Na. Tito Mselem Pwani,


Imeelezwa kuwa, mahitaji ya Madini ya Kaolin katika viwanda vilivyopo nchini ni tani 120,000 kwa mwaka lakini uzalishaji wa madini hayo ni kati ya tani elfu 70 mpaka elfu 80 kwa mwaka ambapo  kuna upungufu wa tani elfu 40 zinazotakiwa kuzalishwa ili kukidhi mahitaji ya viwanda vya ndani.


Hayo yamebainishwa na Waziri wa Madini Doto Biteko Novemba 15, 2021 baada ya kutembelea eneo la uchimbaji wa madini hayo linalomilkiwa na Kampuni ya Pugu Kaolin Mines Limited lililopo kata ya Kimani wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani. 


Waziri Biteko amesema, eneo hilo lina utajiri mkubwa wa madini ya Kaolin ambayo ni bora duniani na linakisiwa kuwa na takribani tani milioni 800 za madini hayo ambazo ni nyingi na haziwezi kumalizwa kwa haraka. 


Kampuni ya Pugu Kaolin Mines Limited imezuiliwa na Wakala wa Misitu Tanzania (TSF) kuendelea kufanya shughuli za uchimbaji wa madini hayo toka mwaka 1997 baada ya kuonekana kuwa eneo hilo lipo ndani ya Hifadhi ya Misitu.


Aidha, Biteko amesema kuwa baadhi ya maeneo ya uchimbaji yako kwenye hifadhi za misitu lakini kuna taratibu ambazo zinapaswa kufuatwa ili kufanya shughuli za uchimbaji wa madini.


"Kikubwa kinachotakiwa ni utaratibu ufuatwe, kuna migodi mingi ikiwemo Geita Gold Mine, Kabanga Nikel, Tulawaka na mingine mingi ipo ndani ya Hifadhi ya Misutu lakini shughuli za uchimbaji wa madini zinaendela cha msingi ni kufuata taratibu,” amesema Waziri Biteko.


Waziri biteko amesema hakuna Sheria inayozuia kufanya shughuli za uchimbaji wa madini kwenye Hifadhi ya Misitu isipokuwa kuna Sheria inayozua kufanyika shughuli za uchimbaji kwenye Hifadhi za TANAPA za Wanyamapori lakini sio kwenye Hifadhi za Misitu.


Waziri Biteko amesema Serikali inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan imelenga kukuza uchumi wa viwanda ambapo amesema uchimbaji wa madini ya Kaolini yatasaidi kuongeza malighafi za viwanda na kukuza uchumi wa viwanda.


Aidha Waziri Biteko amesema Serikali itatoa majibu endapo kama kampuni hiyo ifanye shughuli za uchimbaji ama la baada ya Wakala wa Hifadhi ya Misitu wilayani Kisarawe kutaka kampuni hiyo isifanye shughuli za uchimbaji ndani ya hifadhi hiyo kuepuka uharibifu wa mazingira.


"Haiwezekani kamati mbalimbali zinakuja kwa ajili ya suala hili, wanalipana posho na suala halifiki mwisho, viongozi wengi wemekuja lakini bado suruhisho halijafikiwa, lazima jambo hili lifike mwisho kama hii biashara hatuwezi  tusema  na kama inawezekana tulimalize ili kazi ianze," amesisitiza Waziri Biteko.


Naye, Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe Nickson Simon amesema kuwa, uongozi wa wilaya hiyo unasubiri tamko ili kujua hatma ya eneo hilo kwani mbali ya kuingiza mapato ya Serikali pia litatoa ajira kwa vijana wa eneo hilo.


Simoni amesema ni vizuri suala hilo likafika mwisho ili eneo hilo liweze kutumika kwa ajili ya kuleta maendeleo ya wananchi na yatolewe maamuzi ambayo yatakuwa na manufaa kwa pande zote.


Kwa upande wake , Afisa Mazingira Wilaya ya Kisarawe Douglas Mwela amesema, wilaya hiyo ina migodi sita ya machimbo ya Madini ya Kaolini ambapo kwenye bajeti ya Mwaka 2019/2020 Madini hayo yaliingizia Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe kiasi cha shilingi milioni 270 na mwaka 2020/2021 yaliingiza milioni 288 ambapo madini hayo yanatumiwa zaidi na kiwanda cha Keda cha Chalinze na Mkuranga vya kuzalisha marumaru. 


Mwela amesema hadi robo ya pili ya bajeti ya Mwaka 2021/2022 tayari wamekusanya kiasi cha shilingi milioni 99 na mgodi huo ulikuwa chini ya Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) na uzalishaji ulikoma tangu mwaka 1997.


Madini ya Kaolin yanatumika kutengeneza marumaru, karatasi, kuchangangwa kutengeneza vidonge, rangi, vyombo vya udongo, vipodozi pamoja na dawa za mswaki.


Mbali na Kisarawe Madini ya Kaolin pia yanapatika Mgeta wilayani Mvomero Mkoani Morogoro pamoja na Malangali mkoani Iringa.

Share To:

Post A Comment: