Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Selemani Jafo ametoa msisitizo katika suala la usafi na utunzaji wa mazingira Jijini Arusha leo Mei 23, 2021 alipokuwa katika ziara ya kikazi. Jafo ametoa msisitizo huo alipotembelea eneo la dampo kuu lilalotumika kuhifadhi taka ngumu. 


Katika ziara hiyo Waziri Jafo ametoa wiki mbili kwa uongozi wa Jiji hilo kuhakikisha hali ya taka zilizosambaa hovyo katika dampo hilo kukusanywa vizuri kinyume na hali ilivyo sasa ambapo uchafu umeoneka kusambaa hovyo katika dampo hilo. 


Meneja Msimamizi wa dampo  hilo Bw. Marko Chacha amejitetea kwamba hali hiyo imetokana na kushindwa kufanyakazi ipasavyo kwa mitambo ya kushindilia taka kutokana na mvua. 


Hata hivyo Jafo hakuridhishwa na utetezi wa Afisa huyo kwani Manispaa ya Moshi ambao wapo jirani kabisa na Jiji la Arusha wameweza kusimamia vyema dampo lao na kuwezesha uchafu wote kudhibitiwa vyema ndani ya dampo. Kutokana na hali hiyo Jafo ametoa wiki mbili ili hali hiyo irekebishwe ipasavyo. 


Katika hatua nyingine Jafo amefanya ziara eneo la machimbo ya kifusi ya Isongo ambapo siku za hivi karibuni kulitokea maafa ya watu watatu kufariki na wengine kujeruhiwa kutokana na kudondokewa na kifusi cha udongo. 


Katika eneo hilo Waziri Jafo amemuagiza Meneja wa NEMC Kanda ya Kaskazini ndugu Lewis Nzali kukutana na Afisa anayesimamia sekta ya Madini wa Kanda hiyo ili waone namna bora ya uchimbaji wa madini kwa kuzingatiwa suala la utunzaji wa mazingira.

Share To:

msumbanews

Post A Comment: