Na Mwamvua Mwinyi, Kibaha
Wanawake wa UWT Kibaha Mjini ,mkoani Pwani wanatarajia kuondokana na changamoto ya ukosefu wa soko la uhakika mara baada ya kukamilika.kwa ujenzi wa jengo la duka maalum la kuuzia bidhaa zao.

Ujenzi wa duka hilo unatarajia kukamilika wakati wowote mwaka huu na unatarajia kugharimu milioni 70 ,pamoja na hilo umoja huo umeanzisha darasa la ujasiriamali ili kutoa elimu kwa akinamama.

Mwenyekiti wa UWT Kibaha mjini, Elina Mgonja ,aliyaeleza hayo katika kongamano lililoandaliwa na UWT Kibaha Mjini, kupongeza siku 100 na hotuba aliyoitoa Rais Samia kwa wanawake pale Dodoma, Juni 8 mwaka huu.

Alisema ,tatizo kubwa kwa wanawake wajasiliamali ni soko hivyo wanaamini duka hilo litawezesha kupeleka biashara zao na kuuzika huku wakijiinua kiuchumi.

Aliomba wadau mbalimbali kujitokeza kuunga mkono ujenzi huo uweze kukamilika haraka.

Hata hivyo ,Mgonja aliwaasa wanawake wamuunge mkono Rais Samia kwa kazi kubwa ambayo ameanza kuionyesha ndani ya siku 100 kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alisema, maelekezo yaliyotolewa Dodoma kupitia mkutano wa wanawake wao wanafanya kwa vitendo na kumhakikishia mwenyekiti wa CCM Taifa kuwa wataendelea kumshika mkono mwanamke wa Kibaha ili kujiinua kimaendeleo.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Kibaha, Sara Msafiri ambae alimwakilisha mkuu wa mkoa wa Pwani ,Aboubakar Kunenge ,Sara aliitaka UWT kuandaa dawati la kusikiliza malalamiko ya akinamama kuhusu mirathi na ndoa ili awasaidie upande wa wanasheria.

Pia alieleza vikundi vya ujasiriamali hufa kutokana na kukosa mshikamano ,amewapongeza wilaya hiyo kuwa na Umoja na mshikamano.

Nae mbunge wa viti maalum mkoani Pwani ,Subira Mgalu alimpongeza Rais Samia, kwa bajeti ya kwanza kupitishwa bungeni kwa asilimia kubwa,huku akishukuru majimbo kupokea milioni 500 kila jimbo ambapo Pwani imeshapokea bilioni 4.5 kwa majimbo Tisa.

Pia imetolewa bilioni 100 ili kukamilisha maboma ya vituo vya afya 1,500 nchini na zahanati hatua ambayo inahitaji pongezi.

Makamu mwenyekiti wa halmashauri ya Mji wa Kibaha ,Selina Wilson alisema, kwa kutambua vikundi vya ujasiriamali, halmashauri imetoa milioni 600 ndani ya miezi sita ikiwa ni asilimia 60 kwa mikopo ya akina mama.
Share To:

Post A Comment: