NA HERI SHAABAN, ILALA


Kampuni ya Udalali ya Ama'z imetimiza mwaka mmoja tangu ilipoanzishwa na kuandaa bonanza maalumu la soka ambapo timu ya vijana wa Camp imeibuka mshindi baada ya kuifunga timu ya Noah mabao 6 katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Jakaya Kikwete.


Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Dawa Jumanne, alisema bonanza hilo ni sehemu ya kampuni hiyo kusherehekea mwaka mmoja tangu ilipoanzishwa mwaka jana.  


Alisema kampuni hiyo ilianza kwa kutoa huduma ya udadali lakini sasa inatoa huduma nyingine kama ya usafi na kwamba anatarajia kuanzisha timu ya mpira na tayari ameanza kuwaandaa vijana.


"Tunamshukuru Mungu tunapoadhimisha mwaka mmoja tunajivunia tunakwenda vizuri na sokoni tumepokelewa vizuri, nina ndoto kubwa ya kufanya vitu vingi hivyo Serikali, taasisi mbalimbali na wananchi kwa ujumla watarajie huduma bora kutoka kwetu," alisema Dawa.


Naye Mratibu wa mashindano hayo, Rashidi Msangi, alisema yalikuwa na lengo la kusherehekea kutimiza mwaka mmoja na kujenga afya kwani mazoezi husaidia kuepuka magonjwa mbalimbali hasa yasiyo ya kuambukiza.


Mgeni rasmi katika mashindano hayo Naibu Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, Saady Khimji, ameipongeza kampuni hiyo kwa kubuni mbinu ya kujenga afya za wafanyakazi wake kwa kuandaa mashindano hayo na kuzitaka kampuni zingine kuiga.

Share To:

Post A Comment: