Malkia wa Muziki wa Injili hapa nchini Rose Mhando 
Katibu Mkuu wa Umoja wa Muziki Tanzania (TAMUFO) Stella Joel, ambaye pia ni muimbaji wa muziki wa injili.
Muimbaji wa muziki wa injili, Christopher Mwahangila
Muimbaji wa muziki wa injili, Faraja Ntaboba.
Muimbaji wa muziki wa injili, Bony Mwaitege.
Muimbaji wa muziki wa injili, Upendo Nkone
 


Na Dotto Mwaibale, Arusha


WANAMUZIKI wakali wa Muziki wa Injili hapa nchini wanatarajia  kulitikisa jiji la Arusha na vitongoji vyake kwa kutoa burudani kali katika Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Muziki Duniani ambayo Kitaifa yatafanyika Oktoba 1, 2021.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa leo Katibu Mkuu wa Umoja wa Muziki Tanzania (TAMUFO) Stellah Joel alisema siku hiyo Wana Arusha na vitongoji vyake wategemee kupata burudani kali kutoka kwa wakali hao wa muziki wa injili.

" Maandalizi ya maadhimisho hayo yanaendelea vizuri tunamshukuru Mungu na sasa tunaendelea kumalizia kufanya mazungumzo na wanamuziki mbalimbali ambao wanataka kuja kushiriki," alisema Joel.

Alisema Malkia wa Gospo hapa nchini Rose Mhando ni kati ya wanamuziki wa injili ambaye ataongoza kuiamsha Arusha kwa burudani katika maadhimisho hayo ambayo kwa mara ya kwanza yanafanyika hapa nchini.

 Aliwata baadhi ya wanamuziki wengine wa muziki huo waliothibitisha kushiriki kwenye maadhimisho hayo kuwa ni Bony Mwaitege,Upendo Nkone, Amani Mwasote kutoka Mbeya, Jane Miso,  Mzungu Four, Edson Mwasabwite,Christopher Mwahangila, Faraja Ntaboba,Neema Jekonia, Joyce Ombeni, Enock Jonas na wengine wengi.

Joel alitumia nafasi hiyo kutoa shukurani zake kwa Serikali Mkoa wa Arusha, Mkurugenzi wa jiji la Arusha, Mstahiki Meya, Idara ya Utamaduni jiji la Arusha, Baraza la Sanaa la Tanzania (BASATA) Uongozi wa Hoteli ya Kitalii ya Kibo Palace, Waandishi wa Habari na wadau wa muziki wakiwemo wanamuziki wa kada mbalimbali wa Arusha kwa ushirikiano ambao wanaendelea kuutoa ili kufanikisha maadhimisho hayo.

Kwa mawasiliano zaidi kuhusu maadhimisho hayo piga kwa Stella Joel Mratibu na Katibu Mkuu TAMUFO, 0756 846166.

Share To:

dotto mwaibale

Post A Comment: