Jeshi la Polisi Mkoa wa Morogoro, linamshikilia Shinje Njilangila (30), mkazi wa Kijiji cha Mbamba, wilayani Kilosa kwa tuhuma za mauaji ya shemeji yake Dotto Ngembe (28), kwa kumchoma na kitu chenye ncha kali.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Wilbroad Mutafungwa, alisema tukio hilo lilitokea usiku wa kuamkia Agosti 12 baada ya Ngembe kuingilia mgogoro wa kimahusiano uliozuka baina ya mtuhumiwa na mkewe, Kulwa Ngembe, ambaye ni dada wa marehemu.

Kamanda Mtafungwa alisema mauaji hayo yalitokea nyumbani kwa marehemu ambaye alikuwa amewaita wanandoa hao kwaajili ya kusuluhisha ugomvi uliokuwa ukiendelea baina yao, ndipo mtuhumiwa alipomshambulia shemeji yake hadi kumsababishia umauti.

“Chanzo cha tukio hili mtuhumiwa alimfuata mkewe nyumbani kwa shemeji yake kwaajili ya usuluhishi, lakini ilipofika majira ya saa sita usiku ndipo alipofanya mauaji kwa kaka wa mke wake aliyekuwa akimtuhumu kuwa ndio chanzo cha mgogoro wao na baada ya kutekeleza mauaji hayo alikimbia mafichoni,” alisema Mtafungwa.
Share To:

Post A Comment: