UTAFITI  wa mradi wa Magadi soda katika bonde la Engaruka wilayani Monduli mkoani Arusha umegharimu shilingi bilioni 6 huku ukitarajiwa kuokoa fedha nyingi zinazotumika kuagiza magadi soda nje ya nchi.

Hayo yameelezwa leo jijini Dar es Salaam  na Kaimu  Mkurugenzi wa Mwendeshaji wa Shirika la Taifa la Maendeleo ( NDC), Rhobi Sattima akipokea ripoti ya upembuzi yakinifu ya utafiti uliofanywa na Shirika la Maendeleo na Utafiti wa Viwanda (TIRDO.)

Sattima alisema utafiti wa awali ulifanyika mwaka 2008, ambapo NDC kwa kushirikiana na wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) ilifuatiwa na Utafiti wa kina uliofanyika mwaka 2010- 2013 ambapo umeonyesha kuwepo kwa magadi ya kutosha na kushauriwa ufanyike upembuzi yakinifu  kwa ajili ya kujenga kiwanda.

Alisema kazi ya upembuzi yakinifu ulihusisha kuhakiki wingi wa magadi soda yaliyopo, tathmini ya masoko ndani na nje ya nchi, tathmini za kimazingira, tathmini ya Miundombinu inayohitajika na kufahamu gharama za ujenzi wa kiwanda pamoja na teknolojia Bora ya kuvuna magadi soda.

"Kwa sasa nchi yetu inaagiza magadi soda toka nje ya nchi kwa takribani Dola za Marekani Milioni 12 kwa mwaka, kwa ajili ya shuguli mbali mbali ikiwemo kuchenjua baadhi ya madini, Viwanda vya karatasi, Viwanda vya kutengeneza dawa za Binadamu na wanyama," alisema Sattima.

Kwa upande wa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Maendeleo la Utafiti wa Viwanda (TIRDO), Profesa  Mkumbukwa Mtambo alisema baada ya utafiti wamebaini magadi yaliyopo katika tabaka la udongo yana madini mengi ya Sodium bicarbonate na Sodium Carbonate.

" Sampuli zilizochukuliwa zinaonyesha madini ya bircarbonste gramu 12.0 mpaka gramu 25.49 kwa lita na madini ya sodium carbonate gramu 125.93 mpaka 245.92 kwa lita." alisema Profesa Mtambo.

Kuhusu soko, Profesa Mtambo alisema kwa makisio ya uzalishaji wa magadi soda katika bonde hilo la Engaruka ni tank 500,000 kwa mwaka na kwamba uzalishaji unaweza kuongezeka hadi tank 1,000,000  ambapo utaweza kukidhi mahitaji ya soko la ndani kwa asilimia 13 mpaka asilimia 30 kufikia mwaka 2030  na soko la nje asilimia 87.

Share To:

Post A Comment: