Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula amesema kaya 18 zilizokataa kuondoka kongoji cha Uvinze kilichopo ndani ya hifadhi ya Saadan Bagamoyo zitafanyiwa tathmini na timu ya watalamu wa Kisekta, Mkoa na Wilaya.

Hatua hiyo inafuatia wananchi wa Kaya hizo kugoma kuondoka eneo la hifadhi ya Saadan kwa  maelezo kuwa hapo ni asili yao na njia yoyote ya kulazimishwa kuondoka kunawafanya kupoteza asili yao ambayo baba na babu zao waliishi hapo.

Tayari baadhi ya Kaya zimeondoka zimeondoka eneo hilo la hifadhi ya Taifa ya Saadan baada ya kufanyiwa  uthamini na kulipwa fidia.

Timu ya Mawaziri wa Wizara za Kisekta ikioongozwa na Mwenyekiti wake Dkt Angeline Mabula iliruka kwa Helikopta kujionea kaya zilizopo ndani ya hifadhi ya Taifa ya Saadan ikiwa ni njia ya kutafuta ufumbuzi wa migogoro ya matumizi ya ardhi katika vijiji 975.

Mawaziri walioko kwenye ziara hiyo itakaowafikisha pia mikoa ya Morogoro, Arusha, Mara, Kigoma na Mbeya mbali na Waziri mwenye dhamana ya Ardhi ni Naibu Waziri wa Uvuvi na Mifugo Abdalah Ulega, Mery Masanja Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii pamoja na Hamis Chilllo waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira. Pia katika ziara hiyo wapo Makatibu Wakuu wa wizara za kisekta na wataalamu kutoka wizara hizo.

Akizungumza na wananchi wa kijiji cha Saadan Kitongoji cha Uvinje ambacho kaya 18 ziko ndani ya hifadhi ya Taifa ya Saadan tarehe 24 Machi 2022, Waziri Dkt Mabula alisema wataalamu wa Kisekta, mkoa na Halmashauri ya wilaya ya Bagamoyo watapita kufanya tathmini uwandani katika kijiji hicho.

‘’Taratibu zote zitafanyika tukiondoka hapa tutaacha wataalamu watafanya tathmini na kama mtabaki au mkindoka mtaambiwa na lolote litakaloamuliwa baada ya tathmini tunaomba ushirikiano wenu na hakuna sehemu serikali inatumia mabavu’’ alisema Dkt Mabula.

Baadhi ya wakati wa kaya hizo 18 waliueleza ujumbe wa Mawaziri wa Wizara za Kisekta kuwa, uamuzi wa kuhamishwa eneo wanaloishi la Saadan Bagamoyo hauzingatii misingi ya haki kwa kuwa wameishi eneo hilo kwa muda mrefu tangu mababu na baba zao.

Walisema wananchi wa kijiji hicho wamekuwa wakitambulika na kushiriki shughuli zote zikiwemo za uchaguzi kwa muda mrefu hivyo wanashangazwa na suala la kutakiwa kuondoka.

‘’ Uamuzi wa kutuhamisha hapa lazima uende sambamba na sababu za wao kuhama na kuelezwa pia umbali wa kitongoji chao na hifadhi ya Taifa ya Saadan kwa lengo la kuelewa uingiaji wao kwenye hifadhi’’ alisema Rajabu Abdallah.

Kwa upande wake Merry Masanja, Naibu Waziri wa Malisili na Utalii aliwaambia wananchi hao kuelewa kuwa sheria ya Tanzania inaeleza wazi kuwa, umiliki wa ardhi si wa mtu yeyote na unapohitajika wakati wowote na serikali unachukuliwa lakini kinachoangaliwa ni haki za binadamu.

Naye Naibu Waziri wa Uvuvi na Mifugo Abdallah Ulega aliwaelezea wakazi hao kuwa suala la wananchi kuhama eneo moja kwenda lingine ni la kawaida kwa kuwa hata Mtume Muhammad pamoja na kuzaliwa mji mtakatifu wa Maka lakini alihamia Madina na kuacha kila kitu na  kuwataka  wakazi hao kutafakari msimamo wao kwa kuzingatia pia masuala ya imani ya dini.

Timu ya Mawaziri wa Wizara za Kisekta ipo katika ziara ya kutembelea maeneo yenye migogoro ya matumizi ya ardhi kwa ajili ya kupeleka mrejesho wa maamuzi ya Baraza la Mawaziri kuhusiana na migogoro ya matumizi ya ardhi katika vijiji 975.
Share To:

Post A Comment: