WABUNGE wameitaka Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) kushughulikia tatizo la baadhi ya madiwani kutokulipwa posho kwa zaidi ya miezi 11.

Walisema hayo wakati wa mjadala wa  taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka ulioshia Juni 2019.

Wakati wa michango yao, baadhi ya wabunge walisema wapo madiwani ambao hawajalipwa posho zao hadi leo wakati baadhi wakielekea kuvunja mabaraza ya madiwani kutokana na Uchaguzi Mkuu Oktoba.

Mbunge wa Viti Maalumu, Konchester Rwamlaza (Chadema) alihoji kuhusiana na baadhi ya madiwani kutokupata posho zao kwa wakati huku akidai kwamba wana zaidi ya miezi 10 hawajalipwa.

“Posho za madiwani hadi sasa hivi madiwani wana zaidi ya mwaka hawajalipwa posho, kwa kweli tunawanyanyasa, ni kwanini madiwani wanatendewa hivyo, nina wasiwasi kama wameshindwa kulipwa hata vikao havikai.

“Unajiuliza halmashuri hizi zinajiendeshaje, watasimamiaje wakati wao wamekaa kilofalofa, nina wasiwasi wanaweza hata wasipewe kiinua mgongo chao, kule hawalipwi, hata ukienda Kyelwa wana zaidi ya miezi 11 hawajalipwa,” alisema Konchester.

Mbunge wa Viti Maalumu, Marry Chatanda (CCM) aliiomba Tamisemi kuwalipa posho madiwani kwani maisha yao yamezidi kuwa magumu.

“Halmashauri ya Korogwe imeshindwa kuwalipa madiwani posho zao, madiwani walikatiwa bima lakini wameshindwa kupata fedha kwa ajili ya kulipia bima hizo.

“Niiombe Tamisemi halmashauri  kama hizi zifuatiliwe kwa karibu, mabaraza yanavunjwa, hawa madiwani ambao hawakulipwa hizo posho, tuiombe Tamisemi jambo hili iliangalie, sio jambo jema kwetu kwani viongozi wenzetu wanateseka,” alisema Chatanda.

Mbunge wa Nanyama, Abdallah Chikota (CCM) ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya LAAC, aliiomba Ofisi ya Rais itoe vitendea kazi, iongeze watumishi kuwe na ajira kwa wahandisi wa ujenzi katika halmashauri nchini.
Share To:

Post A Comment: