Msemaji wa Klabu ya Simba, Hajji Manara akizungumza leo na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam


UONGOZI wa Simba umesema kuwa kuelekea kwenye mchezo wao wa kimataifa wa Ligi ya Mabingwa Afrika, dhidi ya Al Merrikh, Machi 16 hakutakuwa na ruhusa ya mashabiki kuingia kuipa sapoti timu hiyo.

Licha ya kwamba kulikuwa na katazo la mashabiki kwa timu nyingi ambazo zinashiriki Ligi ya Mabingwa Afrika ila kwa Simba walikuwa wanapata kibali cha kuingiza nusu ya mashabiki.

Hii ilikuwa ni kwa sababu ya kuchukua tahadhari ya Virusi vya Corona ambavyo ni janga la dunia.

Leo Machi 13, Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara amesema kuwa wakati wakiwa kwenye maandalizi ya mechi hiyo itakayokuwa na ushindani mkubwa wamepokea taarifa kutoka Shirikisho la Soka Tanzania, (TFF) kwamba hawataruhusiwa kuwa na mashabiki.

“Simba imezoea kucheza bila mashabiki ikiwa nje ya nchi lakini sikumbuki kama hapa nchini tumewahi kucheza bila mashabiki. Tunawaomba radhi mashabiki kwa mechi hii sababu ni maamuzi ya CAF ambao ndio wenye mamlaka ya soka Afrika.

“Tukiwa kwenye maandalizi ya mechi yetu dhidi ya Al Merrikh hapo tulipokea taarifa kutoka TFF kwamba hatutaruhusiwa kuwa na mashabiki, hivyo hii ni taarifa mashabiki wetu watuwie radhi.

“Watakaoruhusiwa kuingia ni watu wachache hasa wale ambao wanahusika na maandalizi ya mechi lakini maandalizi yapo vizuri na tunaamini kwamba kila kitu kitakuwa sawa.

Kwenye mchezo wa kwanza uliochezwa Machi 6, Simba ililazimisha sare ya bila kufungana ikiwa ugenini, ina kazi ya kusaka ushindi kwenye mchezo wa pili ili kuweza kujihakikishia nafasi ya kutinga robo fainali.

Kibindoni kwenye kundi A ina pointi 7 inakutana na Al Merrikh ikiwa na pointi moja.
Share To:

Post A Comment: