NA HERI SHAABAN


MBUNGE wa Jimbo la SEGEREA Bonah Ladslaus Kamoli ,kwa kushirikiana na wadau wa elimu wametoa taulo za kike kwa wanafunzi wa Shule za Sekondari Jimbo la segerea katika mikakati yake ya kukomboa watoto wa kike kupata elimu .


Katika kampeni hiyo endelevu kwa Sekondari 16 Jimbo la segerea za kutoa taulo za kike, Mbunge Bonah alikabidhi taulo za kike shule ya Sekondari Ilala na wadau wa elimu wa kuzalisha taulo za kike kutoka Kampuni ya Parpetual Material ya Dar es Salaam.


Akikabidhi taulo hizo kwa niaba ya Mbunge wa Jimbo la SEGEREA Katibu wa Mbunge Lutta Rucharaba amesema, ofisi ya Mbunge wa Jimbo la segerea imegawa taulo za kike shule za Sekondari Majani ya chai ,Minazi Mirefu na Ilala .


Lutta alisema Ofisi ya Mbunge itaendelea na jitihada za kuhakikisha kwamba, shule zote za jimbo la Segerea zinafikiwa na wanafunzi wanapata taulo za kike kwani ni lengo mahususi la Mbunge Bonah ,kuona kwamba wanafunzi wote hususan wanafunzi wa kike wanahudhuria masomo bila kikwazo chochote.


Lutta alisema , ugawaji wa taulo za kike kwa wanafunzi wa shule za jimbo la Segerea ni mkakati wake mbunge wa jimbo, Mheshimiwa Bonah Kamoli, kwa kutambua yeye ni mwanamke na kubwa zaidi akikumbuka  mazingira ya yeye mwenyewe aliyopitia wakati akiwa shuleni. 


"Ugawaji wa taulo za kike kwa wanafunzi wa shule za jimbo la Segerea ni mkakati wake mbunge  Bonah, kwa kutambua yeye ni mwanamke, ametoka familia ya chini na akimumbuka mazingira ya yeye mwenyewe wakati akiwa shuleni" alisema  Lutta .


Aidha aliongeza kuwa zoezi la ugawaji wa taulo za kike kwa wanafunzi wa shule za jimbo la Segerea ni endelevu kwani tayari Mbunge wa Jimbo la Segerea, ameshagawa taulo za kike kwa wanafunzi wa shule mbalimbali, na leo imekuwa ni zamu ya shule za sekondari Ilala, Minazi mirefu na Majani ya Chai), na pia hivi karibuni tutakwenda kugawa katika shule za sekondari za Binti Musa na Vingunguti.


Kwa upande wake Afisa Masoko kutoka Parpetual Material Limited ambao ni wazalishaji wa taulo za kike za Girlpro,  Salma Muya alisema, wameamua kushirikiana na ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Segerea ili kuweza kugawa taulo za kike kwa wanafunzi kwa kutambua kuwa wanafunzi wa kike wanapitia changamoto nyingi hivyo wanahitaji kusaidiwa waweze kutimiza ndoto zao na kuinuka kitaaluma huku akiahidi kuwa wako tayari kuendelea kutoa msaada huo kwa shule nyingine jimboni humo.


Kwa upande wake Mwanafunzi  Aisha Mohamed wameeleza furaha yao mara baada ya kupokea msaada wa taulo hizo kwa kuyaomba mashirika ya serikali na yasiyo ya serikali kuendelea kuwakumbuka huku wakitoa ombi la kuomba kupunguzwa kwa bei ya taulo za kike ili wanafunzi wengi wakiwemo kutoka familia duni waweze kuzipata kiurahisi.


Aidha wanafunzi hao wametoa shukrani zao kwa ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Segerea na Kampuni ya Parpetual Material Limited na kusema kuwa inatia faraja kuona kuna makundi ya watu na jamii yanawafikiria wao na kuwakumbuka pasi na wao kujua na kuongeza kuwa, msaada wa pedi waliopata utaongeza chachu chachu ya mahudhurio shuleni na hatimaye kuinua kiwango cha taaluma.


Ofisi ya Mbunge Jimbo la Segerea iko katika zoezi endelevu la kuzifikia shule zote za jimbo hilo na kuwapatia wanafunzi wa kike taulo za kike kwa lengo la kuongeza mahudhurio ya wanafunzi na kukuza kiwango cha taaluma katika shule za jimbo hilo.



Mwisho

Share To:

JUSLINE

Post A Comment: