Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), amelihakikishia Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) kwamba Serikali itashirikiana na Sekta Binafsi katika kuharakisha maendeleo ya nchi pamoja na kutenga kiasi kikubwa cha bajeti ya mwaka ujao wa fedha kwa ajili ya kupunguza makali ya kupanda kwa gharama za maisha ya wananchi.

Dkt. Nchemba amesema hayo jijini Dodoma, alipokutana na timu ya wataalamu kutoka  Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), ikiongozwa na Mshauri wa Uchumi na Fedha anayesimamia Idara ya Afrika kwenye Shirika hilo, Bw. Charambos Tsangarides.

Timu hiyo ipo nchini kwa ajili ya kufanya tathimini ya hali ya uchumi na kisera, ikiwa ni hatua ya utekelezaji wa mpango wa Shirika hilo wa kuipatia Tanzania mikopo na misaada zaidi ya kutekeleza miradi ya maendeleo, baada ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan, kukutana na kuzungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika hilo Bi. Kristalina Georgieva, Jijini Washington, Marekani, hivi karibuni.

“Miongoni mwa mambo waliyoafikiana ni kutuma Timu kuja hapa nchini ili kuona namna tutakavyoshirikiana kutengeneza sera mpya za kifedha zitakazosaidia kufufua uchumi kutokana na madhara ya UVIKO 19 pamoja na vita inayoendelea baina ya Urusi na Ukraine” Alifafanua Dkt. Nchemba

Dkt. Nchemba alisema kuwa maelekezo ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Bajeti ijayo, ni kwamba fedha nyingi zaidi zitaelekezwa katika sekta zinazozalisha kwa wingi ikiwemo kilimo, mifugo, uvuvi na kuwaendeleza wafanyabiashara wadogo wadogo ili kuchochea uchumi na ajira. Wakati huo huo sekta za kijamii zitaendelezwa ili kulinda rasilimali watu.

 “Hatua hii itasaidia kufufua na kuimarisha uchumi wetu lakini pia itakuza ajira kwa kuimarisha kilimo cha umwagiliaji, uchumi wa buluu, kutekeleza mpango wa kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara (blueprint), kuongeza mnyoyoro wa thamani wa mazao na kuimarisha shughuli za utalii” alisema Dkt. Nchemba

Kwa upande wake Mshauri wa masuala ya uchumi na fedha na kiongozi wa ujumbe wa IMF, Bw. Charalambos Tsangarides, alisema kuwa timu yake itaangalia uhimilivu wa Deni la Taifa pamoja na Sera mbalimbali ambazo zikiboreshwa zitaleta tija katika kuinua uchumi wa nchi.

Aidha, Bw. Tsangarides alishauri kuwa program inayoandaliwa inalenga kuongeza uwezo wa kifedha kwa Tanzania ili kuchochea ukuaji wa uchumi na kulinda sekta za kijamii kama vile afya, elimu, maji, pamoja na kuboresha rasilimali watu na kuendeleza sekta binafsi.

 

Timu hiyo ya wataalam itakuwepo hapa nchini kwa muda wa majuma mawili ambapo itakutana na wataalam kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Benki Kuu ya Tanzania na wadau wengine mbalimbali.

Share To:

Post A Comment: