeza katika matumizi ya teknolojia katika sekta ya elimu kwa kuhamasisha matumizi ya akili mnemba katika shule.

Ameongeza kuwa kupitia Kongamano hilo lilianza Mei 7, 2025 litatoa fursa ya kuimarisha na kukuza uhusiano na ushirikiano katika nchi za Afrika sambamba na kuboresha sera na mifumo yake ya elimu ili kuendana na teknolojia, ubunifu na hususan matumizi ya akili mnemba.

Akieleza kuhusu eLearning Afrika, Mwanzilishi mwenza wa FIRCAD- Ghana, Dkt. Aida Opoku- Mensah amesema kuwa akili mnemba ina manufaa makubwa kwa maendeleo ya ikiwa ni pamoja na kutumika kutatua changamoto na kufanya shughuli kama binadamu.

Amesema akili mnemba imekuwa na umuhimu mkubwa katika maisha ya kila siku ya mwanadamu kwa kusaidia pia katika ufanyaji tafiti mbalimbali.

Amezungumzia utayari wa Afrika katika matumizi hayo na kusema kuwa baadhi ya nchi za Afrika zimekuwa na mwitikio wa haraka wa matumizi ya akili mnemba kuliko nyingine kutoka na uwekezaji wake.

Ametolea mfano Kenya (m-shule) na Nigeria tayari inatumia mifumo ya akili mnemba kwenye mifumo yake ya elimu na Tanzania kupitia ubongo kipindi kinachoelimisha na kuburudisha.

Amebainisha matumizi makubwa ya akili mnemba nchini China yamesaidia kukuza uchumi wake, aidha Afrika inatakiwa kuwekeza katika akili mnemba ili kusaidia katika sekta mbalimbali  za elimu na miundombinu.

Kongamano na maonesho ya kila mwaka la eLearning Afrika , ambalo lilianzishwa mwaka 2005, ni tukio kubwa linalotoa fursa ya kubadilishana maarifa kwa elimu ya kidijitali, mafunzo na ujuzi katika Bara la Afrika.











Mkuu wa Wilaya ya Longido, Mheshimiwa Salum Kalli, ameitembelea Shule ya Sekondari ya Wasichana Lekule mnamo Mei 7, 2025, ambapo alipata fursa ya kujionea maendeleo ya shule hiyo pamoja na kuzungumza na wanafunzi.

Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Kalli aliwahimiza wanafunzi hao kusoma kwa bidii na kuwa na nidhamu wawapo shuleni, akisisitiza kuwa elimu ndiyo njia pekee ya kufikia mafanikio ya maisha. Aliwataka kuepuka kabisa vitendo vya mimba za utotoni ambavyo vinaweza kuwa kikwazo kikubwa katika safari yao ya kielimu na kuwakatisha ndoto zao za baadae.

Aidha, kama sehemu ya kuwatia moyo, Mkuu huyo wa Wilaya aliwazawadia wanafunzi hao nyama ya ng’ombe kwa ajili ya chakula, jambo lililopokelewa kwa shangwe na furaha kubwa.

Akizungumza kwa niaba ya shule hiyo, Mkuu wa Shule Mwalimu Anna Wenseslausi alimshukuru sana Mkuu huyo wa Wilaya kwa ujio wake na zawadi aliyoitoa.













 


Na WAF, DODOMA 

Serikali imesema huduma za afya ya akili zimeshajumuishwa kwenye vifurushi vya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), na hivyo wananchi wanaonufaika na bima wanaweza kupata matibabu hayo kwa mujibu wa mwongozo wa matibabu uliopo.

Akijibu swali la Mbunge wa Iringa Mjini, Mhe. Jesca Msambatavangu, Naibu Waziri wa Afya Dkt. Godwin Mollel amesema kuwa, huduma za afya ya akili, ushauri nasaha, pamoja na huduma za kibingwa kama vile utengamao, zote zimetajwa kama huduma muhimu kwenye Mwongozo wa Matibabu (Standard Treatment Guideline – STG) na zinagharamiwa na NHIF

“Huduma hizi zinalipiwa kwa kuzingatia aina ya dawa na ngazi ya kituo cha huduma, kwa mujibu wa mwongozo wa matibabu wa Taifa,” amefafanua Naibu Waziri  Dkt. Mollel.

Serikali imeendelea kuhakikisha kuwa huduma za afya ya akili zinapewa uzito sawa na huduma nyingine za msingi, na kuimarisha upatikanaji wake kupitia mifumo ya bima ya afya kwa wote.

Na John Mapepele

Mwenyekiti wa UWT Taifa, Mhe. Mary Pius Chatanda ameshuhudia utiaji saini wa mikataba mitano ya bilioni 13.3 zilizotolewa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ili kuboresha miundombinu ya barabara na madaraja wilayani Rufiji, huku Mhe. Mchengerwa akizindua rasmi Ligi ya ”Mchengerwa Mtu Kazi” inayoanza leo Mei 8, 2025 na kutoa vifaa (jezi na mipira) kwa timu zote 169 kutoka kwenye kata 13 zinazoshiriki mashindano hayo vyenye gharama ya milioni 67 pamoja na fedha taslimu milioni 25 ikiwa ni zawadi za washindi.

Tukio hili la utiaji saini limefanyika Mei 7, 2025 mara baada ya kukamilika kwa ziara ya siku mbili ya Mhe. Chatanda kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika jimbo hilo, katika eneo la uwanja wa stendi wa Ikwiriri  na kushuhudiwa  na maelfu ya wananchi wa wilaya  hiyo huku wasanii kadhaa wakitumbuiza kwa burudani za muziki.

Akitoa taarifa ya miradi hiyo, Meneja wa Wakala za Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) mkoa wa Pwani, Leopold Runji amefafanua kuwa gharama hizo zinahusisha ukarabati wa barabara ya Nyamwage yenye Kilomita 28, ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami ya Chumbi- Kiegele yenye kilomita 1.4, ukarabati wa barabara ya Mohoro- Mtanga kilomita 12.3 na Mohoro Ndundutawa yenye kilomita 7.5.

Pia ukarabati wa barabara ya Nyamwage- Mpakani- Nambunju na ujenzi wa  barabara za lami katikati ya mji wa Ikwiriri ambapo amesema kukamilika kwa miradi hiyo kutasaidia  kuiunganisha  wilaya  hiyo na maeneo mbalimbali ya mikoa ya Tanzania.

Mhe. Chatanda amemshukuru Rais Samia kwa kutoa fedha za miradi na kufafanua kwamba  kwa kufanya hivyo siyo tu ametekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa mafanikio  makubwa  bali ameleta  mapinduzi katika  sekta  ya miundombinu kote nchini.

Amempongeza Mhe. Mchengerwa kwa kusimamia utekelezaji wa miradi  yote   kwa kiwango  cha juu huku akitoa wito  kwa maeneo  mengine nchini kuiga utekelezaji huo.

”Ndugu zangu hapa ni vema tuwe wakweli, unaweza ukaletewa  fedha  za maendeleo  lakini ukashindwa kutekeleza lakini,hivyo nampongeza  mbunge wenu kwa kusimamia utekelezaji wa miradi hii ambayo inakwenda kuleta tija kubwa kwa wananchi  katika Wilaya ya Rufiji” amefafanua Mhe. Chatanda

Mbali na  kukagua  miradi  ya Serikali pia ameshuhudia ujenzi wa  nyumba ya mtumishi  wa chama, pia ameshuhudia mradi mkubwa wa ujenzi wa ukumbi wa kisasa  wa wilaya unaogharimu zaidi ya shilingi bilioni 2.5 unaofadhiliwa na Mbunge wa Rufiji Mhe. Mchengerwa kwa kupitia marafiki na wadau mbalimbali.

Akizungumzia kuhusu miradi ya elimu katika wilaya hiyo, Mhe. Chatanda amesema amefurahishwa na kazi nzuri ya ongezeko kubwa la Shule za Msingi na Sekondari na kutoa wito kwa wananchi kuwapeleka watoto wao  katika shule  hizo ili kuunga mkono  maono ya Mhe. Rais ya kuwakomboa wananchi kielimu pia kwa manufaa makubwa ya taifa na vizazi vyao.

Mbunge wa Rufiji Mhe. Mchengerwa  amesisitiza kuwa Serikali imefanya  kazi kubwa ya ujenzi wa shule ambapo amesema  wakati anaingia kwenye ubunge kulikuwa na  na Shule za Msingi 40 tu ambapo sasa kuna shule 63 na upande wa Vituo vya Afya, awali  kulikuwa na vituo 3 na sasa  vimefika 9, huku asimshukuru Mhe. Rais Samia kwa maono makubwa  ya kuwaletea  maendeleo watanzania.

Aidha, Mhe. Chatanda alipotembelea  na  kukagua  ukarabati wa hospitali ya Wilaya  ya Rufiji na ujenzi wa kichomea taka  katika eneo la Utete  uliogharimu  takribani  milioni 900  na kuwataka  wananchi kutumia  huduma hizo ikiwa ni pamoja na wanaume kuwa msitari wa mbele kuwapeleka wake zao  kwenye  huduma za kliniki ili kujua afya za wenza wao na watoto.

Akizungungumzia kuhusu ukatili wa kijinsia, amewataka wazazi  kuwalea watoto wao katika misingi maadili  ili waweze kuja  kuwa wazazi  bora badala ya kuwaacha  kujifunza kwenye  mitandao.

Wakati huo huo ametoa wito  kwa wananchi  kujitokeza kwa wingi kujiandikisha  na kupiga kura huku akisisitiza  kuchagua CCM kwa kuwa ndicho  chama kilichowaletea  maendeleo.