Kaimu Afisa Vijana  Mkoa wa Singida Frederick Ndahani.
Mwanaharakati wa masuala ya kijamii  Mkoa  wa Singida, Stella Mwagowa
Afisa Mtendaji wa Kata ya Dung'unyi  wilayani  Ikungi mkoani hapa, Yahaya Njiku.
 


Na Dotto Mwaibale, Singida


 VIJANA mkoani hapa wamepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za  kifo cha Rais Dkt. John Magufuli kilichotokea Jana. 

Akizungumza na waandishi  wa habari mkoani hapa jana kwa niaba ya vijana hao Kaimu Afisa Vijana  Mkoa wa Singida Frederick Ndahani alisema   watamkumbuka  Rais Magufuli kwa kuwafundisha  kuwa wazalendo wa Taifa letu.

"  Vijana na  baadhi ya watanzania tulikosa uzalendo lakini Magufuli akatuhasa na kutusihi tuwe wazalendo."  alisema Ndahani.

Ndahani alisema kuonesha jinsi  alivyo  kuwa akiwapenda  vijana  alitoa  nafasi nyingi za uongozi  wakiwemo wakuu wa wilaya, mikoa na baadhi  yao  aliwateua  kuwa  mawaziri.

Alisema aliwateua vijana kwa sababu aliamini wanao uwezo wa kusimamia mambo kwa uchungu kwa kuwa wao ni nguvu ya Taifa.

Aidha Ndahhani  alisema  Rais Magufuli  amefariki akiwa ametujengea uchumi wa viwanda na kutufikisha katika uchumi wa kati sambamba na elimu bure kwa wanafunzi wa shule ya msingi na Sekondari.

Alisema kwa niaba  ya  vijana wa  mkoa  huu wanatoa pole kwa Makamu wa Rais Samia Suluhu, Rais wa Zanzibar, Waziri Mkuu, Wabunge, viongozi wote na watanzania wote kwa msiba huu mkubwa na kuwa  wanamuomba mrithi wake  Mungu amjalie aendeleze yale yote mazuri aliyoyacha.

Mwanaharakati wa masuala ya kijamii kwa ujumla mkoani hapa Stellah Mwagowa alisema  Rais Magufuli aliwaaminisha  vijana kuwa wanaweza kwani  hapo awali hawakuweza kudhubutu kujitokeza kugombea nafasi za uongozi katika chaguzi mbalimbali.

"Magufuli alijenga misingi kwa vijana kugombea nafasi mbalimbali  ambapo katika Bunge la 12 wapo wengi  tofauti na miaka mingine"alisema Mwagowa.

Afisa Mtendaji wa Kata ya Dung'unyi  wilayani  Ikungi mkoani hapa, Yahaya Njiku alisema Rais Magufuli ametuachia alama na vitu ambavyo tutakapo kuwa tunaviangalia hatutaweza kumsahau kutokana na kuanzisha miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo bwawa la kufua umeme la Mwalimu Nyerere ambao utawasaidia vijana kupata ajira na wananchi kupata umeme wa uhakika.

Njiku alitaja miradi mingine aliyoianzisha kuwa ni reli ya kisasa,  madaraja makubwa jijini Mwanza na Dar-es-saalamu, kununua vivuko kwa ajili  ya  usafiri wa majini  pamoja  na usafiri wa anga

Share To:

Post A Comment: